Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Kosa Gani Kutoka Kisiri?

Kuna Kosa Gani Kutoka Kisiri?

Vijana Huuliza . . .

Kuna Kosa Gani Kutoka Kisiri?

“Tulitoka kisiri nyumbani usiku wa manane na kwenda mkahawani ili kuwa na vijana fulani. Kisha tukaanza kurandaranda tu kwenye kilima. Wenzangu wote walivuta sigareti, ingawa mimi sikufanya hivyo kamwe. Tuliketi tu na kupiga domo, huku tukisikiliza muziki wenye mdundo mzito. Kisha tungerudi nyumbani saa 11 alfajiri kabla ya wazazi wangu kuamka.”—Tara. *

“Baba alipoenda kazini na mama yangu akiwa angali usingizini, nilitoka kisiri kupitia mlango wa mbele. Niliuacha mlango wazi ili mama asisikie nikiufunga—ulikuwa mlango wa chuma. Nilirandaranda na rafiki zangu usiku kucha. Halafu asubuhi jua lilipochomoza, ningejaribu kuingia ndani ya nyumba kisiri. Nyakati nyingine mama alitambua sikuwa ndani ya nyumba na kufunga mlango.”—Joseph.

KUTOKA KISIRI NYUMBANI—lasikika kuwa jambo la kuvutia na lenye kufurahisha. Ni fursa ya kufurahia maisha kwa muda ukiwa peke yako, fursa ya kufanya upendayo na kuwa na mtu yeyote unayetaka bila kuwajibika kwa mtu yeyote. Isitoshe, huenda umesikia rafiki zako wakijigambia mambo wanayofanya na kufurahia wanapotoka kisiri nyumbani. Kwa sababu hiyo ni rahisi kushawishiwa kujiunga nao.

Katika uchunguzi wa vijana 110 walio katika vidato vya chini na vidato vya juu katika shule ya sekondari huko Amerika Kaskazini, 55 walisema kwamba waliwahi kutoka kisiri nyumbani angalau mara moja. Wengi wao walifanya hivyo mara ya kwanza walipokuwa na umri wa miaka 14. Hali hiyo imekuwa mbaya sana hivi kwamba wataalamu wanapendekeza kwamba wazazi waweke kamsa za kielektroni ili kuzuia watoto wao kutoka nyumbani bila wao kujua. Kwa nini vijana wengi wanatoka kisiri nyumbani ingawa wanajua wazazi wao wangekasirika?

Kinachosababisha Wengine Kutoka Kisiri

Nyakati nyingine vijana hutoka kisiri nyumbani kwa sababu ya uchoshi na wanatamani kufurahi pamoja na rafiki zao. Kitabu Adolescents and Youth chasema kwamba huenda vijana wakatoka kisiri nyumbani “kwa sababu ya kizuizi walichowekewa kama vile saa za kurudi nyumbani mapema au kupewa nidhamu kwa kukatazwa kwenda kwa burudani fulani katika ujirani. Licha ya vizuizi hivyo, vijana huenda na nyakati nyingine wanafanikiwa kurudi nyumbani bila kugunduliwa.” Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 16 alieleza sababu zinazomfanya kutoka kisiri nyumbani. “Najihisi nikiwa kama mtoto mchanga na kwamba sina uhuru wa kufurahia maisha,” akasema. “Saa nilizowekewa za kurudi nyumbani ni mapema mno kuliko za vijana wengine. Na wazazi wangu hawataki niende mahali wenzangu wanaenda. . . . Hata hivyo, mimi huenda tu kisha nawadanganya.” Joseph, anayetajwa mwanzoni, alianza kutoka kisiri nyumbani akiwa na umri wa miaka 14 alipoenda kwenye burudani ya muziki wa rapu baada ya wazazi wake kumkataza asiende.

Kwa hakika, vijana wengi hawana nia mbaya wanapotoka kisiri nyumbani. Tara, mmojawapo wa vijana wanaotajwa mwanzoni, alisema hivi: “Jambo lililokuwa akilini mwetu si ‘Acheni twende tukafanye dhambi fulani nzito.’ Mimi nilitaka tu kuwa pamoja na dada yangu, naye alitaka kwenda kujifurahisha na rafikize.” Joseph alisema: “Tulirandaranda tu. Nilitaka tu kuongea na rafiki zangu na kuwa pamoja nao.” Ijapokuwa mara nyingi huenda kule kurandaranda tu na rafiki zako kusiongoze kwenye makosa mazito, vijana wengi hujikuta taabani.

Hatari Zilizopo

Mtaalamu wa afya ya akili Dakt. Lynn E. Ponton asema: “Ni kawaida kwa vijana kujasiria.” Dakt. Ponton aendelea kusema kwamba ni jambo la kawaida na labda kuna manufaa kwa vijana kutaka kujitegemea, kujaribu mambo mapya na kujikuta katika hali ngeni zenye kusisimua. Ni sehemu ya ukuzi wao. Lakini vijana wengi hujasiria na kupita mipaka yote—hasa wanapokuwa mbali na uangalizi wa wazazi wao. Gazeti la Teen lasema hivi: “Mchanganyiko wa msongo wa marika, uchoshi, nishati zisizodhibitiwa na labda kichocheo kingine kama vile pombe . . . huwafanya wajasirie vitendo hatari—na kupoteza uhai wao.” Uchunguzi mmoja uliorodhesha baadhi ya vitendo hivyo hatari vya vijana, ambavyo vilitia ndani kuendesha gari kwa kasi mno, kuharibu vitu kimakusudi, kuendesha gari wakiwa walevi, na kuiba.

