Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msaada kwa Wahasiriwa wa Mateso

Msaada kwa Wahasiriwa wa Mateso

Msaada kwa Wahasiriwa wa Mateso

NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA DENMARK

“NI RAHISI KUPONYA MIFUPA ILIYOVUNJIKA KULIKO KUPONYA NAFSI ILIYOVUNJIKA.”—Dakt. Inge Genefke.

MWANAMUME kijana atembea polepole kwenye barabara moja tulivu kwenye mji wa Kizungu kisha atua kuangalia bidhaa zilizoonyeshwa kwenye dirisha la duka moja. Kwa ghafula, mikono yake yaanza kutetemeka. Magoti yake yatikisika. Anashika shingo lake kana kwamba anasakamwa na kitu kooni. Kwenye dirisha ameona tu mfano wa polisi wawili waliovalia yunifomu. Mwanamume huyo kijana hajavunja sheria zozote, na hakuna sababu ya kumfanya aogope. Lakini kuwaona tu wanaume waliovalia yunifomu kunamkumbusha jinsi alivyoteswa miaka mingi iliyopita katika sehemu iliyo na umbali wa maelfu ya kilometa.

Huenda kisa hicho kimempata yeyote kati ya mamilioni ya wanaume, wanawake na hata watoto. Huenda kimempata mtu umjuaye. Mtu aliyetendwa kikatili aweza kuwa mkimbizi au mhamiaji ambaye amehamia katika ujirani wako. Huenda watoto wake wanaenda shule pamoja na watoto wako. Waweza kuwa wamjua kuwa jirani mpole, mtulivu, ambaye kwa kawaida hujali mambo yake mwenyewe. Lakini sura ya nje yaweza kudanganya; yaweza kuficha msononeko wa ndani sana ambao mhasiriwa huhisi anapojaribu kukabiliana na kumbukumbu za kuteseka kimwili na kihisia-moyo za wakati uliopita. Mwono—au sauti—yoyote humfanya akumbuke mateso ya wakati uliopita. Mhasiriwa mmoja wa namna hiyo alisema: “Kila wakati nisikiapo mtoto akilia, mimi hufikiria kuhusu watu niliosikia wakilia gerezani. Kila wakati ninaposikia mvumo hewani, ninakumbuka mvumo wa ufito ukienda juu na chini kabla tu haujanipiga.”

Mateso hayatumiwi na wanasiasa wenye siasa kali na makundi ya magaidi tu. Katika nchi kadhaa, yanatumiwa pia na vikosi vya kijeshi na hata vikosi vya polisi. Kwa nini? Mateso yanaweza kuwa njia rahisi na madhubuti ya kupata habari, kutoa ungamo, kupata ushuhuda wa kwamba mtu amehusika katika jeuri, au kulipiza kisasi. Kulingana na Dakt. Inge Genefke, wa Denmark, mtaalamu wa mateso, serikali nyingine “zimekuja mamlakani na kushikilia cheo chake kupitia zoea la kutesa.” Mhasiriwa mmoja alisema hivi: “Walitaka kuniangamiza kihisia ili wengine waone jambo linalokupata unapoishutumu serikali.”

Kwa watu wengi kuwatesa wanadamu wenzao kwawakumbusha Enzi za Giza. Kwa vyovyote, katika mwaka wa 1948 Umoja wa Mataifa ulikubali lile Azimio kwa Wote la Haki za Kibinadamu ambalo linasema: “Hakuna mtu atakayeteswa au kutendewa kwa ukatili, kushushiwa hadhi au kutendewa au kuadhibiwa kinyama.” (Kifungu cha 5) Hata hivyo, wataalamu fulani wanaamini kwamba, kufikia asilimia 35 ya wakimbizi ulimwenguni wameteswa. Kwa nini kuteswa kumeenea sana? Wahasiriwa huathiriwaje, na ni nini kiwezacho kufanywa ili kuwasaidia?

