Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msaada na Faraja Kutoka Sehemu Nyingi

Msaada na Faraja Kutoka Sehemu Nyingi

Msaada na Faraja Kutoka Sehemu Nyingi

WATU walijitolea kutoka sehemu mbalimbali za Marekani na kutoka nchi nyinginezo. Mmojawapo wa watu hao waliojitolea alikuwa Tom (aliyeonyeshwa juu), mzimamoto kutoka Ottawa, Kanada, mwenye umri wa miaka 29. Yeye alimwambia mwandishi wa Amkeni! hivi: “Niliona matukio hayo kwenye televisheni na nikataka kuwasaidia wazimamoto wenzangu huko New York. Nilianza safari yangu Ijumaa na kufika katika eneo la mlipuko Jumamosi ili kusaidia. Niliwekwa katika kikundi kilichoitwa eti kikosi cha kutumia ndoo. Kazi yetu ilikuwa kuondoa vifusi na kuvitia kwenye ndoo moja baada ya nyingine.

“Tuliyapekua magofu kwa makini, pole kwa pole tukitafuta vifaa ambavyo huenda vingetusaidia kuwatambua wazimamoto waliokuwa wamekufa. Nilipata chombo aina ya Halligan, kilichotumiwa kufungua milango iliyofungwa na vilevile kutenganisha vyuma kutoka kwa mabomba ya mipira ya kuzima moto. Tulijitahidi kufanya kazi hiyo. Tukiwa wafanyakazi wa kujitolea 50, ilichukua muda wa saa mbili kujaza lori moja la takataka.

“Katika siku ya Jumatatu, Septemba 17, tulifukua baadhi ya miili ya wazimamoto waliokuwa wameenda kwenye jengo hilo siku ya Jumanne, Septemba 11. Sitasahau kamwe nilichoona—waokoaji wote waliacha kufanya kazi, wakatoa helmeti zao, na kusimama ili kuonyesha heshima kwa wenzetu waliokufa.

“Nikiwa nimesimama nikiangalia eneo la mlipuko nilishangazwa na namna maisha yalivyo mafupi siku hizi. Ilinifanya nifikirie maisha, kazi, na familia yangu. Ijapokuwa hatari inayohusika, ninafurahia kazi yangu ya kusaidia watu na hata kuokoa uhai.”

Mashahidi Wasaidia

Karibu watu 70 walipata usalama katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, siku mbili za kwanza za msiba huo. Watu waliopoteza makao na mizigo yao hotelini, walipewa mahali pa kukaa, mavazi na chakula. Huenda msaada mkubwa zaidi ambao walipata ni faraja kutoka kwa wazee Wakristo wenye ujuzi.

Mashahidi wa Yehova walituma pia vifaa vilivyohitajika na vyakula kwa wafanyakazi waliotafuta na kuokoa watu katika eneo la mlipuko. Waliandaa pia magari ya kuwasafirisha wazimamoto kutoka kwenye idara yao hadi kwenye eneo la uokoaji. Ricardo (aliye upande wa juu, kulia), Shahidi mwenye umri wa miaka 39 anayefanya kazi ya kuondoa takataka, alikuwa miongoni mwa mamia ya wengine ambao waliondoa tani nyingi za vifusi siku baada ya nyingine. Ricardo alimwambia mwandishi wa Amkeni! hivi: “Hali zilikuwa zenye kufadhaisha sana, hasa kwa wazimamoto waliotafuta wenzao waliopotea. Niliona wakimvuta mzimamoto mmoja aliyekuwa bado hai. Mzimamoto mwingine alikufa baada ya kuangukiwa na maiti. Wazimamoto wengi walilia sana, nami sikuweza kujizuia, nililia pia. Katika siku hiyo, hakuna mtu aliyekuwa na ujasiri kama wazimamoto hao.”

