Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imeandikwa Kwamba Nitamwona

Imeandikwa Kwamba Nitamwona

Imeandikwa Kwamba Nitamwona

Simulizi la Rosalía Phillips

“Utafanikiwa sana! Una kipawa!” Msimamizi wetu alipaaza sauti na kuniambia maneno hayo akiwa ameketi kando ya piano yake muda mfupi kabla ya maonyesho kuanza. Wale washiriki wengine wanne wa kikundi chetu cha wanamuziki walitoa ishara ya kunikaribisha. Nilikuwa mwanamuziki mpya kabisa katika kikundi hicho, nami nilikuwa nimevalia nguo yangu nyekundu yenye mapambo. Nilikuwa na wasiwasi mwingi. Tulikuwa katika mojawapo ya majumba maarufu zaidi ya maonyesho katika Mexico City, ambapo nilianza kazi ya burudani! Hayo yalitukia katika Machi 1976, mwezi mmoja tu kabla sijafikisha miaka 18.

BABA yangu alikuwa amekufa miaka mitatu mapema, na bado nilikuwa nikimkumbuka sana. Watu wengi walimkumbuka pia. Alipendwa na kuheshimiwa sana kwa sababu alikuwa mmojawapo wa waigizaji maarufu wa sinema za vichekesho nchini. Alishiriki katika sinema zaidi ya 120 zilizoigizwa katika kile kipindi cha mafanikio makubwa ya biashara ya sinema nchini Mexico. Jina lake, Germán Valdés, “Tin-Tán,” lilikuwa likitangazwa kwenye mahema makubwa ya maonyesho kotekote katika Amerika ya Kati na ya Kusini, na katika sehemu zenye watu wanaozungumza lugha ya Kihispania nchini Marekani na Ulaya. Hata leo, zaidi ya miaka 30 baada ya kifo chake, sinema zake zingali zinaonyeshwa tena na tena kwenye televisheni.

Tangu nilipokuwa msichana mchanga watu mashuhuri walikuwa wakikusanyika nyumbani kwetu. Mama yangu na dada zake walikuwa katika bendi ya waimbaji watatu inayoitwa Las Hermanitas Julián (yaani, Mabinti wa Julián). Ndugu ya mama yangu anayeitwa Julio Julián alikuwa mwimbaji mashuhuri huko Ulaya, huku mke wake Mhispania anayeitwa Conchita Domínguez, akiwa mwimbaji wa sauti ya soprano. Isitoshe, ndugu za baba yangu, Manuel “Loco” (mwenye kichaa) Valdés na Ramón Valdés, aliyejulikana kama Don Ramón, walikuwa waigizaji maarufu wa vipindi vya vichekesho vya televisheni.

Mimi na ndugu yangu Carlos tulizoea kwenda kwenye maeneo ya kurekodia sinema, majumba ya sinema, na vyumba vya kurekodia sauti kwani Baba alikuwa akitupeleka huko mara nyingi alipokwenda kufanya kazi, na hivyo ndivyo alivyodumisha umoja katika familia yetu. Tuliona tofauti kubwa kati ya maeneo hayo na nyumbani kwetu, ambako tuliishi kwa umoja na upendo! Baba yangu alikuwa mtu mwenye upendo na mchangamfu, naye alipenda kufurahia maisha. Alikuwa mkarimu sana, hata nyakati nyingine alipita kiasi. Alinifundisha kwamba kuwa mwenye furaha hakutegemei kuwa na mali bali hutegemea kutoa.

Badiliko Lenye Kuhuzunisha

Kuelekea mwishoni mwa mwaka wa 1971, Mama alitueleza mimi na ndugu yangu kwamba Baba ana ugonjwa usioweza kutibiwa. Kwa mwaka mmoja na nusu, nilimwona akiteseka, huku akitumia dawa zenye nguvu zilizomsaidia kuendelea kuishi.

Ningali nakumbuka wakati ambapo ambulansi ilikuja nyumbani kwetu ili kumchukua Baba na kumpeleka hospitali. Nilijua kwamba hangerudi. Nilihuzunika sana. Kwa kuwa alikuwa akiteseka, nilihisi kwamba mimi pia napaswa kuteseka. Nilijichoma mkono kwa sigara na kulia sana. Baba yangu alikufa mnamo Juni 29, 1973. Nilianza kujiuliza hivi: ‘Kwa nini mtu mzuri hivyo, aliyekuwa akiwafurahisha watu, ametuacha? Yuko wapi sasa? Je, nikisema naye anaweza kunisikia? Je, maisha yangu yanaweza kuwa na kusudi bila yeye kuwepo?’

