Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nitaachaje kujiumiza?

Nitaachaje kujiumiza?

Vijana Huuliza . . .

Nitaachaje kujiumiza?

“Singeweza kuzuia mfadhaiko wangu. Kisha nikapata kitu nilichoweza kudhibiti, yaani, uchungu.”—Jennifer, 20. *

“Nilipokasirika nilijikata. Ilikuwa njia yangu ya kulia. Baada ya kufanya hivyo ningefurahi.”—Jessica, 17.

“Sijajikata kwa majuma mawili hivi. Huo ni muda mrefu kwangu. Sifikiri nitaacha kabisa.”—Jamie, 16.

JENNIFER, Jessica, na Jamie hawajuani lakini hali zao zinafanana sana. Wote watatu walikuwa na mfadhaiko wa kihisia. Nao walitumia njia ileile kukabiliana na mshuko-moyo. Jennifer, Jessica, na Jamie walijituliza kwa muda kwa kujiumiza. *

Ingawa linaweza kuonekana kuwa jambo la kushangaza, kujiumiza ambako kunatia ndani kujikata, kumeongezeka sana kati ya vijana. Gazeti la Kanada National Post linasema kwamba zoea hilo “huwaogopesha wazazi, huwatatanisha washauri [wa shule] na hutahini ustadi wa madaktari.” Pia linasema kwamba kujiumiza “kunaweza kuwa mojawapo ya uraibu sugu ambao madaktari wamewahi kukabili.” Je, wewe au mtu fulani ambaye mna uhusiano wa karibu naye amewahi kukabiliana na zoea hilo? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini?

Kwanza, jaribu kuelewa sababu inayofanya utake kujiumiza. Kumbuka, kujiumiza si zoea ambalo husababishwa tu na wasiwasi. Mara nyingi, ni njia ya kukabiliana na aina fulani ya mfadhaiko. Yule anayejikata hutumia uchungu wa kimwili kutuliza uchungu wa kihisia. Kwa hiyo, jiulize: ‘Kwa nini mimi hujiumiza? Mimi hufikiria nini ninapohisi kwamba ninataka kujikata?’ Je, kuna hali fulani katika maisha yako, labda inayohusu familia au marafiki wako, ambayo inakufadhaisha?

Bila shaka, utahitaji ujasiri ili kujichunguza. Lakini kuna manufaa mengi ya kufanya hivyo. Mara nyingi, hiyo ndiyo hatua ya kwanza ya kuacha zoea la kujiumiza. Hata hivyo, unahitaji kufanya mengi zaidi tu ya kufahamu chanzo cha tatizo lako.

Umuhimu wa Kuzungumza na Mtu

Ikiwa una tatizo la kujiumiza, utanufaika ukimweleza rafiki mkomavu na unayemtumaini hisia zinazokuhangaisha. Methali moja ya Biblia inasema: “Wasiwasi moyoni humkosesha mtu raha, lakini neno jema humchangamsha.” (Methali 12:25, BHN) Utapata maneno yenye kufariji na yenye fadhili ukimweleza mtu hisia zako.—Methali 25:11.

Unaweza kuzungumza na nani? Itafaa ikiwa utachagua mtu mwenye umri mkubwa, aliye na hekima, mkomavu, na mwenye huruma. Wakristo wanaweza kupata msaada kutoka kwa wazee wa kutaniko ambao ni “kama mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha mwamba mzito katika nchi iliyochoka.”—Isaya 32:2.