“Wakati na Tukio Lisilotazamiwa”

Maelfu ya watu walikufa katika msiba huo. Miongoni mwao ni Mashahidi 14, waliokuwa katika eneo la msiba huo au karibu na hapo. Joyce Cummings, mwenye umri wa miaka 65 ambaye ni mwenyeji wa Trinidad, alikuwa ameenda kumwona daktari wa meno karibu na Jengo la World Trade Center. Inasikitisha kwamba msiba ulitokea wakati huo. Yaelekea moshi ulimlemea na upesi akapelekwa kwenye hospitali iliyokuwa karibu, lakini hakuweza kuokolewa. Kisa chake kilikuwa kimojawapo cha visa vya watu wanaopatwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11, NW) Joyce alijulikana kama mweneza-evanjeli mwenye bidii.

Calvin Dawson (ona sanduku) alikuwa anafanya kazi na shirika la udalali kwenye orofa ya 84 ya mnara wa kusini. Alikuwa ofisini mwake na aliuona vizuri mnara wa kaskazini mara tu ulipogongwa na ndege. Mwajiri wake ambaye hakuwepo wakati huo alimpigia simu kuuliza kilichokuwa kimetendeka. Mwajiri huyo alisema: “Calvin alijaribu kuniambia alichoona. ‘Watu wanaruka!’ yeye alisema. Nikamwambia atoke na awaambie wengine pia watoke ofisini.” Calvin hakufaulu kutoka nje. Mwajiri huyo aliendelea kusema: “Calvin alikuwa mwanamume mzuri aliyependwa nasi sote, hata na wale miongoni mwetu wasio watu wa dini. Tulivutiwa sana na wema wake na fadhili zake kwa wengine.”

Shahidi mwingine aliyekufa pia alikuwa James Amato (upande wa chini kulia, kwenye ukurasa wa kushoto), baba ya watoto wanne aliyekuwa afisa wa idara ya zimamoto ya New York. Waliomjua walisema kwamba alikuwa mtu mwenye ujasiri sana hivi kwamba “angeingia ndani ya nyumba inayoteketea huku wengine wakitoroka.” James alipandishwa cheo kuwa msimamizi wa kikosi kikubwa cha wazimamoto baada ya kifo chake.

Shahidi mwingine mzimamoto mwenye ujuzi wa miaka saba, alikuwa George DiPasquale, mume wa Melissa na baba ya binti wa miaka miwili, Georgia Rose. George alikuwa mzee wa kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova kwenye Kisiwa cha Staten. Alikuwa kwenye orofa ya kumi mnara wa kusini ulipoporomoka. Yeye pia alikufa alipokuwa akijaribu kuwaokoa wengine.

Hao ni wawili tu miongoni mwa mamia ya wazimamoto, polisi, na wafanyakazi wa dharura waliopoteza maisha zao wakijaribu kwa ujasiri kuwaokoa watu. Ujasiri wa waokoaji hao hauwezi kusahauliwa kamwe. Baadaye, meya wa jiji la New York City, Rudolph Giuliani, aliambia kikundi cha wazimamoto waliopandishwa vyeo hivi: ‘Utayari wenu wa kujitoa kwa ujasiri wakati wa hali ngumu sana ni kichocheo kwetu sote. Na hakuna watu walio na mfano bora wa ujasiri kuliko watu wa Idara ya Zimamoto ya Jiji la New York.’

Kuwafariji Wengine

Baada ya msiba huo, Mashahidi wa Yehova karibu 900,000 huko Marekani waliazimia kwa pamoja kuwafariji wale waliokuwa wakiomboleza. Upendo wao kwa jirani uliwasukuma kuwafariji waombolezao. (Mathayo 22:39) Wanapohubiri, wamejitahidi pia kuwaonyesha watu lile tumaini pekee lililopo kwa wanadamu wanaoteseka.—2 Petro 3:13.

Mashahidi waliwahurumia watu waliokutana nao. Kusudi lao lilikuwa kuwafariji watu kupitia kwa Maandiko na kuiga kielelezo chenye kuburudisha cha Kristo, aliyesema: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi. Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:28-30.

