Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Masimulizi ya Imani Kutoka Gereza Maarufu

Masimulizi ya Imani Kutoka Gereza Maarufu

Masimulizi ya Imani Kutoka Gereza Maarufu

Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova hujitolea kutembelea magereza mbalimbali ili kuwasaidia wafungwa wanaotaka kumkaribia Mungu. Kwa muda wa zaidi ya miaka 20, tumefanikiwa kuwa na programu ya elimu ya Biblia katika gereza la serikali huko Atlanta, Georgia, Marekani. Kujifunza Biblia gerezani si jambo rahisi. Sisi wahudumu tuliojitolea tumehubiria wahalifu walioiba benki, wanyang’anyi, wauaji, walanguzi wa dawa za kulevya, walaghai, na wale ambao wametenda matendo haramu ya kingono. Watu kama hao wamesaidiwa jinsi gani?

KWANZA labda ungependa kujua ni lini Mashahidi wa Yehova walipoingia katika gereza hilo kwa mara ya kwanza na kwa sababu gani. Ilikuwa tarehe 4 Julai mwaka wa 1918, wakati kikundi cha wahudumu wanane Wakristo mashuhuri walipopanda hatua 15 za ngazi ya mawe ya gereza hili. Ikiwa desturi ya siku hizo ilifuatwa, walikuwa wamefungwa pingu mikononi ambazo ziliunganishwa na minyororo iliyokuwa imekazwa tumboni, miguu yao ikiwa imefungwa kwa pingu vilevile. Wafungwa hao wapya walikuwa wanaume wa kiroho ambao walisimamia kazi ya Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Wanaume hao hawakujua kwamba ingechukua karibu mwaka mzima kuthibitisha kwamba kifungo chao hakikuwa cha haki. Hatimaye, Machi 1919, Mashahidi hao wanane waliteremka ngazi iyo hiyo wakiwa huru, bila pingu. Baadaye waliondolewa hatia kabisa mahakama ilipoamua kufuta mashtaka. *

Wanaume hao Wakristo waliofungwa huko Atlanta walifunza madarasa ya Biblia humo gerezani. Baadaye, mmoja wa wafungwa hao wanane, A. H. Macmillan, aliripoti kwamba makamu wa afisa wa gereza aliyekuwa mwenye uhasama mwanzoni, alisukumwa kusema hivi hatimaye: ‘Masomo hayo ni mazuri ajabu!’

Leo, baada ya zaidi ya miaka 80, madarasa ya Biblia yenye matokeo yanaendelea kuwanufaisha wafungwa katika gereza hilohilo. Mara kadhaa, maafisa wa gereza wamewatunukia baadhi ya Mashahidi wa Yehova wanaotembelea gereza hilo tuzo za heshima. Mafanikio ya programu ya elimu ya Mashahidi wa Yehova yametajwa vilevile katika jarida la taifa la Volunteer Today, linalochapishwa na Idara ya Sheria ya Marekani, Shirika la Magereza ya Serikali.

Madarasa hayo ya Biblia yanasaidia sana wafungwa kuboresha mwenendo wao. Kwa sababu hiyo, baadhi ya wafungwa wameachiliwa mapema. Wadhihaki huenda wakadhani kwamba wafungwa wanajifunza Biblia pamoja nasi ili tu waachiliwe mapema. Ijapokuwa wachache wamekuwa na nia hiyo, wengi wamekuwa na nia inayofaa. Mara nyingi tunafurahi tunapopata habari kwamba wanafunzi wetu wanaendelea kudumisha mwenendo mzuri wa Kikristo miaka mingi baada ya kuachiliwa. Yafuatayo ni mambo machache ambayo tumeyaona katika gereza hili kubwa maarufu.

Wahamiaji Waliofungwa Wanapata Tumaini

Mapema katika miaka ya 1980, sisi tuliohubiri katika gereza hilo la Atlanta tulikuwa na pendeleo la kuwasaidia wahamiaji wengi waliofungwa. Baadhi yao walifanya mabadiliko makubwa ajabu.

Mwanzoni Raoul * alikuwa mfungwa hatari sana. Yeye na rafikiye mmoja walikuwa wahalifu sugu, na walikuwa wamefungwa kwa sababu ya uuaji. Wazee waliowasaidia walisema kwamba watu hao walikuwa wakatili sana. Raoul alikuwa na maadui walionuia kumwua. Mwanamume mmoja alikuwa amekula kiapo kumwua Raoul, na Raoul vilevile alikuwa amekula kiapo kumwua mwanamume huyo. Raoul aliogopa sana wakati yule adui wake mkuu alipohamishwa Atlanta. Ilikuwa wazi kwamba maadui hao wangekutana siku moja kwenye ua wa gereza, chumba cha kulia chakula, au kwenye jengo la kulala. Hata hivyo, baada ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, Raoul alifanya mabadiliko makubwa katika mwenendo wake, mawazo yake, na sura yake. Hatimaye, wakati wanaume hao wawili walipokutana katika ua wa gereza, yule adui hata hakumtambua Raoul! Lile pambano la kuuana lililotarajiwa halikutukia kamwe.

