Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanafaidi Jamii

Wanafaidi Jamii

Wanafaidi Jamii

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI HISPANIA

KWA karne nyingi, sehemu mbalimbali katika majiji ya Hispania zimetengwa kwa ajili ya majengo ya ibada. Viongozi wa majiji waliamini kwamba dini inaweza kusaidia jamii zao. Kwa kawaida, Kanisa Katoliki ndilo lililokuwa likipewa mashamba ili kujenga makanisa, kwani dini ya Katoliki ndiyo iliyokuwa dini rasmi katika nchi hiyo. Lakini mambo yamebadilika.

Katika mwaka wa 1980, sheria fulani ilitungwa nchini humu ili kuhakikisha uhuru wa kidini na ilisema kwamba “hakuna dini yoyote ambayo inapaswa kuwa dini rasmi.” Jambo hilo limewafanya maafisa kadhaa wa jiji kutambua kazi ya Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo wametoa mashamba kwa ajili ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme.

Wasimamizi wa majiji mbalimbali wamesema kwamba Mashahidi wamestahili kupewa mashamba hayo kwa sababu “kazi yao inaelimisha watu,” na vilevile “inafaidi watu wote katika jamii.” Wengine wametaja “faida ambayo Mashahidi wa Yehova wameleta katika jiji hilo” na “kazi wanayofanya bila malipo.”

Kwa kutumia mbinu fulani ya pekee ya ujenzi, Mashahidi waliojitolea kufanya kazi hiyo wamejenga Majumba mengi ya Ufalme kwa muda wa saa 48. Meya wa jiji la La Línea huko kusini-magharibi mwa Hispania alisema hivi: “Ninapendezwa sana na roho ya kujitolea ya wajenzi hao, na ninahisi kwamba tunapaswa kuwaunga mkono. Tunahitaji roho hiyo katika ulimwengu wa leo wenye migawanyiko.” Alisema kwamba Jumba hilo jipya la Ufalme “linaonyesha roho ya ushirikiano.”

Majirani pia wametambua ushirikiano huo. Wakati wa ujenzi wa Majumba pacha ya Ufalme huko Vitoria, kaskazini mwa Hispania, Marian, anayekaa katika eneo hilo alisema: “Ikiwa kila mtu angeonyesha upendo huo, hatungekuwa na matatizo leo.” Baada ya kuona jengo hilo likikamilika, msanifu mmoja wa majengo katika eneo hilo alisema hivi: “Ningependa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova ili niwe na shangwe kama nyinyi!”

Katika jiji la Zaragoza, kaskazini-mashariki mwa Hispania, maafisa waliwapa Mashahidi shamba la meta 600 za mraba bila malipo. Gazeti la eneo hilo lilisema kwamba “Mashahidi wa Yehova walifanya kazi kama mamia ya chungu.” Majirani waliwakaribisha wafanyakazi hao kwa uchangamfu. Mmoja wao alisema hivi: “Makasisi hudhoofisha imani yangu, lakini mmeiimarisha.”

Mashahidi wanawashukuru majirani na viongozi wa mitaa kwa kuwasaidia katika ujenzi wa majengo yao ya ibada. Wameazimia kutumia Majumba yao ya Ufalme kufanya kazi bora ya elimu inayoweza kufaidi jamii, yaani, kuhubiri na kufundisha Neno la Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Jiji la La Línea, Cádiz, Hispania