Matokeo ya Baadaye

Haishangazi kwamba wahasiriwa wengi wa mateso hukimbia kutoka nchi yao ili kuanza maisha mapya kwingineko. Ingawa mazingira hubadilika, mateso—ya kimwili na kisaikolojia—huendelea. Kwa kielelezo, mhasiriwa aweza kuwa na hisia za hatia kwa sababu ya kushindwa kuwalinda marafiki na watu wa jamaa kutokana na kutendwa kinyama. Anaweza pia kusitawisha hali ya kutowaamini wengine akihofu kuwa kila mtu akutanaye naye huenda akawa ndiye mtoa-habari. “Mhasiriwa wa mateso siku zote atakuwa mtu asiyefahamika,” asema mwandikaji Carsten Jensen. “Amepoteza itibari yake kwa watu milele.”

Tokeo ni mchanganyiko wa vurugu la kimwili na kiakili ambalo laweza kumkanganya mhasiriwa na yeyote atakaye kumsaidia. Nyakati nyingine matatizo ya kimwili yaweza kutibiwa bila shida, lakini matatizo ya kisaikolojia ni magumu. “Mwanzoni tulifikiri hivi, ‘Sawa tu tutaponya magonjwa yao ya kimwili—kisha wataweza kuendelea na shughuli zao za kawaida,’” akiri Dakt. Genefke. “Lakini upesi tukatambua kuwa ni uchungu uliokuwa mioyoni mwao ndio uliokuwa unawatesa.” Hata hivyo, Dakt. Genefke asema: “Imeshangaza kuona kwamba inawezekana kutuliza na kuwasaidia wahasiriwa hata baada ya miaka mingi.”

Katika mwaka wa 1982, kwenye Hospitali ya Kitaifa ya Copenhagen, Dakt. Genefke pamoja na matabibu wengine kutoka Denmark, walianzisha kituo kidogo cha kuwatibu wakimbizi ambao walikuwa wahasiriwa wa mateso. Kutokana na chanzo hiki kidogo mpango wa tufeni pote uitwao International Rehabilitation Council for Torture Victims (IRCT) ukaanzishwa. Baraza hilo linaelekeza kazi ya kutoa kitulizo kupitia vituo zaidi ya 100 ulimwenguni pote likiwa katika makao makuu huko Copenhagen. Katika miaka ambayo imepita, baraza hilo limejifunza mengi kuhusu kuwatibu wahasiriwa wa mateso.

Jinsi ya Kutoa Msaada

Mara nyingi husaidia wahasiriwa wanapozungumzia mambo yaliyowapata. “Miaka 20 iliyopita,” yasema karatasi moja ya habari kutoka IRCT, “wahasiriwa wa mateso mara nyingi walikuwa wahasiriwa kwa njia mbili. Kwanza kwa kuwa katika hali ya kuteswa kimwili/kisaikolojia, na pili kwa kutoweza kuzungumzia hali hiyo.”

Kwa kweli haipendezi kuzungumzia habari yenye kuhuzunisha kama kuteswa. Lakini ikiwa anayeteseka ataka kumwambia siri rafiki fulani naye akataa kusikiliza, anayeteseka aweza kukata tumaini hata zaidi. Kwa hiyo, ni muhimu kwa mhasiriwa kuhakikishiwa kwamba kuna mtu anayemjali. Bila shaka hakuna mtu anayepaswa kuingilia mambo ya kibinafsi ya mwingine. Hatimaye, ni juu ya mhasiriwa kuamua ikiwa anataka kuambia yeyote mambo yake ya siri, ni wakati gani atafanya hivyo na ni nani atakayeambia.—Mithali 17:17; 1 Wathesalonike 5:14.

Wataalamu wengi hupendekeza kufikiria upande wa kimwili na wa kiakili wa mateso. Kwa wahasiriwa fulani, kuanza kuishi maisha ya kawaida kunahitaji msaada wa kitaaluma. Matibabu yanaweza kutia ndani mazoezi ya kupumua na ya mawasiliano. * Kwa kawaida hisia za aibu zapaswa kushughulikiwa kwanza. Mwanatiba mmoja alimwambia hivi mwanamke fulani ambaye alikuwa amebakwa na kupigwa mara nyingi: “Aibu uhisiyo ni ya kawaida na yaeleweka. Lakini kumbuka kwamba si yako. Aibu hiyo ni ya wale waliokufanyia hivyo.”