Huenda wazo la kumweleza mtu mwingine siri zako likakuogopesha. Huenda ukahisi kama Sara. Anasema hivi: “Mwanzoni haikuwa rahisi kumtumaini yeyote. Niliamini kwamba watu wakinifahamu kabisa watatoroka kwa sababu ya kuchukizwa na zoea hilo.” Hata hivyo, alipoanza kueleza hisia zake, Sara alianza kuelewa ukweli wa maneno ya Methali 18:24: “Yuko rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.” Anasema hivi: “Wakristo wakomavu ambao niliwaeleza hisia zangu hawakunilaumu, haidhuru niliwaeleza jambo gani kuhusu zoea langu la kujiumiza. Badala yake, walinitolea mapendekezo ambayo ningeweza kutumia. Walinionyesha sababu kutoka katika Maandiko, nao walinitia moyo nilipovunjika moyo na kujihisi kuwa sifai hata kidogo.”

Kwa nini usimweleze mtu tatizo lako la kujiumiza? Ikiwa unahisi kwamba huwezi kuzungumza na mtu uso kwa uso, zungumza kwa kutumia barua au simu. Kumweleza mtu hisia zako kunaweza kukusaidia kupona. Jennifer anasema: “Jambo muhimu zaidi lilikuwa kujua kwamba kulikuwa na mtu aliyenijali kikweli, na kwamba ningeweza kuzungumza naye nilipohisi nimevunjika moyo.” *

Umuhimu wa Sala

Donna alikuwa amegonga mwamba. Kwa upande mmoja, alihisi kwamba alihitaji mwongozo wa Mungu. Kwa upande mwingine, alihisi kwamba Mungu hangemtegemeza hadi aache kujikata. Ni nini kilichomsaidia Donna? Jambo moja lilikuwa kutafakari andiko la 1 Mambo ya Nyakati 29:17, ambalo linasema kwamba Yehova Mungu ni “mchunguzaji wa moyo.” Donna anasema hivi: “Yehova alijua kwamba moyoni nilitaka sana kuacha kujikata. Nilipoanza kumwomba msaada, nilishangaa. Polepole, nilipata nguvu za kushinda tatizo hilo.”

Mtunga-zaburi Daudi, ambaye alipatwa na matatizo mengi, aliandika hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Naam, Yehova anajua kwamba unateseka. Isitoshe, ‘anakujali.’ (1 Petro 5:7) Moyo wako unapokuhukumu, kumbuka kwamba Mungu ni ‘mkuu kuliko moyo wako naye anajua mambo yote.’ Naam, anajua sababu inayokufanya ujiumize na kinachofanya iwe vigumu kwako kuacha. (1 Yohana 3:19, 20) Ukimkaribia katika sala na kujitahidi kushinda zoea hili ‘atakusaidia kwelikweli.’—Isaya 41:10.

Hata hivyo, vipi ukirudia zoea hilo? Je, hilo linamaanisha kwamba umeshindwa kabisa? La hasha! Methali 24:16 inasema hivi: “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.” Akifikiria andiko hilo la Biblia, Donna anasema hivi: “Nilianguka zaidi ya mara saba lakini sikukata tamaa.” Donna aligundua kwamba anahitaji kuendelea kujitahidi. Naye Karen pia alitambua jambo hilo. Anasema hivi: “Nilijifunza kwamba zoea linaporudi, sijashindwa, bali ni kuteleza kidogo tu, na hilo linafanya nijitahidi tena mara nyingi iwezekanavyo.”

Unapohitaji Msaada Zaidi

Yesu alisema kwamba ‘walio wagonjwa wanahitaji tabibu.’ (Marko 2:17) Katika visa vingi ni muhimu kumwona mtaalamu ili kufahamu ikiwa zoea hilo la kujiumiza linasababishwa na tatizo fulani la kiakili au la kihisia, kisha akueleze ni matibabu gani yanayohitajika. * Jennifer aliamua kutafuta msaada kama huo, pamoja na msaada aliokuwa akipata kutoka kwa waangalizi Wakristo wenye upendo. Anasema: “Wazee si madaktari, lakini wamenitegemeza sana. Ingawa tamaa ya kujiumiza huja mara kwa mara, nimefaulu kukabiliana nayo kwa msaada wa Yehova, kutaniko, na mbinu za kukabiliana ambazo nimejifunza.” *