Kufanya Kazi Bila Kusudi Maishani

Baada ya muda, huzuni yangu ilikwisha nami nikaanza kusomea kazi ya kupamba nyumba. Nilikuwa mkaidi mara kwa mara, basi ikanibidi kuacha shule. Mimi na mama yangu tuliamua kushirikiana zaidi na watu wengine. Tulikuwa tukihudhuria karamu kubwa za watu mashuhuri katika fani ya burudani. Mara nyingi, karamu ilipokuwa ikikaribia kwisha, mkaribishaji alisema hivi, “Rosalía, tafadhali tuimbie moja ya nyimbo zako.” Walipenda sauti yangu na njia yangu ya kuimba kwa hisia, nao walisema kwamba nilirithi kipawa cha wazazi wangu.

Kwenye karamu moja kama hiyo, mtunzi na msimamizi wa bendi ya Arturo Castro and His Castros 76 alisikia nikiimba naye akanialika nijiunge na kikundi chake. Mwanzoni sikupenda wazo hilo. Hata ingawa nilipenda muziki na nilikuwa nimecheza gita na kutunga nyimbo tangu nilipokuwa na miaka 14, sikutaka kuwa mwanamuziki wa kulipwa. Lakini kwa kuwa mama yangu alinisihi sana, na familia yetu ilihitaji pesa, mwishowe nilikubali. Hivyo ndivyo nilivyoanza kazi ya burudani katika lile tukio nililosimulia mwanzoni.

Nilikuwa na shughuli nyingi tangu nilipoanza kufanya kazi. Kikundi chetu kilitembelea maeneo mbalimbali ya Mexico na kufanya maonyesho mawili kila usiku. Tulifanya kazi huko Guatemala, Venezuela, New York, na Las Vegas. Nilifanya kazi na kikundi hicho kwa miaka miwili. Kisha, nikaombwa nishiriki kutayarisha sinema. Niliombwa niigize pamoja na waigizaji wakuu katika sinema mbili na kuwa mwigizaji mkuu katika sinema moja, nami nilituzwa mara mbili kwa kushiriki katika sinema hizo.

Siku moja nilipigiwa simu na kampuni kubwa zaidi ya televisheni nchini. Walinipa kandarasi ya kuwa mwigizaji mkuu katika kampuni yao na kuwa mwigizaji mkuu katika kipindi cha mfululizo ambacho kingeitwa kwa jina langu. Hivyo ningekuwa mashuhuri sana katika burudani. Ningepata mshahara mkubwa, hata kama singefanya kazi kila siku. Nilikataa kandarasi hiyo kwa sababu nilihisi kwamba sistahili kupata mambo yote hayo na pia nilihofu kupoteza uhuru wangu. Nilikubali kuigiza kile kipindi cha mfululizo ili niendelee kusomea uigizaji katika chuo kikuu. Hata hivyo, sikuwa na furaha. Sikufurahi kuwaona waigizaji wakijikakamua kwa miaka mingi ili wawe waigizaji wakuu, huku mimi nikipewa sehemu hiyo hasa kwa sababu nilikuwa binti ya Tin-Tán.

Baada ya muda nikaanza kazi ya kurekodi. Nilianza kwa kurekodi muziki niliotunga kwa ajili ya kipindi cha mfululizo nilichoigiza. Baadaye, nilirekodi muziki katika kituo maarufu huko London. Nilirekodi muziki zaidi, nikashiriki katika sinema, na vipindi vingine vya mfululizo. Magazeti yalianza kuandika habari zangu katika kurasa za mbele za makala za burudani. Hivyo, inaweza kusemwa kwamba nilikuwa nimefikia upeo wa mafanikio. Lakini bado sikuridhika. Nilijionea jinsi waigizaji walivyojitutumua na kushindana, na jinsi walivyokosa adili na unyoofu. Niliacha kuwatumaini watu.

Kisha wakati fulani katika mwaka wa 1980, nilimwona mjomba wangu Julio wakati familia yetu ilipokutana. Alikuwa ameamua kuacha kazi ya maonyesho ya muziki, nami nilimsikiliza akizungumza kuhusu paradiso iliyoahidiwa na Mungu. Julio alisema kwamba ukosefu wa haki na huzuni vitaondolewa duniani na upendo utadumu. Pia alisema kwamba jina la Mungu wa kweli ni Yehova. Nilipendezwa zaidi aliposema kwamba katika Paradiso wapendwa wetu waliokufa watafufuliwa. Tarajio la kumwona tena baba yangu lilinifurahisha sana. Bado nilikuwa ninamkosa na nilitamani utegemezo na upendo wake. Ningefurahi sana kumwona tena! Lakini nilihisi kwamba hilo haliwezekani. Mjomba wangu, Julio, alinipa Biblia na kutukaribisha mimi na mama yangu tuhudhurie kusanyiko la Mashahidi wa Yehova ambalo lingefanywa majuma machache baadaye. Tulimwambia kwamba huenda tukahudhuria.

