Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilijaribu Kuwatumikia Mabwana Wawili

Nilijaribu Kuwatumikia Mabwana Wawili

Nilijaribu Kuwatumikia Mabwana Wawili

IMESIMULIWA NA KEN PAYNE

Nilizaliwa mwaka wa 1938 na kulelewa katika shamba la babu yangu huko New Mexico, Marekani. Shamba hilo lenye ekari 24,000 lilikuwa na mito na mbuga, na milima ilionekana kwa mbali. Ninakumbuka milio ya kondoo, ng’ombe, na farasi, na vilevile sauti ya vigurudumu vya kuhimiza farasi. Nyakati nyingine nilikuwa nikisikiliza sauti ya upepo uliovuma nyasini na mlio mkali wa ndoero waliokuwa karibu na tangi la maji.

MAMBO yanayompata mtu utotoni yana uvutano mwingi baadaye katika maisha yake. Mimi nilitumia wakati mwingi pamoja na babu yangu. Alikuwa stadi wa kusimulia mambo mengi yaliyotukia zamani huko Marekani Magharibi. Hata aliwajua watu wengine waliokuwa wamejiunga na kijana mmoja jambazi aliyeitwa Billy the Kid. Jambazi huyo maarufu alijulikana sana baada ya kuwaua watu wengi pindi moja mwaka wa 1881. Yeye mwenyewe aliuawa pindi hiyo akiwa na umri wa miaka 21.

Wazazi wangu walikuwa Mashahidi wa Yehova, nao walinipeleka katika huduma ya Kikristo kuwahubiria watu kwenye mashamba ya mbali na katika nyumba ndogo za matofali ya udongo kotekote katika bonde la Hondo. Mara nyingi walitumia sahani za santuri zenye hotuba za J. F. Rutherford. * Bado ninakumbuka sauti yake. Tulitumia santuri hizo kuwahubiria watu wa aina zote; wafugaji, wakulima Wamexico, na Wahindi Waamerika kama vile Waapache na Wapueblo. Nilipenda sana kutoa magazeti barabarani kwa sababu sio watu wengi waliokataa kuchukua magazeti kutoka kwa mvulana mdogo, hata katika miaka ya vita ya pili ya ulimwengu.

Ndiyo, nilizoezwa vizuri. Hata hivyo, nilishindwa kutii onyo hili la Yesu: “Hakuna awezaye kutumikia kama mtumwa mabwana-wakubwa wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kutumikia kama watumwa Mungu na Utajiri.” (Mathayo 6:24) Laiti ningeweza kusema kwamba nimetumia maisha yangu kwa furaha katika utumishi wa wakati wote. Lakini mapema maishani, tangu nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, jambo fulani lililonivutia, yaani, ‘bwana’ mwingine, lilinikengeusha nisifuate njia hiyo. Ni jambo gani hilo?

Nilitamani Sana Kuendesha Ndege

Ndege aina ya Piper Cub ilitua karibu na banda letu la ng’ombe mwaka wa 1941. Ilitumiwa kuwawinda mbweha wa jangwani waliokula kondoo wetu. Papo hapo, nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, nikaazimia kwamba ningekuwa rubani. Miaka ambayo akili yangu ilifinyangwa ilipita na nilipokuwa na umri wa miaka 17 niliondoka nyumbani, nikaanza kufanya kazi kwenye uwanja wa ndege wa Hobbs huko New Mexico. Nilifanya kazi ya kushughulikia ndege na kufagia mabanda ya ndege ili kulipia masomo ya kuendesha ndege. Huduma ya Kikristo haikuwa ya maana maishani mwangu.

