Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nitashughulikaje na Watu Wenye Hasira?

Nitashughulikaje na Watu Wenye Hasira?

Vijana Huuliza . . .

Nitashughulikaje na Watu Wenye Hasira?

“Alikuwa na hasira kali. Nafikiri alitaka kunipiga kwa sababu aliona nilikuwa mdogo. Nilipokuwa nikisonga nyuma, nilisema: ‘Hebu ngoja! Ngoja kidogo! Ngoja kidogo! Mbona unataka kunipiga? Sijakufanya lolote. Hata sijui umekasirishwa na nini. Je, twaweza kusuluhisha jambo hilo?’”—David, mwenye umri wa miaka 16.

JE, UMEWAHI kukasirikiwa na mtu mkatili? Biblia ilitabiri kwamba watu leo wangekuwa “wakali, wasio na upendo wa wema.” (2 Timotheo 3:3) Hata ingawa umejaribu uwezavyo kuepuka “urafiki na mtu mwenye hasira nyingi . . . , mtu wa ghadhabu nyingi,” kuna nyakati ambazo huwezi kuepuka watu wenye hasira. (Mithali 22:24) Utafanya nini ukijikuta katika hali kama hiyo?

Unalopaswa Kufanya Mtu Anapokukasirikia

Huenda vijana wengi siku hizi wakaghadhibika wakati mtu anapowakasirikia. Lakini kufanya hivyo hutokeza huzuni nyingi zaidi. Isitoshe, usipojidhibiti utakuwa sawa na mtu aliyeghadhibika. Andiko la Mithali 26:4 husema hivi: “Usimjibu mpumbavu sawasawa na upumbavu wake; usije ukafanana naye.” Kijana anayeitwa Jeremy alijionea ukweli wa maneno hayo kupitia hali ngumu. Alieleza yaliyotukia mezani wakati wa chakula cha mchana shuleni: “Kulikuwa na kikundi cha wavulana fulani ambao sikuzote walitaniana na kuwafanyia wengine mzaha. Walizungumza juu yangu mara nyingi. Kwa kawaida nilipuuza mambo waliyosema. Hata hivyo, wakati mmoja wao alipozungumza kuhusu mamangu, nilishindwa kujidhibiti na nilimshambulia kwa hasira kali.” Matokeo yakawa nini? Jeremy alisema hivi: “Alinitandika kwelikweli.”

Biblia hutoa shauri hili la hekima: “Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.” (Mithali 15:1) Naam, ukisema “neno liumizalo” wakati mtu anapokukasirikia, jambo hilo litafanya hali iwe mbaya zaidi. Hata hivyo, mara nyingi jawabu la upole laweza kutuliza mambo na kumaliza uhasama.

Kumbuka David aliyetajwa mwanzoni. Alimwomba yule mchokozi amweleze ni nini kilichomkasirisha. Mtu fulani alikuwa ameiba chakula chake cha mchana, na alimfokea tu mtu aliyekutana naye kwanza. David alimwambia hivi: “Hutapata chakula chako cha mchana kwa kunipiga.” Kisha David akapendekeza waende kwenye mkahawa. David alisema hivi: “Kwa kuwa nilimjua muuzaji kwenye mkahawa huo, nilimsaidia apate chakula kingine. Alinishukuru, na baada ya hapo akawa mwenye urafiki.” Je, waona jinsi maneno ya upole yalivyo na nguvu? Kama mithali moja inavyosema, “ulimi laini [mpole, NW] huvunja mfupa.”—Mithali 25:15.

Je, Mtu Mpole Ni Dhaifu au Mwenye Nguvu?

Ni kweli kwamba huenda watu wasipende wazo la kuwa na “ulimi mpole.” Huenda ikaonekana kwamba kulipiza hasira kwa hasira ni ishara ya ukakamavu au ya uanaume. Huenda hata ukahofu kwamba ukiwa mpole, wengine watafikiri wewe ni dhaifu. Lakini kuwa mpole kwamaanisha nini? Kwa mujibu wa kitabu kimoja cha marejeo, kuwa mpole kwamaanisha kuwa mwanana. Hata hivyo, kitabu hicho chaongezea kusema hivi: “Uanana huo unaambatana na nguvu kama za chuma.” Hivyo, upole hauonyeshi kwamba mtu ni dhaifu bali unaweza kuonyesha kwamba ana nguvu. Jinsi gani?

Sababu moja ni kwamba mtu mpole hutuliza hali na hapeperushwi ovyoovyo. Kwa upande mwingine, mtu ambaye si mpole huonekana kuwa hana uhakika, mwenye kukata tamaa, au hata mwenye kuhangaika. Pia, yeye hukosa kujidhibiti. Kwa kuwa hawezi kudhibiti hisia zake, yamkini yeye huzozana na watu mara nyingi. Naam, “asiyetawala roho yake ni mfano wa mji uliobomolewa, usio na kuta.” (Mithali 25:28) Hivyo, mtu mpole ndiye mwenye nguvu!

Watu Wapole Wanaotajwa Katika Biblia

Fikiria mfano wa Yesu Kristo. Alisema kwamba yeye ni “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni.” (Mathayo 11:29) Hakuwa kamwe mkatili wala mkaidi, na hakulipiza uovu kwa uovu. Kwa hakika, mtume Petro, aliyekuwa rafiki ya Yesu, aliripoti hivi: “[Yesu] alipokuwa akitukanwa, hakuwa akitukana kwa kurudisha. Alipokuwa akiteseka, hakutisha, lakini alifuliza kujikabidhi mwenyewe kwa yeye ambaye huhukumu kwa uadilifu.” (1 Petro 2:23) Hata hivyo, kumbuka kwamba Yesu huyohuyo ndiye ‘aliingia katika hekalu na kuwafukuza nje wale wote waliokuwa wakiuza na kununua.’ (Mathayo 21:12) Na iwapo angehitaji msaada wa Mungu, Yesu angewaita “malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika”! (Mathayo 26:53) La, hakuwa mnyonge.