Ukisha zoea kutotii, ni rahisi kufanya makosa mengine mazito. Ni kama Yesu alivyosema katika Luka 16:10: “Mtu asiye mwaminifu katika lililo dogo zaidi sana ni asiye mwaminifu katika lililo kubwa pia.” Haishangazi basi, kutoka kisiri nyumbani kwaweza kuongoza kwenye dhambi nzito. Tara alifanya uasherati. Joseph alianza kuuza dawa za kulevya, akakamatwa na kufungwa gerezani. Kijana Mkristo aitwaye John alianza kutumia dawa za kulevya na kuiba magari. Kwa kusikitisha, vijana wengi huvuna matokeo ya tabia hiyo—mimba haramu, magonjwa yanayoambukizwa kingono, au uraibu wa pombe au dawa za kulevya.—Wagalatia 6:7, 8.

Madhara Yake

Madhara ya kihisia huwa makubwa kuliko ya kimwili. Dhamiri yenye kuhangaika yaweza kuumiza sana. (Zaburi 38:3, 4) Joseph asema hivi: “Kuna mithali moja inayosema kwamba hujui thamani ya kitu ulicho nacho hadi utakapokipoteza. Nyakati nyingine nikikumbuka mambo niliyofanya, mimi hushangaa jinsi nilivyokuwa mpumbavu.”

Jambo jingine muhimu ni uwezekano wa kuharibu sifa yako. Andiko la Mhubiri 10:1, Biblia Habari Njema, lasema hivi: “Nzi waliokufa husababisha marashi kunuka; upumbavu kidogo hubatilisha hekima na heshima.” Nyakati za kale marashi au manukato yangeweza kuharibiwa na kitu kidogo sana kama nzi mfu. Vivyo hivyo, sifa nzuri ambayo umejitahidi kusitawisha yaweza kuharibiwa na “upumbavu kidogo” tu. Na iwapo wewe ni Mkristo tendo hilo pasina shaka litakuzuia kupata mapendeleo kutanikoni. Utawatiaje moyo wengine wafuate kanuni za Biblia na huku wanajua kwamba wewe mwenyewe ulizipuuza?—Waroma 2:1-3.

Mwishowe, fikiria mfadhaiko wa wazazi wako wanapogundua kwamba humo nyumbani. Mzazi mmoja alieleza jinsi alivyoshtuka alipogundua kwamba binti yake wa miaka 15 hakuwa nyumbani. Alisema kwamba yeye na mume wake ‘walikuwa na wasiwasi sana’ kwa sababu hawakufahamu alikoenda binti yao. Je, wewe wataka wazazi wako wawe na wasiwasi na kihoro jinsi hiyo?—Mithali 10:1.

Kupata Uhuru Zaidi

Kwa wazi, inaweza kutamausha endapo wazazi wako wanaonekana kuwa wakali kupita kiasi. Lakini je, kutoka kisiri nyumbani ndilo suluhisho? Pasina shaka hatimaye utagunduliwa. Hata uwe mwerevu kiasi cha kuwahadaa wazazi wako, Yehova Mungu anaona matendo yako, hata yale unayotenda gizani. (Ayubu 34:21) Punde si punde, matendo yako yatafunuliwa na wazazi wako hawatakuamini tena. Matokeo yatakuwaje? Utapoteza kile ulichotamani—uhuru!

Kumbuka: Ili kufurahia uhuru, wazazi wako wanahitaji kukuamini. Na ili wapate kukuamini lazima watii. (Waefeso 6:1-3) Ikiwa wahisi kuwa wazazi wako kwa njia fulani wanakosa kukubali sababu, zungumza nao kinagaubaga na kwa heshima. Huenda watasikiliza hoja yako. Kwa upande mwingine, huenda ukaona kwamba wana sababu nzuri za kukuwekea vizuizi fulani. Hata ikiwa hukubaliani nao, usisahau kamwe kwamba wanakupenda na wanapendezwa kikweli na hali yako njema. Endelea kuimarisha utumainifu walio nao kukuelekea na baada ya muda utapata uhuru unaotamani. *

‘Usiende Nao’

Katika nyakati za kale, vijana wenye kumhofu Mungu walishawishwa kujiunga na rafiki zako kufanya makosa. Kwa hiyo Solomoni aliwahimiza vijana hivi: “Mwanangu, wenye dhambi wakikushawishi, wewe usikubali. . . . Usiende njiani pamoja nao.” (Mithali 1:10, 15) Tii shauri hilo wale wanaojiita eti rafiki zako wanapokwambia mtoke kisiri nyumbani. Solomoni aendelea kuonya hivi: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”—Mithali 22:3.

Ikiwa tayari umeanza kutoka kisiri nyumbani, koma! Hatimaye utajiletea majuto tu. Waeleze wazazi wako juu ya tabia hiyo, halafu kubali nidhamu au vizuizi vyovyote ambavyo huenda wakakuwekea. Iwapo lazima, tafuta rafiki wengine—rafiki wenye uvutano ufaao. (Mithali 13:20) Tafuta namna nyingine ifaayo na isiyo hatari ya kujifurahisha.

Jambo la maana zaidi, jenga hali yako ya kiroho kwa kusoma Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. “Jinsi gani kijana aisafishe njia yake?” akauliza mtunga-zaburi. Ajibu hivi: “Kwa kutii, akilifuata neno lako [la Mungu].” (Zaburi 119:9) Na uamuzi wako wa kufanya yaliyo mema unapozidi kukita mizizi, utaona kwamba ingawa kutoka kisiri nyumbani huenda kukavutia na kusisimua, kuna hatari nyingi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 19 Ili kupata habari zaidi juu ya uwezavyo kupata uhuru zaidi, ona sura ya 3 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

“Wazazi wangu hawataki niende mahali wenzangu wanaenda. . . . Hata hivyo, mimi huenda tu kisha nawadanganya”

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kutoka kisiri nyumbani huongoza kwenye makosa mazito