Naamua Kubadili Maisha Yangu

Usiku mmoja nilikuwa kitandani nikivuta sigara huku nikisoma Biblia ambayo mjomba wangu alikuwa amenipa. Kutokana na yale niliyosoma katika kitabu cha Methali, nilikata kauli kwamba nuru, uelewaji, na uhai hutoka kwa Mungu, huku giza, mvurugo, na kifo vikitoka katika chanzo tofauti. Usiku huohuo, nilizima sigara yangu ya mwisho na kumsubiri Mama afike. Nililia huku nikimwomba anisaidie kufanya maamuzi makubwa. Kisha, nikaenda kwenye jumba la maonyesho ambako nilikuwa nikifanya mazoezi ya kuigiza sehemu ya Cordelia katika mchezo wa kuigiza wa Shakespeare ulioitwa King Lear. Niliacha kuigiza mchezo huo na kuvunja uhusiano wangu na rafiki yangu wa kiume, aliyekuwa mmoja wa waigizaji wakuu.

Hata hivyo, sikuwa nimejifunza jinsi ya kumtumikia Mungu, kwa hiyo sikuwa na kichocheo chochote. Nilishuka moyo sana. Nilimwomba Mungu anisaidie niridhike bila kutegemea kipawa nilichorithi au umaarufu wangu. Niliacha kushirikiana na marafiki wangu wote na kuacha shughuli zangu za kawaida.

Kupata Mafanikio ya Kweli

Nilipokuwa nimevurugika hivyo, nilikumbuka kwamba mjomba wangu alikuwa amenialika kuhudhuria kusanyiko. Nilimpigia simu, naye akaja kunichukua ili twende kwenye kusanyiko. Nilivutiwa na mambo niliyoona huko. Niliona watu wenye utaratibu ambao hawakutumia lugha chafu wala kuvuta sigara, na ambao hawakujaribu kujifanya ili kuwafurahisha wengine. Yale niliyosikia yakisemwa kutoka katika Biblia yalinikumbusha mambo niliyokuwa nimesoma katika kitabu kidogo chenye kichwa Is the Bible Really the Word of God? * ambacho nilikuwa nimepata nyumbani kwetu muda mfupi baada ya kifo cha baba yangu.

Wapata wakati huo, niliombwa niwe mwigizaji mkuu katika kipindi kingine cha mfululizo. Nilipenda sehemu niliyopaswa kuigiza kwa kuwa ilionekana kwamba inaunga mkono kanuni za Biblia nilizokuwa nimejifunza kwenye kusanyiko. Hivyo, nikakubali kuigiza sehemu hiyo. Kwa upande mwingine, nilikumbuka tena na tena maneno haya ya Biblia: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini. Kwa maana . . . nuru ina ushirika gani na giza?”—2 Wakorintho 6:14.

Nilitamani kumpendeza Mungu. Nilitaka kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme pamoja na mjomba na shangazi yangu. Ingawa kutaniko lao lilikuwa umbali wa saa moja hivi kutoka nilipoishi, nilihudhuria mikutano ya Jumapili kwa majuma matatu mfululizo. Mjomba wangu aliamua kunipeleka kwenye kutaniko lililokuwa karibu na mahali nilipoishi. Tulifika mikutano ilipokuwa ikiisha, nami nikakutana na Isabel, msichana wa rika langu. Isabel alikuwa mwenye fadhili na hakujifanya. Mjomba wangu alipomjulisha kwamba mimi ni Rosalía Valdés, hakuzingatia jina langu hata kidogo. Hilo lilinipendeza sana. Alijitolea kunifundisha Biblia nyumbani kwangu.

Tulianza kujifunza kwa kutumia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. * Isabel alikubali kwa hiari kubadilika kulingana na ratiba yangu. Nyakati nyingine alilazimika kungoja hadi usiku sana, ili nimalize kuigiza sehemu yangu. Nilifurahi sana kwamba kuna mtu anayependezwa nami kwa sababu tu ninataka kujifunza kweli za Biblia! Isabel alikuwa mnyoofu na mwenye tabia nzuri, sifa ambazo nilifikiri zinapatikana tu kwa kusomea falsafa na sanaa. Tulipanga kujifunza kwa saa nyingi, na nyakati nyingine tulijifunza mara kadhaa kwa juma.

