Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kusafiri kwa Ndege Nina umri wa miaka 10 na ninaishi California, Marekani. Ninashukuru kwa gazeti la Amkeni! lenye kichwa “Je, Bado Ni Salama Kusafiri kwa Ndege?” (Desemba 8, 2002) Wanafunzi 47 katika shule yetu wanapanga kusafiri kutoka San Diego hadi Sacramento. Nilikuwa na wasiwasi kwamba huenda kukatokea msiba wa ndege au huenda ndege ikatekwa nyara. Lakini makala hiyo iliondoa wasiwasi wangu, na maelezo kuhusu mbinu za kisasa za usalama yaliondoa hofu yangu. Nitajitahidi kuwapa gazeti hili wanafunzi wote wa darasa letu ambao wanaogopa kusafiri kwa ndege.

V. M., Marekani

Kuacha Vita Niliguswa hisia na simulizi la Toshiaki Niwa katika makala yenye kichwa “Niliacha Vita Nikaanza Kutafuta Amani.” (Desemba 8, 2002) Nilizaliwa nchini Ufilipino miaka michache baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Watu katika familia yetu walisimulia kuhusu ukatili wa wanajeshi katika vita hivyo. Nilipokuwa mtoto, nilijiuliza hivi, “Watu hao waliwezaje kufanya hivyo?” Simulizi la Ndugu Niwa lilinisaidia kuelewa jambo hilo vizuri zaidi. Asanteni kwa kuchapisha makala kama hizo. Simulizi hilo linaonyesha kwamba Yehova ana nguvu nyingi za kubadili mwenendo wa watu.

A. C., Marekani

Chembe za Msingi Nimesoma gazeti la Amkeni! kwa miaka 20 na kupitia makala zake, nimejifunza mambo mengi. Wakati watu walipoanza kuzungumza juu ya chembe za msingi na jinsi ya kufanyiza viumbe kwa kutumia chembe, sikuelewa jinsi ambavyo chembe fulani zingeweza kufanyizwa nje ya mwili wa mwanadamu. Makala “Je, Sayansi Imevuka Mipaka kwa Kutumia Chembe za Msingi?” (Novemba 22, 2002), ilinisaidia kuelewa jinsi hilo linavyowezekana na kwa nini jambo hilo limezusha ubishi.

F. M., Italia

Nilipokuwa nikisoma makala hizo, niliogopeshwa sana na mbinu ambazo wanadamu wanatumia kutibu magonjwa hatari. Ninawashukuru sana kwa jitihada zenu za kuandika makala hizo na kutueleza ukweli kuhusu mambo hayo. Sasa ninatazamia kwa hamu kubwa siku ambayo Mungu ataponya magonjwa yetu yote.

T. F., Ufilipino

Upendo Waonyeshwa Makala yenye kichwa “Upendo Waonyeshwa Kupitia Kazi Kubwa ya Kutoa Msaada” (Novemba 22, 2002) ilinipendeza sana! Mambo ambayo wafanyakazi hao wa kujitolea walifanya katika miezi hiyo michache yanaonyesha wazi kwamba watu wa Mungu wana upendo na kwamba Muumba wetu anabariki sana jitihada za watumishi wake.

C. T., Ujerumani

Niliposoma makala hiyo, machozi yalidondoka. Wakati Mto Elbe ulipofurika, watu 44 katika kutaniko letu walilazimika kuhama. Mimi na mume wangu tulikaribishwa na familia nyingine ya kutaniko letu, na wana wetu wakubwa wawili wakaenda kuishi na familia nyingine. Tangu msiba huo ulipotokea, akina ndugu katika kutaniko letu wamekuwa na uhusiano wa karibu zaidi. Familia yetu inathamini kazi ya kutoa msaada inayofanywa wakati wa misiba kama ule uliotukia Houston.

S. R., Ujerumani

Moto Nilipendezwa na makala yenye kichwa “Faida na Hasara za Moto.” (Septemba 22, 2002) Hata hivyo, ninapinga maelezo ya picha kwenye ukurasa wa 25 yanayosema: “Kongoni walioduwaa wakimbia moto kwenye Bonde la Ufa la Bitterroot huko Montana.” Nina picha hiyohiyo, lakini yangu ni kubwa zaidi na haionyeshi kwamba kongoni hao wameduwaa. Mara nyingi wafanyakazi wanaozima mioto ya misituni huona mbawala na kongoni karibu na sehemu zinazoteketea, lakini wanyama hao huendelea tu kuramba madini au kujibiringisha kwenye majivu. Hata kunapokuwa na mioto mikubwa, wao hujua la kufanya. Ni kana kwamba hawatishiki hata kidogo.

B. D., Marekani

“Amkeni!” linajibu: Tunathamini maoni hayo. Ama kweli, hakuna mtu anayeweza kusema kwa uhakika jinsi ambavyo wanyama huhisi katika hali kama hizo.