Nilioa nilipokuwa na umri wa miaka 18, na hatimaye tulipata watoto watatu. Nilipataje riziki? Kwa kuendesha ndege za kunyunyizia dawa za kuwaua wadudu, ndege za kukodishwa, na ndege zilizotumiwa kuwanasa wanyama wawindaji, na vilevile kwa kuwafundisha watu kuendesha ndege. Baada ya miaka sita, nilianza kufanya kazi katika kampuni ya ndege ya Texas International Airlines. Niliendesha ndege za kampuni hiyo zilizoanza safari jijini Dallas, Texas. Maisha yangu yakawa na utaratibu zaidi, na hata nilitumikia nikiwa mzee katika Kutaniko la Denton. Niliongoza mafunzo kadhaa ya Biblia pia. Nilijifunza pamoja na rubani mmoja, mke wake, na watoto wao, ambao wote walikubali kweli ya Biblia.

Kufikia mwaka wa 1973, nilikuwa nimeendesha ndege zenye majembe kwa miaka mitatu hivi, lakini hamu yangu ya kuendesha ndege ilipungua wakati ndege hizo aina ya DC-3 zilipoacha kutumiwa. Nilitamani kurudi New Mexico. Lakini ningepataje riziki kama ningeacha kazi ya kuendesha ndege?

Nilianza Kupenda Sanaa

Tangu mwaka wa 1961, nilipenda kuchora picha zenye mandhari mbalimbali za Marekani Magharibi, na nilikuwa nikifanikiwa kuziuza. Kwa hiyo, niliacha kazi ya kuendesha ndege, nikarudi New Mexico, inayojulikana kama nchi yenye kuvutia. Hata hivyo, sikuendesha maisha yangu kwa busara. Nilijishughulisha na sanaa kupita kiasi. Nilitumia wakati wangu wote kuchora picha, baadaye nilianza kufinyanga sanamu, na nilipata kazi ya muda ya kuendesha ndege. Nilifanya kazi kwa muda wa saa 12 hadi 18 kila siku. Nilipuuza sana familia yangu na Mungu wangu. Matokeo yakawa nini?

Ndoa yangu ilivunjika na mimi na mke wangu tukatalikiana. Nilihamia jimbo la kaskazini la Montana, na nilianza kutumia vileo kupita kiasi ili nijifariji. Kwa sababu ya kupuuza kanuni za Kikristo nilijikuta katika hali ya yule mwana mpotevu katika mfano wa Yesu. (Luka 15:11-32) Kisha, siku moja nikatambua kwamba sikuwa na rafiki wa kweli hata mmoja. Nilipokutana na watu wenye taabu, nilikuwa nikiwaambia hivi: “Watafute Mashahidi wa Yehova. Wao wanaweza kukusaidia sana.” Kisha wao wakaniuliza: “Kwa nini wewe si Shahidi basi?” Ilinibidi kukiri kwamba Shahidi hawezi kuishi vile nilivyoishi.

Hatimaye, mwaka wa 1978, nilirudi tena New Mexico na kuanza kushirikiana na kutaniko lile ambamo Mashahidi walinifahamu. Ilikuwa mara ya kwanza kuingia katika Jumba la Ufalme baada ya miaka kadhaa, na nililia sana. Yehova alinirehemu sana. Ndugu katika kutaniko walinionyesha fadhili sana na kunisaidia kurudia njia za Yehova.

Mwenzi Mpya na Mwanzo Mpya

Nilimwoa Karen mwaka wa 1980, Shahidi mrembo niliyekuwa nimemfahamu kwa miaka kadhaa. Alikuwa na wana wawili, Jason na Jonathan, ambao aliwapata katika ndoa yake ya kwanza. Upendo wake kwa Yehova uliimarisha maisha yangu, na tulipata wana wawili wengine, Ben na Phillip. Hata hivyo, maisha yetu hayangekuwa na raha mustarehe. Msiba ulikuwa mbele yetu.

Nilijifunza sanaa na kutumia wakati mwingi kuchunguza miili na viungo vya wanadamu na wanyama, hasa vile vya farasi. Pia nilijifunza usanifu wa msingi wa sanaa. Nilianza kufinyanga sanamu za udongo, hasa sanamu za mambo ya kale ya Marekani Magharibi, kama vile farasi, Wahindi Waamerika waliopanda farasi, wachungaji wa mifugo, na hata daktari wa siku za kale aliyesafiri kwa gari linalokokotwa na farasi. Biashara yangu ilifanikiwa hatua kwa hatua. Kwa hiyo tukaamua kufungua duka la kuuza na kuonyesha vitu vya sanaa. Karen alibuni jina Mountain Trails Gallery (Duka la Vijia vya Milimani).