Raoul alipoamua kubatizwa ili aonyeshe kwamba amejiweka wakfu kwa Mungu, beseni ya ubatizo ilihitajika. Kasisi wa gereza alisaidia kwa kutoa jeneza jeusi kwa ajili ya ubatizo. Jeneza hilo lilijazwa maji. Lakini ilionekana kana kwamba Raoul alikuwa mkubwa kuliko jeneza hilo. Kwa hiyo, wazee wawili walisaidiana kumbatiza Raoul ili wahakikishe kwamba alikuwa ametumbukizwa kabisa, jinsi Biblia inavyoagiza. (Luka 3:21, NW, kielezi-chini) Leo, Raoul yuko huru naye anaendelea kutumikia akiwa mhudumu Mkristo mwenye bidii.

Katika mwaka wa 1987 uamuzi wa kufukuza nchini wahamiaji wengi waliofungwa ulisababisha ghasia kubwa sana gerezani iliyoripotiwa na vyombo vya habari ulimwenguni pote. Watu walitekwa nyara. Hata hivyo, watu wengi hawajui kwamba kulikuwa wafungwa wahamiaji wajasiri ambao walihatarisha maisha yao kwa kukataa kushiriki katika ghasia hiyo mbaya iliyotokea ghafula. Hao walikuwa wanafunzi wa madarasa yetu ya Biblia. Wanaume hao, ambao mbeleni walikuwa tayari kupigana hadi kifo, hawakushiriki katika ghasia hiyo yenye ukatili iliyoharibu mali nyingi. Hiyo inathibitisha wazi kwamba Biblia ina nguvu ya kugeuza hata wahalifu wakatili wawe Wakristo wanaopenda amani!—Waebrania 4:12.

Kupata Msamaha

Tunakumbuka vilevile kisa cha James. Alikuwa Shahidi wa Yehova mbeleni lakini alijiachilia adhoofike kiroho. Alishindwa kukinza kishawishi, akatumia udanganyifu kuiba fedha za benki. Alitengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo na kufungwa katika gereza hilo la serikali la Atlanta. Baadaye alituambia hivi: “Kipindi hicho ndicho kilichokuwa kibaya zaidi katika maisha yangu.”

Maisha gerezani yalikuwa magumu. “Nilihisi upweke sana na nilikata tamaa kabisa,” akakumbuka James. Hata hivyo, kufungwa kwake katika chumba kidogo cha gereza kulifanya ajichunguze kabisa. Alieleza hivi: “Kile kilichonihuzunisha hasa hakikuwa hali ngumu ya maisha gerezani bali jinsi nilivyoshindwa kutimiza matakwa ya Baba yangu wa mbinguni.” Baada ya miezi kadhaa mfungwa mmoja aliyekuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi hao waliojitolea alimwendea James na kumwalika ahudhurie madarasa ya mafunzo ya Biblia. Mwanzoni James alikataa kwa kuwa aliona aibu. Lakini mwanamume huyo mchanga hakuacha kumkaribisha, na hatimaye James akahudhuria mkutano mmoja wa Jumapili.

Alivutiwa sana kuona jinsi Mashahidi waliofunza darasa hilo walivyojali wanafunzi na kuwaonyesha upendo. Baadaye, aligundua jambo jingine lililompendeza. Kwa sababu ya yale ambayo James alikuwa ameona mbeleni, alidhani kwamba watu wote wa dini waliojitolea kusaidia wafungwa walilipwa mshahara mkubwa kwa kazi yao. Lakini alishangaa alipojua kwamba Mashahidi hawakudai malipo yoyote wala kupokea fedha taslimu kwa utumishi wao.—Mathayo 10:8.

James alianza kutazamia kila mkutano kwa hamu. Ndugu walioongoza mikutano hiyo walikuwa wenye fadhili na wenye kutia moyo. Alimheshimu hasa mzee mmoja. James anasema hivi: “Nilingoja ziara zake kwa hamu sana kwa kuwa alifanya kweli ya Neno la Mungu ivutie; alikuwa mtu hodari kwa kuchochea wengine. Alinisaidia kuona umuhimu wa kuchunguza Biblia kindani kabisa, ili nielewe kweli na hiyo kweli iingie moyoni mwangu, na hasa niweze kukuza akili ya Kristo.”