Mwanzoni ilikuwa vigumu kuacha maoni yangu yasiyo sahihi. Hata hivyo, pole kwa pole kweli za Biblia zilibadili maoni hayo. Nakumbuka jinsi ahadi hii ya Mungu ilivyonitia moyo: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zaburi 37:10, 11) Isitoshe, nilisadiki zaidi kwamba nitamwona baba yangu tena katika Paradiso. Mara nyingi nilifikiria maneno haya ya Yesu: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka, wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima.”—Yohana 5:28, 29.

Baada ya kumaliza kuigiza sehemu yangu katika kile kipindi cha mfululizo, niliombwa niigize katika vipindi vingine. Ingawa vipindi hivyo vingeniwezesha niwe mashuhuri zaidi, kukubali kushiriki katika vipindi hivyo kungemaanisha kwamba ninaunga mkono ukosefu wa adili, ibada ya sanamu, na mafundisho mengine ya uwongo. Nilikuwa nimejifunza kwamba kwa kweli Shetani yuko na kwamba hataki tumtumikie Yehova. Kwa hiyo nilikataa kazi hizo, nami nikaanza kuhudhuria mikutano yote. Mama yangu na ndugu yangu hawakuelewa sababu yangu ya kukataa kufanya kazi hizo ambazo zingeniwezesha kupata pesa nyingi sana. Wakati huohuo waliona mabadiliko niliyokuwa nikifanya. Niliacha kuhuzunika na kushuka moyo, nami nikawa mchangamfu na mwenye shangwe. Hatimaye nikawa na kusudi maishani!

Nilitamani kuwaeleza wengine yale niliyokuwa nikijifunza na upesi nikawa mhubiri wa ujumbe mzuri kuhusu Ufalme wa Mungu. Nyakati nyingine nilipokuwa nikihubiri, wenye nyumba walishindwa kukaza fikira kwani wengi wao walijua kwamba mimi ni mwigizaji. Mara kwa mara, mimi na mhubiri mwenzangu tulifika kwenye nyumba za watu wakati kipindi nilichokuwa nimeigiza kilipokuwa kikionyeshwa kwenye televisheni. Wenye nyumba walishangaa sana kuniona nyumbani kwao!

Mnamo Septemba 11, 1982, nilibatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova. Sasa nilikuwa na kusudi maishani, nami ningeweza kufanya kazi tofauti kabisa. Bidii ya Isabel kwa ajili ya huduma ilinichochea. Alitumikia akiwa painia wa kawaida, yaani mtumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Muda si muda, niliandamana naye alipoenda kuwafundisha wengine kuhusu Biblia. Isabel akawa rafiki yangu mkubwa.

Kwa kuwa nilikuwa nimeacha kazi ya uigizaji, mimi na mama yangu tulilazimika kuridhika na maisha ya chini. Wakati huohuo, nilitunga nyimbo kwa ajili ya albamu yangu ya nne, ambayo ilikuwa na nyimbo zilizozungumzia maadili na imani yangu mpya. Niliandika wimbo uliozungumzia tumaini langu hakika la kumwona baba yangu tena. Niliuita wimbo huo “Imeandikwa Kwamba Nitamwona.” Mama yangu aliguswa moyo sana nilipomwimbia wimbo huo mara ya kwanza. Aliona kwamba nimesadikishwa sana. Nilisisimuka aliposema kwamba anataka kujifunza Biblia. Alibatizwa miaka miwili baadaye, akawa mtumishi wa Yehova. Bado anashiriki kwa bidii katika huduma.

Baada ya muda, ikawa rahisi kwangu kukataa kazi mbalimbali. Nilipokabili jaribu au kishawishi, niliimarishwa kuendelea kumtumikia Yehova kwa kuwazia jinsi tutakavyoishi pamoja na baba yangu katika paradiso maridadi.

Siku moja niliombwa nishiriki kuigiza kipindi cha watoto cha Sesame Street katika Kihispania. Niliona kwamba siwezi kushiriki nami nikamwambia mtayarishi kwamba kanuni za Biblia haziniruhusu kuunga mkono sikukuu na siku za kuzaliwa. Mtayarishi alisema kwamba ikiwa ningekubali kazi hiyo, angeheshimu imani yangu nasi tungetia sahihi makubaliano yaliyoonyesha mambo ambayo sitaki kufanya. Basi nikashiriki kuigiza vipindi 200. Baada ya hapo, nikaacha kazi ya kuigiza.