Mwaka wa 1987, tulinunua duka huko Sedona, Arizona, na tuliliita jina hilo. Nilifanya kazi yangu ya usanii nyumbani na kuwatunza wavulana, huku Karen akifanya kazi dukani. Hata hivyo, wavulana wakawa wagonjwa na hatukufanikiwa kuuza vitu vingi. Tuliamua Karen awatunze watoto nyumbani, nami nilianza kufanya kazi yangu ya kufinyanga dukani, palepale mbele ya wateja. Sasa biashara yetu ilianza kufanikiwa sana.

Watu waliniuliza juu ya sanamu zangu za shaba. Nilipowaeleza kuhusu kazi yangu na vitu ambavyo nilivitumia kama vielelezo, nilikuwa nikiwafundisha mengi juu ya zama za kale za Marekani Magharibi. Nilitaja majina, mahali mbalimbali, na matukio ambayo nilikuwa nimejifunza kwa kusoma sana kuhusu eneo hilo. Watu walipendezwa kikweli na sanamu nilizokuwa nikitengeneza, na wengine walitaka kulipa sehemu fulani ya bei ya ile sanamu niliyokuwa nikiitengeneza, wakiwa na nia ya kulipa gharama yote baada ya sanamu kukalibiwa. Kwa hiyo, nilianza kuuza vitu vyangu vya sanaa kabla sijamaliza kuviunda, na biashara ilisitawi sana. Biashara yangu ilipanuka hivi kwamba wakati mmoja tulikuwa na maduka matatu na karakana kubwa ya kukalibu yenye wafanyakazi 32. Lakini kazi hiyo yote ilinichosha sana! Mimi na Karen tulijiuliza jinsi ambavyo tungeweza kupunguza kazi. Tulitaja tatizo hilo katika sala. Nilikuwa mzee wa kutaniko na nilijua kwamba ningeweza kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova.

Nilianza Kumtumikia Bwana Mmoja Tena

Mwangalizi wetu wa mzunguko alitembelea kutaniko letu mwaka 1996 na akatukaribisha kwa chakula cha mchana. Kabla hatujaanza kula alituuliza swali ambalo hatukutarajia lililotushtua. Je, tungekuwa tayari kuhamia eneo la Wahindi Waamerika Wanavajo, ili kusaidia kuanzisha kutaniko katika mji wa Chinle? Hiyo ingekuwa kazi ngumu lakini ya kupendeza sana. Tulikuwa tumetembelea eneo hilo la Wahindi Waamerika mara kadhaa ili kuwahubiria watu wanaoishi mbali katika eneo hilo, na sasa tulipata lengo jipya maishani. Hiyo ilikuwa nafasi nzuri ya kuacha kutafuta mali ili kutumia wakati mwingi zaidi kumtumikia Yehova na watu wake. Tulianza kumtumikia bwana mmoja tena!

Mzee mwingine na familia yake, familia ya Carusetta, ambao walikuwa marafiki wetu wa karibu, waliombwa kuungana nasi katika mradi huo. Sisi na wao pia tuliuza nyumba zetu za starehe na kuagiza nyumba zinazoweza kuvutwa kwa gari, ambazo tuliweza kupeleka hadi eneo la Wahindi Waamerika. Niliuza maduka yangu na hatimaye karakana pia. Sasa maisha yetu hayakuwa na mambo mengi, na tuliweza kupanua huduma yetu ya Kikristo.