Vikundi vya wazee wenyeji wa makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ya Manhattan, walikubaliwa kwenda kwenye eneo la mlipuko ili kuzungumza na kuwafariji waokoaji. Matokeo yalikuwa mazuri. Wahudumu hao walisema: “Wanaume hao walitokwa na machozi tulipowasomea maandiko.” Waokoaji wengine walikuwa katika mashua kwenye bandari wakipumzika. “Wanaume hao waliviinamisha vichwa vyao wakiwa wamefadhaishwa na yale waliyoona. Tuliketi chini pamoja nao na kuwasomea maandiko kutoka kwa Biblia. Walitushukuru sana kwa kufika huko na kutuambia kwamba walihitaji faraja hiyo sana.”

Watu waliotembelewa baada ya msiba walitaka vichapo vya kusoma, walipewa maelfu ya broshua. Baadhi yazo zilikuwa, Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, Je! Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote?, na Je! Kweli Mungu Anatujali? Pia makala za kwanza katika nakala mbili za Amkeni! zilipewa uangalifu wa pekee: “Mbinu Mpya za Ugaidi” (Mei 22, 2001) na “Kupambana na Mfadhaiko wa Tukio Lenye Kutisha” (Agosti 22, 2001). Katika visa vingi, Mashahidi walieleza kuhusu tumaini la Biblia la ufufuo. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Huenda mamilioni walifikiwa na ujumbe huo wenye kufariji.

Msiba Huo Unapaswa Kutuchochea Kufikiri

Msiba kama huo uliotokea katika jiji la New York City, unapaswa kutuchochea kufikiria namna tunavyotumia maisha yetu. Je, tunajali masilahi yetu tu au tunajaribu kuongeza furaha ya wengine? Nabii Mika aliuliza hivi: “BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” (Mika 6:8) Unyenyekevu unapaswa kutusukuma kusoma Neno la Mungu ili kujua tumaini hakika la wafu na kile ambacho Mungu atafanya hivi karibuni ili kurudisha hali za Paradiso katika dunia hii. Iwapo ungependa kujua zaidi kuhusu ahadi za Biblia, tunakutia moyo uwasiliane na Mashahidi wa Yehova wanaoishi karibu nawe.—Isaya 65:17, 21-25; Ufunuo 21:1-4.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

SALA YA TATIANA

Lena, mke wa Calvin Dawson, alimwambia mwandishi wa Amkeni! jinsi binti yake mwenye umri wa miaka saba alivyosali siku chache tu baada ya kujua kwamba baba yake hangerudi nyumbani. Baada ya Lena kusali, Tatiana alimuuliza mama yake kama angeweza kusali pia. Mama yake alikubali. Tatiana alisali hivi: “Yehova, Baba yetu wa mbinguni, tunakushukuru kwa chakula hiki na kwa uhai wa siku hii. Na tunaomba kwamba roho yako iwe pamoja nami na Mama ili tuwe na nguvu. Na tunaomba roho yako iwe na Baba, ili apate nguvu atakaporudi. Naye atakaporudi, atakuwa mzuri, mwenye nguvu, na furaha na afya, nasi tutamwona tena. Katika jina la Yesu . . . samahani, usisahau kumsaidia Mama kuwa na nguvu. Amina.”

Bila kujua kama Tatiana alielewa, Lena alimwambia hivi: “Tiana, hiyo ilikuwa sala nzuri. Lakini, mpenzi, unajua kwamba Baba harudi?” Mara moja Tatiana alishangaa. “Harudi?” akauliza. Mama yake akamwambia, “La. Nafikiri nilikuambia hivyo. Nilifikiri ulielewa kwamba Baba harudi.” Tatiana akasema: “Lakini uliniambia sikuzote kwamba atarudi katika ulimwengu mpya!” Alipotambua hatimaye kile bintiye alichomaanisha, Lena alisema: “Pole Tatiana, nilikuelewa vibaya. Nilifikiri ulimaanisha kwamba Baba atarudi kesho.” Lena aendelea kusema: “Nilifurahi kujua kwamba ulimwengu mpya ulikuwa halisi kwake.”