Uwe na uhakika kwamba unaweza kujifunza kukabiliana na hali ngumu kwa njia nzuri zaidi. Sali kama alivyofanya mtunga-zaburi: “Uweke imara hatua zangu katika maneno yako, wala namna yoyote ya jambo lenye kuumiza lisinitawale.” (Zaburi 119:133) Kwa kweli, utapata uradhi na utajiheshimu sana utakapoweza kudhibiti zoea hilo lisiendelee kukutatiza.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Unaweza kufanya nini badala ya kujikata unaposhuka moyo?

▪ Unaweza kuzungumza na nani iwapo una tatizo la kujikata?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina fulani katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 6 Ili upate habari zaidi kuhusu yanayohusika katika kujiumiza na visababishi vyake, ona makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Mimi Hujiumiza?” katika toleo la Amkeni! la Januari 2006.

^ fu. 14 Nyakati nyingine unaweza kuandika hisia zako. Waandishi wa zaburi za Biblia walikuwa wanaume wenye hisia nyingi ambao walitumia maneno kueleza majuto, hasira, kukata tamaa, na huzuni. Kwa mfano, huenda ukataka kusoma Zaburi 6, 13, 42, 55, na 69.

^ fu. 20 Nyakati nyingine kujiumiza husababishwa na magonjwa mengine kama vile kushuka moyo, tatizo la kubadilika-badilika kwa hisia, tatizo la kushindwa kudhibiti mawazo au misukumo, au tatizo la kula. Amkeni! haipendekezi tiba yoyote hususa. Wakristo wanapaswa kuhakikisha kwamba matibabu wanayotumia hayapingani na kanuni za Biblia.

^ fu. 20 Matoleo ya zamani ya Amkeni! yamekuwa na makala ambazo zimezungumzia mambo yanayosababisha kujiumiza. Kwa mfano, ona makala “Kuyaelewa Magonjwa ya Kihisia” (Januari 8, 2004), “Msaada kwa Matineja Walioshuka Moyo” (Septemba 8, 2001), na “Ni Nini Kinachosababisha Matatizo ya Kula?” (Januari 22, 1999), kutia ndani makala “Vijana Huuliza . . . Nawezaje Kukabiliana na Hali Ikiwa Mzazi Wangu Ni Mlevi?” (Agosti 8, 1992) la Kiingereza.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

KUMSAIDIA MTU ANAYEJIUMIZA

Unaweza kumsaidiaje mshiriki wa familia au rafiki ambaye ana tatizo la kujiumiza? Kwa kuwa huenda mtu huyo akahitaji sana mtu wa kuzungumza naye, unaweza kumsikiliza. Jaribu kuwa “rafiki wa kweli . . . aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Huenda ukakasirika mara moja na kumwamuru aache kufanya hivyo mara moja. Lakini huenda kutenda hivyo kukamfanya ajitenge tu. Isitoshe, mengi zaidi yanahitajika kuliko tu kumwambia mtu aache kujiumiza. Unahitaji busara ili kumsaidia mtu anayejiumiza ajifunze njia mpya za kukabiliana na matatizo. (Methali 16:23) Wakati pia unahitajika. Kwa hiyo uwe mwenye subira. Uwe “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.”—Yakobo 1:19.

Ikiwa wewe ni kijana, usifikiri kwamba unaweza kumsaidia mtu anayejiumiza ukiwa peke yako. Kumbuka, anaweza kuwa na tatizo jingine au ugonjwa unaohitaji kutibiwa. Pia, kujiumiza kunaweza kuhatarisha uhai, hata ikiwa anayejiumiza hataki kujiua. Basi, itafaa kumtia moyo mtu anayejikata amweleze jambo hilo mtu mzima mkomavu ambaye anajali.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Usipuuze umuhimu wa kuzungumza na mtu anayekupenda na umuhimu wa sala