Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Misitu ya Mvua Nilipendezwa sana na mfululizo “Ni Nani Atakayeokoa Misitu ya Mvua?” (Juni 22, 2003) Sikushangaa nilipoona kwamba mlizungumzia misitu ya mvua ya Amerika Kusini. Kwa kuwa misitu ya Afrika na Asia iko katika hali mbaya zaidi, angalau wanadamu wanaweza kuokoa ile ya Amerika Kusini. Ninatazamia kwa hamu wakati ambapo Mungu ataingilia kati na kukomesha uharibifu wa misitu ya dunia yetu ili uumbaji urudie utukufu wa awali.

G. R., Uswisi

Asanteni sana kwa makala hizo. Kwa muda fulani sasa, nimekuwa nikifanya utafiti kuhusu mazingira, hivyo nimebadilisha jinsi ambavyo nimekuwa nikinunua vitu na kutupa takataka. Ninasikitika sana kwamba mimea imeharibiwa na wanyama wamelazimika kuhama au kuuawa na wanadamu wenye pupa. Nafarijiwa na kutiwa moyo kujua kwamba Muumba anajua kinachoendelea na kwamba atarekebisha mambo hivi karibuni. Asanteni kwa kuchapisha makala hizo nzuri.

V. T., Kanada

Ninapenda mazingira na nimekuwa nikihangaikia misitu ya mvua kwa miaka mingi. Ninafurahi kuona kwamba Mashahidi wa Yehova wanajali uumbaji wa Mungu. Ninafurahi kujua kwamba siku moja misitu ya mvua itakuwa salama.

T. H., Marekani

Msiba Asanteni kwa makala “Vijana Huuliza . . . Nifanyeje Msiba Ukitokea?” (Juni 22, 2003) Nilipomaliza tu kuisoma makala hiyo, nilihisi kwamba Yehova amenisaidia nitatue tatizo ambalo nimekabili kwa miaka mingi. Nikiwa Mkristo, ninajua kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” ambazo ni “ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, mara tu nilipotazama habari yenye kuogopesha katika televisheni, nilisumbuka. Nilivunjika moyo sana mpaka nikakosa nguvu na wakati mwingine nilikaa nyumbani badala ya kwenda kuhubiri. Nilihofia mambo ambayo huenda yangetokea au yasitokee wakati ujao. Lakini makala hiyo ilinisaidia nikumbuke umuhimu wa kuendelea na mambo ya kiroho na kumwambia Yehova mambo yetu yote na kumtumaini kabisa. Nawashukuru kutoka moyoni kwa ajili ya vitabu vyenu.

E. K., Japan

Mnamo Januari 2003, babu yangu alikufa hospitalini. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kumwona mtu wa ukoo wa karibu akifa. Makala hiyo ilijibu maswali niliyokuwa nayo. Moyo wangu uliguswa hasa na habari chini ya kichwa kidogo kinachosema “Kwa Nini Misiba Hutokea?” Ilinisaidia nitambue kwamba mambo yaliyoikumba familia yetu ni tokeo la matukio yasiyotazamiwa. Haikumaanisha kwamba Yehova ametuacha. Baada ya kusoma makala hiyo, hofu nyingi niliyokuwa nayo ilitoweka.

M. O., Japan

Mahitaji ya Kiroho Makala “Jinsi Mahitaji Yangu ya Kiroho Yalivyotoshelezwa” ilinifanya nilie. (Juni 22, 2003) Nilizaliwa katika familia ya Kikatoliki na kuhudhuria shule ya Kikatoliki kwa miaka minane. Ingawa hatukusoma Biblia shuleni wala kwenye Misa, sikuzote niliipenda Biblia na niliisoma kila jioni. Kama Lucia Moussanett, nilitamani kutenda mambo niliyojifunza katika Biblia lakini sikujua jinsi ya kufanya hivyo. Nilipoanza kufundishwa Biblia na Mashahidi wa Yehova, mahitaji yangu ya kiroho yalitoshelezwa. Asanteni sana kwa masimulizi kama hayo yenye kugusa moyo!

K. F., Marekani