Mnamo Oktoba 1996, tulifanya mkutano wa kwanza katika kutaniko letu jipya la Chinle. Tangu wakati huo, Wanavajo wengi wamehubiriwa, na kutaniko letu lina mapainia Wanavajo stadi wanaoongea lugha yao. Tumeanza kujifunza lugha hiyo ngumu polepole ili tukubaliwe na watu ijapokuwa sisi si Wanavajo. Tulinunua ardhi kwa kibali cha mamlaka ya Wahindi Waamerika, na tukajenga Jumba la Ufalme mjini Chinle, ambalo liliwekwa wakfu mwezi wa Juni mwaka huu.

Msiba!

Mnamo Desemba 1996, Karen na wana wetu walifunga safari ya kwenda Ruidoso, New Mexico, kwa matembezi ya muda mfupi. Ilinibidi kubaki Chinle. Wazia jinsi tulivyoshtuka na kuhuzunika wakati ambapo mwana wetu Ben, mwenye umri wa miaka 14, aligonga jiwe alipokuwa akiteleza kwa skii, na akafa! Hilo lilikuwa jaribu kubwa sana kwetu, ni tumaini la Biblia la ufufuo ambalo limetuwezesha kustahimili msiba huo. Pia ndugu zetu Wakristo wametutia nguvu sana. Hotuba ya mazishi ilitolewa katika Jumba la Ufalme la Sedona, ambako tulikuwa tumeishi kwa miaka kadhaa. Wanavajo wengi walikuja kusikiliza hotuba hiyo, na ilikuwa mara ya kwanza kwa watu wanaoishi karibu na Jumba la Ufalme kuwaona Wanavajo wengi hivyo. Ndugu na dada kutoka eneo la Wahindi Waamerika walikuwa wamesafiri zaidi ya kilometa 300 ili kutufariji.

Tunafurahi sana kuona maendeleo ya kiroho ambayo Phillip, ndugu mdogo wa Ben, amefanya. Ana miradi mizuri ya kiroho na anatuletea furaha nyingi. Ameongoza mafunzo kadhaa ya Biblia, na hata alijifunza pamoja na mwalimu fulani. Lakini sote tunatamani sana kumwona Ben tena katika ulimwengu mpya ambao Yehova ameahidi.—Ayubu 14:14, 15; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:1-4.

Tumebarikiwa kuwa na watu wa familia wenye upendo wanaotufariji. Mwana wangu wa kambo, Jonathan, anamtumikia Yehova pamoja na mke wake, Kenna. Vilevile, mwana wangu mdogo niliyempata katika ndoa yangu ya kwanza anayeitwa Chris, anamtumikia Yehova pamoja na mke wake, Lorie. Wajukuu wetu, Woodrow na Jonah hutoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Baba yangu alikufa mwaka wa 1987, lakini mama yangu mwenye umri wa miaka 84 bado anamtumikia Yehova, na vilevile ndugu yangu John, na mke wake Cherry.

Nimeona kwamba maneno haya ya Yesu ni ya kweli: “Hakuna awezaye kutumikia kama mtumwa mabwana-wakubwa wawili . . . Hamwezi kutumikia kama watumwa Mungu na Utajiri.” Hata sasa sanaa inaweza kuchukua wakati na nguvu nyingi. Hiyo ndiyo sababu nimejifunza umuhimu wa kuwa na busara na kuwa macho, ili sanaa isiwe tena jambo kuu maishani mwangu. Ni bora sana kufuata ushauri huu wa mtume Paulo: “Ndugu zangu wapendwa, iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.”—1 Wakorintho 15:58.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 J. F. Rutherford aliongoza kazi ya Mashahidi wa Yehova hadi kifo chake mwaka wa 1942.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Ndege yangu huko Chinle mwaka wa 1996

[Picha katika ukurasa wa 19]

Sanamu ya shaba inayoitwa “No Time to Dally” (Hakuna Wakati wa Kurandaranda)

[Picha katika ukurasa wa 21]

Mkutano wa kujifunza Biblia mahali ambapo Jumba la Ufalme limejengwa

[Picha katika ukurasa wa 21]

Mimi na mke wangu Karen

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kuwahubiria watu wanaoishi katika nyumba ya kawaida ya Wanavajo