Kwa sababu sikuwa nimemaliza kandarasi moja na ile kampuni ya kurekodi muziki, nilirekodi nyimbo kumi kutia ndani ule wimbo uliozungumzia baba yangu na ufufuo. Niliimba wimbo huo kwenye televisheni na kwenye pindi nyingine, na nilitumia pindi hizo kueleza mambo ninayoamini. Hata hivyo, ile kampuni ya kurekodi muziki ilianza kunishinikiza nirekodi nyimbo zilizochochea ngono. Basi nikajiuzulu.

Baraka za Kumtumikia Mungu

Mnamo Desemba 1983, mimi na Isabel tulitembelea ofisi za Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Tukiwa huko nilikutana na Russell Phillips ambaye baadaye alinioa. Tuliandikiana barua kwa miaka miwili hivi. Nakumbuka vizuri sana siku niliyoanza upainia wa kawaida, kwani Russell alinitumia maua ya waridi kutoka New York!

Nilifanya upainia pamoja na Isabel kwa mwaka mmoja. Kisha akaalikwa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Mexico. Mazungumzo yake kuhusu mgawo wake mpya yalinichochea nitamani kuongeza utumishi wangu na ikiwa ni mapenzi ya Yehova nitumikie Betheli.

Pia nimebarikiwa kuwa na Russell. Kutokana na upendo wake kwa Yehova na tengenezo Lake, nimejifunza kuthamini utumishi wa wakati wote. Kwa kuwa alikuwa ametumikia katika Betheli ya Brooklyn kwa miaka mitatu, alipenda Betheli sana. Tulipooana tulitumikia tukiwa mapainia wa kawaida huko Colorado, Marekani. Baadaye tuliombwa tushiriki ujenzi wa ofisi za tawi katika nchi nyingine tukiwa wafanyakazi wa ujenzi wa kimataifa. Tulishangaa sana tulipopata mgawo wa kwenda Mexico! Katika Aprili 1990, tulipata pendeleo la kuwa washiriki wa familia ya Betheli nchini Mexico. Mfano wa Russell ulinitia moyo sana. Nilivutiwa sana na roho yake ya kujitolea ambayo ilimchochea kuhama nchi yao, kuacha familia yao, na kuja Mexico ili kuunga mkono kazi ya Ufalme.

Mimi na Russell tulifurahia sana pendeleo letu la kutumikia katika ofisi ya tawi ya Mexico. Lakini mambo yakabadilika ghafula nilipopata mimba. Hatukutarajia jambo hilo. Hata hivyo, sikuzote tulikuwa tumevutiwa na wazazi ambao hulea watoto wao katika kweli, nasi tuliuona kuwa mgawo mpya. Katika Oktoba 1993, Evan alizaliwa, naye Gianna akazaliwa miaka miwili na nusu baadaye. Hata ingawa tunahitaji kuendelea kujitahidi kuwalea watoto wetu, sisi hufurahi kila wakati wanapoeleza yale wanayoamini wanapokuwa shambani. Sasa mmoja ana miaka 11 na yule mwingine ana miaka 8.

Kwa sasa, Russell anatumikia katika Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa ya Majumba ya Ufalme, na hivi majuzi nilianza tena utumishi wa wakati wote nikiwa painia. Kwa miaka 20 iliyopita, nimewasaidia washiriki 12 wa familia yetu na watu wengine 8 kujifunza ukweli wa Biblia na kuanza kumtumikia Yehova.

Watoto wangu wanaponiuliza hivi, “Mama, je, ilikuwa vigumu kuacha kazi yako ya maonyesho?” Mimi hunukuu maneno haya ya mtume Paulo: “Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa sababu yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kumpata Kristo.” (Wafilipi 3:8) Ninamshukuru sana Yehova kwa kuniwezesha kuacha maisha ya ubatili yasiyo na kusudi na kuniruhusu niwe miongoni mwa watu wake wa pekee! Daima mimi humshukuru kwa baraka zake nyingi zinazopatikana kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. Mara nyingi mimi huimba kwa shangwe wimbo niliotunga kuhusu baba yangu. Ninasadiki kwamba nitamwona tena.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova ingawa hakichapishwi tena.

^ fu. 24 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova ingawa hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nikiwa na wazazi wangu na ndugu yangu nilipokuwa na umri wa mwaka mmoja

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nilipokuwa nikiimba pamoja na bendi ya Arturo Castro and His Castros 76

[Hisani]

Angel Otero

[Picha katika ukurasa wa 14]

Nikiwa na familia yangu leo

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Activa, 1979