James hakuweza kuamini kwamba Mungu angemsamehe makosa yake. Ni nini kilichomsaidia? “Jinsi wanaume hao waaminifu waliojidhabihu walivyotutendea ilituonyesha wazi kwamba Mungu alikuwa ametusamehe. * Nilielewa jambo moja vizuri: Ijapokuwa dhambi zangu zilikuwa nzito, ndugu huyo hakudokeza kamwe kwamba Mungu hangeweza kunisamehe. Yehova hakuniacha kamwe. Aliona toba yangu ya moyoni na kwamba nimeacha mwenendo wangu wa upumbavu na udanganyifu; naye amenibariki sana.” Ndiyo, James alirudishwa katika kutaniko la Kikristo. Amedumu akiwa Mkristo mtendaji na mwenye bidii tangu aachiliwe yapata miaka kumi iliyopita. Mke wake na familia yake wanafurahi sana kwa kuwa sasa yeye ni mtumishi wa huduma na hivi majuzi alitoa hotuba yake ya kwanza ya watu wote.

Kuona Njia

Tulikutana na Johnny mapema katika miaka ya 1990. Familia ya Johnny walishirikiana kwa kadiri fulani na Mashahidi wa Yehova alipokuwa akikua, lakini hakuna yeyote kati yao aliyekuwa imara kiroho ili kumwongoza Johnny kiroho na kiadili. Hatua kwa hatua, Johnny akawa mhalifu. Alihukumiwa kifungo katika kambi ya gereza iliyopakana na gereza la Atlanta. Alipokuwa humo kambini alisikia juu ya madarasa yetu ya Biblia naye akaamua kuhudhuria.

Mwanzoni Johnny hakujua kusoma vizuri. Hata hivyo, alikuwa na hamu sana ya kujifunza juu ya Yehova na Yesu Kristo hivi kwamba aliazimia kujifunza kusoma kwa ufasaha. (Yohana 17:3) Mara nyingi wafungwa wanaohudhuria madarasa yetu wanasaidiwa kuwa wasomaji wazuri, hasa kuelewa yale wanayosoma na kusoma mbele za watu. Johnny alijifunza kwa bidii sana hivi kwamba wanafunzi wenzake walianza kumwona kuwa mwanafunzi wa Biblia bora kabisa.

Miezi mingi baadaye, Johnny alihamishwa hadi gereza la serikali huko Talladega, Alabama, ili ahudhurie masomo ya dawa za kulevya. Alipowasili huko, alianza mara moja kuhudhuria mikutano ya Kikristo ambayo Mashahidi wa Yehova walifanya huko. Aliendelea kushiriki kwa ukawaida hadi alipoachiliwa hatimaye. Siku hiyo ya furaha ilipowadia, Johnny hakupoteza wakati bali aliwasiliana mara moja na Mashahidi wa Yehova katika mji wa kwao. Alikaribishwa kwa uchangamfu, naye akaendelea kujifunza na kufanya maendeleo ya kiroho.

Shauku ya Johnny na upendo wake kwa kweli ya Biblia umemtia moyo mama yake pia kushirikiana zaidi na kutaniko la Kikristo. Johnny anamtia moyo mama yake na kumsaidia sana. Hivi majuzi alibatizwa ili kuonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa Yehova Mungu, naye anaendelea kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya Kikristo.

Mavuno Makubwa

Katika miaka 20 iliyopita, zaidi ya wafungwa 40 katika gereza la Atlanta wamesaidiwa kuwa wahudumu waliobatizwa wa Mashahidi wa Yehova na wafungwa wengine 90 wamenufaika pia na mafunzo ya Biblia ya kila juma. Wafungwa wengine wamebatizwa baada ya kuachiliwa au kuhamishwa hadi magereza mengine.

Sisi ambao hutembelea gereza hilo maarufu kila juma ili kuwasaidia watu wanaotubu kwelikweli, tunathamini huduma hiyo ya pekee ya Kikristo. (Matendo 3:19; 2 Wakorintho 7:8-13) Katika gereza hilo lenye hali isiyofurahisha, lenye minara yenye walinzi wenye silaha, maaskari, malango yanayofunguliwa kwa umeme, na seng’enge yenye wembe, sisi tumefurahishwa na kustaajabishwa kuona wahalifu waliofungwa humo wakiacha maisha yao ya uhalifu na kuwa raia wanyofu na waabudu waaminifu wa Mungu.—1 Wakorintho 6:9-11.—Imechangwa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ukitaka habari zaidi juu ya kesi hiyo, soma kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa 647-656, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 9 Majina ya wafungwa yamebadilishwa.

