Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutua Ghafula!

Kutua Ghafula!

Kutua Ghafula!

SIMULIZI LA CÉSAR MUÑOZ

Baada ya kufurahia likizo pamoja na familia yangu katika jiji la Monterrey, Mexico, nilijitayarisha kurudi kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Mexico City, ambapo mimi hutumika. Mnamo Jumapili Desemba 1, 2002, nilipanda ndege Na. 190, na safari ikaanza saa 1:00 jioni.

BAADA ya kusafiri kwa saa moja na nusu hivi bila matatizo, ndege ilianza kushuka. Ghafula, ikapanda, na sote tukashtushwa na sauti yenye kuogofya kutoka chini. Kisha rubani akasema kwamba milango ya magurudumu imekataa kufunguka. Ilikuwa imekwama! Baadhi ya abiria walilia kwa woga. Wengine walisali kwa sauti. Sikujua ni nini kingetokea.

Rubani alituambia kwamba angejitahidi kufungua milango ya magurudumu. Hivyo tulipokuwa juu ya Mexico City, aliipeleka ndege juu na chini na kutoka upande mmoja hadi mwingine kwa saa moja hivi. Ndege iliyumbayumba vibaya sana kuliko treni yoyote ya burudani niliyowahi kupanda. Bila shaka lilikuwa jambo la kushtua sana! Kisha rubani akatuambia hivi: “Tunasikitika kuwajulisha kwamba milango ya magurudumu haijafunguka. Kile tunachoweza kufanya ni kutua ghafula bila magurudumu.” Tuliangaliana kwa wasiwasi, tukiwazia kwamba tutakufa.

Tulipewa maagizo kuhusu tunavyopaswa kufanya ndege inapotua ghafula. Tulitoa viatu na vitu vingine vyote ambavyo vingesababisha majeraha na kuketi jinsi tulivyoambiwa. Nilidhani kwamba ndege yetu ingeanguka uwanjani! Mara hiyo nilisali kwa Yehova Mungu na kutulia.—Wafilipi 4:6, 7.

Mara nyingi nimesikia watu wakisema kwamba mtu anapokaribia kufa, yeye hukumbuka mambo aliyofanya maishani na kuwaza kwamba laiti angalifanya hili au lile. Nilisikitika kwamba sikuwa nimemhubiria msichana aliyeketi kando yangu kuhusu Ufalme na niliazimia kwamba nikiokoka, nitatumia kila nafasi kuhubiri. Pia nilifikiri kuhusu utumishi wangu kwa Yehova.

Niliona magari ya kuzima moto, ambulansi, na watu wengi waliokuwa wamesimama karibu wakati ndege ilipoanza kushuka. Kisha tukatikiswa sana sehemu ya chini ya ndege ilipogonga uwanja wa ndege. Kulikuwa na cheche za moto ndege ilipogonga chini. Magari ya kuzima moto kutoka pande zote yakainyunyizia ndege maji ili kuipoza.

Hatimaye, baada ya wasiwasi mwingi, ndege ikasimama. Tulipiga makofi na kushangilia sana kwamba rubani alifaulu kutua kwa ghafula. Kisha tukaambiwa tuondoke mara moja kwenye ndege hiyo. Kwa haraka tulikimbilia milangoni na kushuka ngazi zilizoinuka, tukafikia sehemu zenye usalama za uwanja huo wa ndege.

Nikiwa nimesimama mbali kidogo huku nikitetemeka, nilitazama ndege hiyo ikiwa imeegemea upande mmoja. Ni abiria wachache tu waliojeruhiwa kidogo. Wengine walipata matibabu kwa sababu ya mshtuko kwenye ambulansi zilizokuwa karibu.

Nilitazamia kufika nyumbani saa 3:00 usiku, lakini niliwasili saa nne baadaye. Hata hivyo, nilishukuru kuwa hai! Kisa hicho kimenifanya nifikiri. Nilitambua kwamba maisha yanaweza kwisha wakati wowote. Uhai wako unapokuwa hatarini, huenda ikawa kuchelewa mno kurekebisha maisha yako au kutenda mema zaidi mbele za Mungu. Sasa ninathamini sana nafasi niliyo nayo ya kutumia maisha yangu kwa hekima na kumtumikia Mungu wangu, Yehova, kila siku kwa uwezo wangu wote.—Zaburi 90:12.