Waokokaji wa Kambi za Mateso

Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili mamilioni ya watu waliteswa kwa kushushiwa hadhi katika kambi za mateso za Hitler. Miongoni mwao kulikuwa maelfu ya Mashahidi wa Yehova ambao walinyanyaswa kwa sababu walikataa kukana itikadi za kidini. Kwa kweli imani yao iliwasaidia kuvumilia hali hizo zenye kujaribu. Jinsi gani?

Muda mrefu kabla hawajawekwa kwenye kambi za mateso, Wakristo hawa walikuwa wamejifunza Neno la Mungu kwa uangalifu. Hivyo, hawakukorowezwa majaribu yalipozuka, wala hawakumlaumu Mungu mateso yao yalipoendelea. Kupitia funzo la Biblia, Mashahidi hao walikuwa wamejifunza ni kwa nini Mungu anaruhusu uovu na jinsi atakavyoukomesha katika wakati wake. Funzo la Biblia liliwafunza kwamba Yehova “hupenda haki” na kwamba yeye hukasirika wanadamu wanapowatendea wenzao vibaya.—Zaburi 37:28; Zekaria 2:8, 9.

Bila shaka, wengi wa waokokaji hawa wa kambi za mateso wamelazimika kukabiliana na kiwewe baada ya mateso yaliyowapata. Katika kufanya hivyo wametiwa nguvu sana kwa kufuata shauri la mtume Paulo. Wakati Paulo alipokuwa akiteseka katika gereza la Waroma, hali ambayo lazima ilimletea hangaiko kubwa, aliwaandikia hivi waamini wenzake: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 1:13; 4:6, 7.

Kupitia funzo la Biblia, washika-uaminifu-maadili hawa wamejifunza kwamba Mungu ameahidi kufanya dunia iwe paradiso, matokeo machungu yenye kushusha hadhi kama vile mateso yataondolewa hatimaye.

Mashahidi wa Yehova wanashiriki tumaini hili linalotegemea Biblia pamoja na jirani zao katika nchi zaidi ya 230. Hali zilizovurugika za ulimwengu huwafanya wakutane na watu wengi ambao wameteseka kwa sababu ya unyama wa mwanadamu. Wanapokutana na wahasiriwa wa mateso, Mashahidi hujitahidi sana kushiriki na watu hao ahadi ya Biblia ya wakati ujao mwangavu. Wana furaha iliyoje kueneza habari njema kuhusu wakati ujao ambapo kuteswa kutakuwa jambo la kale!—Isaya 65:17; Ufunuo 21:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Amkeni! halipendekezi tiba yoyote hususa. Wakristo wapaswa kuwa na uhakika kwamba tiba yoyote wanayofuatia haipingani na kanuni za Biblia.

[Blabu katika ukurasa wa 24]

“HAKUNA MTU ATAKAYETESWA AU KUTENDEWA KWA UKATILI, KUSHUSHIWA HADHI AU KUTENDEWA AU KUADHIBIWA KINYAMA.”—Kifungu cha 5, Azimio kwa Wote la Haki za Kibinadamu

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

JINSI UNAVYOWEZA KUSAIDIA

IKIWA UNAMFAHAMU MTU AMBAYE ANAPATA NAFUU KUTOKANA NA ATHARI ZA MATESO, MADOKEZO YAFUATAYO YAWEZA KUWA YENYE MSAADA:

● Onyesha hisia-mwenzi. Waweza kusema hivi: “Najua kuna taabu nyingi sana katika nchi ulikotoka. Unakabilianaje na hali?”—Mathayo 7:12; Waroma 15:1.

● Usiingilie mambo yake ya kibinafsi au usisisitize sana kutoa msaada. Badala ya hivyo, uwe mwenye fadhili na mwenye ufikirio. Acha mhasiriwa ajue kwamba uko tayari kusikiliza.—Yakobo 1:19.

● Epuka kutoa msaada kupita kiasi. Usimnyime anayeumia hali ya kujistahi au faragha. Wazo ni kusaidiana mzigo pamoja na anayeumia si kujaribu kuubeba wote.