^ fu. 17 Toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1991, liliwatia moyo wazee Wakristo wawatembelee wengi wa wale waliotengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo. Kusudi la kufanya hivyo ni kuwatia moyo wamrudie Yehova.—2 Wakorintho 2:6-8.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20, 21]

“Mliwahi Kuwakaribisha Baadhi ya Marafiki Wangu wa Karibu”

MNAMO Aprili 1983, Frederick W. Franz, aliyekuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alitembelea gereza la serikali ya Marekani huko Atlanta. Alikuwa na hamu sana ya kutembelea gereza hilo. Alipoingia katika jengo hilo, alipaza sauti na kumwambia hivi askari aliyeketi kwenye meza ukumbini: “Ninataka ujue kwamba mliwahi kuwakaribisha baadhi ya marafiki wangu wa karibu hapa!” Askari huyo alitatanishwa. Franz alimaanisha nini?

Miaka 64 iliyopita Joseph F. Rutherford na washiriki wake saba walikuwa wameshtakiwa kwa wongo kwamba wamefanya njama, na kuhukumiwa isivyo haki. Baadaye, Rutherford na Franz wakawa marafiki wa karibu na walifanya kazi pamoja. Sasa, zaidi ya miaka 40 baada ya kifo cha Rutherford—na yeye mwenyewe alipokuwa na umri wa miaka 90 hivi—Franz alifurahia kutembelea mahali ambapo rafiki yake alikuwa amefungwa miaka mingi iliyopita. Bila shaka alitafakari ile kazi ambayo Rutherford na wenzake walikuwa wamefanya ndani ya gereza hilo. Hiyo ilikuwa kazi gani?

Muda mfupi baada ya Rutherford na wenzake kuwasili, makamu wa afisa wa gereza aliwaambia hivi: “Tutawapa kazi ya kufanya. Je, Nyinyi mwaweza kufanya kazi gani?”

A. H. Macmillan, mmojawapo wa wale wanane alijibu hivi: “Makamu, sijafanya kamwe kazi nyingine maishani mwangu isipokuwa kuhubiri. Je, kuna kazi kama hiyo huku?”

“La, bwana! Mlihukumiwa kifungo hiki kwa sababu ya kuhubiri, nakuambia sasa, hamtahubiri hapa.”

Majuma kadhaa yalipita. Wafungwa wote walipaswa kuhudhuria ibada iliyoendeshwa kila Jumapili penye mahali pa ibada, na wale waliotaka waliweza kuhudhuria shule ya Jumapili baadaye. Wanaume hao wanane waliamua kuanzisha funzo lao wenyewe la Biblia, ambalo kila mmoja wao alichukua zamu kuongoza. Baadaye Rutherford alisema: “Watu wachache wenye udadisi walianza kuja, na hata wengine zaidi wakaja.” Punde idadi ya kikundi hicho kidogo cha watu 8 iliongezeka kufikia watu 90!

Wafungwa waliitikiaje masomo hayo ya Biblia? Mfungwa mmoja alisema hivi: “Mimi nina umri wa miaka 72, na ilinibidi kufungwa gerezani ili nisikie kweli. Kwa hiyo, ninafurahi kwamba nilifungwa katika gereza hili.” Mwingine alisema hivi: “Wakati wangu wa kuachiliwa umekaribia; ninasikitika kwamba nitaachiliwa . . . Niambie ninaweza kupata watu kama nyinyi wapi nitakapoachiliwa?”

Usiku wa kuamkia kuachiliwa kwao, wanaume hao wanane walipokea barua iliyowagusa kutoka kwa mwanamume kijana aliyekuwa amehudhuria darasa lao. Aliandika hivi: “Ninataka mjue kwamba mmetia ndani yangu tamaa ya kuwa mtu bora, mwenye kustahili heshima, ikiwa itawezekana kwa mtu duni kama mimi, mwenye sifa mbaya na ambaye amekandamizwa na maisha magumu sana kubadilika hivyo. . . . Mimi ni mtu dhaifu sana, najua jambo hilo vizuri kuliko mtu yeyote mwingine, lakini nitajaribu na nitajikakamua ili mbegu ile mliyoipanda itoe mazao yake kamili, na niweze kujisaidia mimi mwenyewe na pia wale walio karibu nami. Huenda ni jambo geni kusikia mtu kama mimi akisema maneno hayo, lakini yanatoka moyoni mwangu, na ni ya kweli.”

Leo, zaidi ya miaka 80 baadaye, mbegu za kweli ya Biblia bado hupandwa na Mashahidi wa Yehova katika gereza hilo la Atlanta, na vilevile katika magereza mengine mengi.—1 Wakorintho 3:6, 7.