Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dunia Inaweza Kuokolewa!

Dunia Inaweza Kuokolewa!

Dunia Inaweza Kuokolewa!

MAKALA zinazotangulia zimeonyesha kwamba wanadamu hawapaswi kuendelea kutumia mali za asili za dunia kupita kiasi kama wanavyofanya sasa. Ni kweli kwamba viongozi wa ulimwengu wamejitahidi sana kupunguza uchafuzi, ukataji wa miti, na matatizo mengine yanayokabili mazingira. Tangu mwaka wa 1972, wakati ambapo Mkutano wa Umoja wa Mataifa Kuhusu Mazingira ya Wanadamu ulifanywa na kufuatiwa na mikutano mingine ya aina hiyo, nchi 163 hivi zimeshiriki katika mikutano hiyo ili kuidhinisha miradi ya kuhifadhi mazingira. Kumekuwa na matokeo gani? David Hunter, msimamizi mkuu wa Kituo cha Sheria za Mazingira za Kimataifa, anasema hivi: “Inasikitisha kwamba mikataba, miradi, na hati nyingi hazijazuia uharibifu wa mazingira ulimwenguni pote.” Hunter anaongeza hivi: “Karibu takwimu zote kuhusu mazingira huonyesha kwamba hali ni mbaya zaidi leo kuliko ilivyokuwa wakati wa Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa 1992.”

Kwa nini kuna maendeleo machache sana hivyo ingawa masuala ya mazingira yameshughulikiwa kwa zaidi ya miaka 30? Sababu moja ni uhitaji uliopo wa kusitawisha uchumi. Uchumi wa mataifa hutegemea pesa zinazopatikana watu wanaponunua bidhaa. Kwa hiyo, ni lazima bidhaa zitokezwe. Na bidhaa hutengenezwa kwa kutumia mali za asili. Hilo ndilo linalosababisha uharibifu wa mazingira. Basi suluhisho ni nini?

Mwongozo Mbaya

Biblia hueleza kile kinachofanya jitihada za mwanadamu za kujiongoza ziambulie patupu. Nabii Yeremia alisema hivi: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Maneno hayo ni ya kweli kabisa!

Je, umewahi kutembelea bustani? Inafurahisha sana kuona miti, mimea, na maua yanayovutia! Hata hivyo, bustani inayopendeza haiwezi kujitokeza. Watunzaji wa bustani wenye ustadi hutumia wakati mwingi kutunza miti, kukata nyasi, na kupalilia maua ili kuboresha bustani. Ebu wazia jinsi ambavyo mazingira yangekuwa ikiwa dunia yote ingetunzwa kama bustani.

Bila shaka, Muumba wetu alikusudia dunia itunzwe kwa njia hiyo. Kulingana na simulizi la uumbaji linalopatikana katika Neno la Mungu lililoandikwa kwa uongozi wa roho yake, ‘Yehova Mungu alimchukua mtu na kumweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.’ (Mwanzo 2:15) Wanadamu hawakuagizwa tu waitunze bustani ya Edeni, bali pia waliagizwa waifanye dunia yote kuwa Paradiso.—Mwanzo 1:28.

Adamu na Hawa walipokosa kutii walipoteza ukamilifu na vilevile pendeleo la kuitunza na kuipanua Paradiso. (Mwanzo 3:1-6, 23) Tukiwa wazao wao, tumerithi dhambi na kutokamilika kutoka kwao. (Waroma 5:12) Uharibifu wa mali za asili za dunia ni jambo moja tu linaloonyesha matokeo mabaya ya mwanadamu kujitawala. Naam, wanadamu hawawezi kutatua matatizo yao. Wanahitaji msaada.

Suluhisho

Yesu alipokuwa duniani, aliwafundisha wanafunzi wake kusali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Biblia inafundisha kwamba kupitia Ufalme wa Mungu wa mbinguni, dunia itafanywa kuwa Paradiso. (Zaburi 37:10, 11) Wakati huo, miti na mimea itazaa kwa wingi katika mazingira safi. (Zaburi 72:16) Kwa mwongozo wa Mungu, dunia itasafishwa, nao wanadamu watajifunza kutunza mazingira. Je, kweli hilo litatukia?

Biblia inasema kwamba dunia “haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Wakati wa Mungu utakapofika, wote watakaokuwapo watafurahia baraka za milele, ambazo zitatia ndani afya nzuri, chakula tele, na nyumba nzuri. Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu kusudi la Mungu? Basi, wasiliana na Mashahidi wa Yehova. Watafurahi kutumia Biblia kukuonyesha jinsi Dunia itakavyookolewa!

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kwa mwongozo wa Mungu, wanadamu watajifunza kutunza mazingira

[Hisani]

Girl and farmer: © Jeremy Horner/ Panos Pictures