Waamuzi 15:1-20

  • Samsoni alipiza kisasi dhidi ya Wafilisti (1-20)

15  Baada ya muda, wakati wa mavuno ya ngano, Samsoni alimchukua mwanambuzi na kwenda kumtembelea mke wake. Akasema: “Ningependa kuingia nikamwone mke wangu katika chumba cha kulala.”* Lakini baba ya mwanamke huyo hakumruhusu kuingia.  Baba ya mwanamke huyo akasema, “Nilidhani, ‘Hakika unamchukia.’+ Kwa hiyo nikampa kijana mwenzako.+ Dada yake mdogo ni mrembo kuliko yeye. Tafadhali, mchukue huyo badala yake.”  Hata hivyo, Samsoni akawaambia, “Wakati huu Wafilisti hawatanilaumu nikiwadhuru.”  Basi Samsoni akaenda na kuwakamata mbweha 300. Kisha akachukua mienge, akawafunga mikia wawili-wawili na kuweka mwenge mmoja kati ya kila mikia miwili.  Halafu akaiwasha moto ile mienge na kuwaachilia mbweha hao waingie katika mashamba ya nafaka ya Wafilisti. Basi akateketeza kila kitu kuanzia masuke mpaka nafaka iliyo shambani, na pia mashamba ya mizabibu na ya mizeituni.  Wafilisti wakauliza: “Ni nani aliyefanya hivi?” Wakaambiwa: “Ni Samsoni, mkwe wa yule Mtimna, kwa sababu alimchukua mke wa Samsoni na kumpa kijana mwenzake.”+ Kwa hiyo Wafilisti wakaenda na kumteketeza mwanamke huyo na baba yake.+  Kisha Samsoni akawaambia, “Kama haya ndiyo mambo mnayofanya, sitawaacha mpaka nitakapolipiza kisasi.”+  Basi akawapiga na kuwaua watu wengi, mmoja baada ya mwingine, kisha akashuka na kwenda kukaa pangoni katika mwamba wa Etamu.  Baadaye Wafilisti wakapanda na kupiga kambi kule Yuda, nao walikuwa wakizunguka-zunguka katika mji wa Lehi.+ 10  Ndipo watu wa Yuda wakawauliza, “Kwa nini mmekuja kutushambulia?” Wakajibu: “Tumekuja kumkamata* Samsoni, na kumtendea kama alivyotutendea.” 11  Basi wanaume 3,000 wa Yuda wakashuka kwenye pango lililo katika mwamba wa Etamu, wakamuuliza Samsoni, “Je, hujui kwamba Wafilisti wanatutawala?+ Kwa nini umetutendea hivi?” Akawajibu: “Nimewatendea kama walivyonitendea.” 12  Lakini wakamwambia, “Tumekuja kukukamata* ili tukutie mikononi mwa Wafilisti.” Samsoni akawaambia, “Niapieni kwamba ninyi hamtanidhuru.” 13  Wakamwambia, “Usiogope, tutakufunga tu na kukupeleka kwao, lakini hatutakuua.” Basi wakamfunga kwa kamba mbili mpya na kumtoa mwambani. 14  Alipofika Lehi, Wafilisti walishangilia sana kumwona. Kisha roho ya Yehova ikamtia nguvu,+ na kamba alizofungwa mikononi zikawa kama nyuzi za kitani zilizochomwa moto, nazo zikalegea* na kuanguka kutoka mikononi mwake.+ 15  Akaona utaya mbichi wa punda dume; akauchukua na kuutumia kuua wanaume 1,000.+ 16  Kisha Samsoni akasema: “Kwa utaya wa punda—rundo moja, marundo mawili! Kwa utaya wa punda nimeua wanaume 1,000.”+ 17  Baada ya kusema hayo, aliutupa utaya huo na kupaita mahali hapo Ramath-lehi.*+ 18  Kisha akahisi kiu sana, akamlilia Yehova akisema, “Ni wewe uliyemtumia mtumishi wako kuleta ukombozi huu mkubwa. Je, sasa nife kwa kiu na kuchukuliwa na watu wasiotahiriwa?” 19  Basi Mungu akapasua mahali penye shimo huko Lehi, na maji yakatiririka kutoka humo.+ Alipoyanywa, roho yake ikamrudia* akapata nguvu tena. Ndiyo sababu aliiita sehemu hiyo En-hakore,* nayo iko Lehi mpaka leo. 20  Samsoni alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka 20 katika siku za Wafilisti.+

Maelezo ya Chini

Au “chumba cha ndani.”
Au “kumfunga.”
Au “kukufunga.”
Tnn., “zikayeyuka.”
Maana yake “Kilima cha Utaya.”
Au “nguvu zake zikamrudia.”
Maana yake “Chemchemi ya Anayeita.”