Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Sanamu za Kuchorwa Zitumiwe Katika Ibada?

Je, Sanamu za Kuchorwa Zitumiwe Katika Ibada?

Maoni ya Biblia

Je, Sanamu za Kuchorwa Zitumiwe Katika Ibada?

KILA Agosti 15, sherehe kubwa ya kidini hufanywa kwenye kisiwa cha Ugiriki cha Tínos. Maelfu ya watu hukutana ili kumheshimu Maria mama ya Yesu na sanamu yake ya kuchorwa ambayo inaaminika kuwa ina nguvu za kimuujiza. * Kitabu cha marejeo cha Othodoksi ya Ugiriki kinasema: “Tukiwa na imani ya pekee na kujitoa, sisi humheshimu Theotokos Mtakatifu Zaidi, Mama ya Bwana wetu, na kumwomba atulinde, atukinge, na kutusaidia. Sisi hutafuta msaada kutoka kwa Watakatifu wanaofanya miujiza—wanaume na wanawake Watakatifu—kwa ajili ya mahitaji yetu ya kiroho na ya kimwili . . . Sisi hujitoa kabisa kubusu na kuabudu vitu vyao vitakatifu na sanamu zao.”

Watu wengine wengi ambao hudai kuwa Wakristo ni wafuasi wa dini zenye desturi za ibada ya aina hiyo. Lakini je, mafundisho ya Biblia huunga mkono matumizi ya sanamu za kuchorwa katika ibada?

Wakristo wa Mapema

Fikiria mambo yaliyotukia yapata mwaka wa 50 W.K., wakati mtume Paulo alipotembelea Athene, jiji ambalo lilikazia sana matumizi ya sanamu katika ibada. Paulo aliwaeleza Waathene kwamba Mungu “hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono, wala hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote . . . Kwa hiyo, . . . hatupaswi kuwazia kwamba Mungu ni kama dhahabu au fedha au jiwe, kama kitu kilichochongwa kwa ufundi na mtungo wa mwanadamu.”Matendo 17:24, 25, 29.

Kwa kweli, maonyo hayo kuhusu kutumia sanamu yanapatikana mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambayo pia huitwa Agano Jipya. Kwa mfano, mtume Yohana aliwashauri Wakristo hivi: “Jilindeni na sanamu.” (1 Yohana 5:21) Paulo aliwaandikia Wakorintho hivi: “Hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu?” (2 Wakorintho 6:16) Kabla ya kugeuza imani, Wakristo wengi wa mapema walikuwa wakitumia sanamu katika ibada. Paulo aliwakumbusha Wakristo huko Thesalonike jambo hili alipoandika hivi: ‘Mlimgeukia Mungu mkatoka kwenye sanamu zenu ili mmtumikie Mungu aliye hai na wa kweli.’ (1 Wathesalonike 1:9) Ni wazi kwamba, Wakristo wa mapema wangekuwa na maoni kama ya Yohana na Paulo kuhusu sanamu za kuchorwa.

“Wakristo” Wakubali Kutumia Sanamu za Kuchorwa

Kichapo Encyclopædia Britannica kinasema kwamba “katika karne tatu za kwanza za Kanisa la Kikristo, . . . hakukuwa na sanaa ya Kikristo, nalo kanisa lilipinga kabisa kuanzishwa kwa sanaa. Kwa mfano, Clement wa Aleksandria alishutumu sanaa ya kidini (ya kipagani) kwa kuwa iliwatia watu moyo waabudu kitu ambacho kimeumbwa badala ya kumwabudu Muumba.”

Basi ilikuwaje watu wengi wakaanza kutumia sanamu za kuchorwa? Kichapo Britannica kinaendelea kusema: “Karibu katikati ya karne ya tatu, sanaa ya uchoraji ilianza kutumiwa na kukubaliwa na Kanisa la Kikristo lakini kulikuwa na upinzani mkali katika makanisa fulani. Picha zilianza kutumiwa makanisani wakati tu Kanisa la Kikristo lilipokuwa kanisa la serikali ya Roma chini ya Maliki Konstantino mapema katika karne ya nne kisha zikakubaliwa kama zoea la kawaida katika Kanisa la Kikristo.”

Wapagani wengi ambao sasa walianza kujiita Wakristo walikuwa na zoea la kuabudu picha za kuchorwa za maliki. Katika kitabu chake Icon Painting, John Taylor anasema hivi: “Kupatana na ibada ya maliki, watu waliabudu picha yake iliyochorwa kwenye turubali au mbao, na kutokana na zoea hilo, watu wakaanza kuabudu sanamu za kuchorwa.” Hivyo, zoea la wapagani la kuabudu picha liligeuka na kuwa ibada ya picha za Yesu, Maria, malaika, na “watakatifu.” Picha hizo ambazo zilianza kutumiwa makanisani pole kwa pole zilianza kuwekwa katika nyumba za mamilioni ya watu na kuabudiwa huko.

Kuabudu “kwa Roho na Kweli”

Yesu aliwaambia wasikilizaji wake kwamba lazima watumishi wa Mungu waabudu “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Kwa hiyo, mtu mnyoofu anapotaka kujua ukweli kuhusu kutumia sanamu za kuchorwa katika ibada, anapaswa kuchunguza Neno la Mungu ili kuelewa habari hiyo.

Kwa mfano, Biblia ina maneno haya ya Yesu: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Paulo alisema kwamba “kuna Mungu mmoja, na mpatanishi mmoja kati ya Mungu na wanadamu, mwanadamu, Kristo Yesu,” na kwamba “Kristo . . . hutuombea.” (1 Timotheo 2:5; Waroma 8:34) Madaraka hayo huwa na maana zaidi tunaposoma kwamba Kristo anaweza “kuwaokoa kwa ukamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu yeye yuko hai sikuzote ili kuwaombea.” (Waebrania 7:25) Tunapaswa kusali kwa Mungu kupitia jina la Yesu Kristo. Hakuna mtu yeyote au sanamu yoyote ya kuchorwa isiyo na uhai ambayo inaweza kuchukua mahali pa Yesu. Ujuzi huo kutoka katika Neno la Mungu unaweza kumsaidia mtu yeyote anayetafuta kweli apate njia ya kumwabudu “Baba kwa roho na kweli” na kupata manufaa za njia hii kuu zaidi ya ibada. Kwa kweli, kama Yesu alivyosema, “Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.”—Yohana 4:23.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kwa ujumla, sanamu ya kidini ya kuchorwa ni mfano au ishara inayoabudiwa na washiriki wa dini fulani. Kwa mfano, katika Kanisa Othodoksi la Mashariki, baadhi ya sanamu hizo humwakilisha Kristo; nyingine Utatu, “watakatifu,” malaika au, kama ilivyotajwa juu, Maria mama ya Yesu. Mamilioni ya watu huheshimu sana sanamu za kuchorwa sawa na vile wengi huheshimu sanamu zinazotumiwa katika ibada. Dini fulani zisizodai kuwa za Kikristo zina imani na maoni kama hayo kuelekea sanamu za kuchorwa na sanamu za miungu yao.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]

Boris Subacic/AFP/Getty Images