Pia, fikiria mfano ambao Mwamuzi Gideoni aliweka, kama ilivyorekodiwa katika Biblia kwenye Waamuzi 8:1-3. Baada ya kupata ushindi mkubwa vitani, baadhi ya maaskari wa kabila la Efraimu waliudhika kwa sababu walihisi kwamba hawakuwa wameshirikishwa vitani. “Kwa nini wewe kututendea sisi kama haya? hata usituite, hapo ulipokwenda kupigana na Midiani?” wakauliza maaskari hao. “Nao wakateta naye sana.” Gideoni alikuwa “shujaa.” (Waamuzi 6:12) Angewashambulia kwa urahisi kwa sababu ya uchokozi wao. Badala yake, alitoa jibu la upole ambalo liliwanyamazisha kabisa watu hao wakali. Gideoni aliuliza hivi: “Je! mimi nimefanya nini sasa kama mlivyofanya ninyi?” Jibu hilo la upole lilikuwa na matokeo gani? “Hasira zao walizokuwa nazo juu yake zikatulia.”

Hatimaye, fikiria simulizi la Biblia kuhusu mwanamke aliyeitwa Abigaili. Daudi alikuwa akijificha akimtoroka adui yake Sauli, mfalme wa Israeli. Japo walikuwa uhamishoni, wanaume wa Daudi waliwalinda Waisraeli wenzao mara nyingi. Mtu mmoja waliyesaidia alikuwa mume wa Abigaili, Nabali, aliyekuwa tajiri sana. Hata hivyo, Nabali alikuwa “hana adabu, tena mwovu katika matendo yake.” Wanaume wa Daudi walimwomba Nabali chakula walipokuwa na uhitaji. Badala ya kushukuru kwa sababu wanaume wa Daudi walikuwa wamemlinda bila malipo, Nabali ‘aliwatukana’ wajumbe wa Daudi wala hakuwapa chochote.—1 Samweli 25:2-11, 14.

Daudi aliposikia hilo, alikasirika na kuwaamuru wanaume wake hivi: “Haya! jifungeni kila mtu upanga wake.” Daudi na wanaume wake walikuwa wanakwenda kumwua Nabali na wanaume wote wasio na hatia wa nyumba yake, lakini Abigaili akaingilia kati. Alimlaki Daudi kwa kumpa zawadi ya vyakula na vinywaji. Aliomba msamaha kwa ajili ya ukatili wa mumewe na akamsihi Daudi asiwaue watu wasio na hatia.—1 Samweli 25:13, 18-31.

Maombi ya unyenyekevu ya Abigaili yalizuia hasira ya Daudi. Kwa hakika, Daudi alipong’amua jinsi hasira yake ilivyokuwa hatari, alisema hivi: “Na ahimidiwe BWANA, Mungu wa Israeli, ambaye amekuleta hivi leo kunilaki; na ibarikiwe busara yako, na ubarikiwe wewe, uliyenizuia hivi leo nisimwage damu, wala kujilipiza kisasi kwa mkono wangu mwenyewe.” (1 Samweli 25:32-35) Naam, katika hali nyingi “jawabu la upole” laweza kutuliza ghadhabu ya watu wengine. Hata hivyo, vipi ikiwa jawabu lako la upole halina matokeo yoyote?

“Ondoka”

Unaweza kuepuka kuchochea ghadhabu kwa kuondoka tu. Biblia husema hivi: “Moto hufa kwa kukosa kuni.” Pia inatoa shauri hili: “Acheni ugomvi [“ondoka,” NW] kabla haujafurika.” (Mithali 17:14; 26:20) Merissa, mwenye umri wa miaka 17, alisema hivi: “Kijana mmoja mashuhuri shuleni alinijia na akataka tuzungumze. Aliniambia kwamba mimi ni mrembo. Punde si punde, msichana mpenzi wake akanijia akiwa na hasira kali. Alinilaumu kwa kuchezacheza na kijana huyo na alitaka tupigane! Nilijaribu kumweleza yaliyotukia, lakini hakutaka kusikiliza. Baada ya saa za shule alirudi akiwa na wasichana wengine ili kunipiga! Nilimwita mlinzi mara moja, na nikamweleza msichana huyo mwenye hasira kwamba sitaki vita na kwamba kijana huyo ndiye aliyenijia. Baada ya hapo niliondoka.” Merissa hakukubali kuongozwa na hisia zake. Mbali na kuepuka vita alichukua hatua za kujilinda. Kama Mithali 17:27 inavyosema, “azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; na mwenye roho ya utulivu ana busara.”

Hata hivyo, vipi ikiwa wewe ndiwe uliyemkasirisha mtu mwingine—labda bila kukusudia? Omba msamaha na ufanye hivyo haraka! Huenda jambo hilo likazuia hasira ya mtu huyo. Hizi ni nyakati zenye mikazo mingi, na watu wengi hukasirika upesi. Lakini ukitumia kanuni za Biblia katika shughuli zako, huenda utaepuka kukasirikiwa.

[Picha katika ukurasa wa 24]

“Jawabu la upole hugeuza hasira”

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nyakati nyingine inakubidi uondoke tu