Ezekieli 25:1-17
25 Neno la Yehova likanijia tena likisema:
2 “Mwana wa binadamu, uelekeze uso wako kwa Waamoni,+ na utabiri dhidi yao.+
3 Unapaswa kusema hivi kuhusu Waamoni, ‘Sikieni neno la Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Kwa sababu ulisema ‘Aha!’ dhidi ya mahali pangu patakatifu wakati palipotiwa unajisi, na dhidi ya nchi ya Israeli ilipofanywa ukiwa, na dhidi ya watu wa nyumba ya Yuda, walipopelekwa uhamishoni,
4 kwa hiyo, ninakutia mikononi mwa Watu wa Mashariki uwe mali yao. Watapiga kambi zao* ndani yako na kusimamisha mahema yao kati yako. Watakula matunda yako, na kunywa maziwa yako.
5 Nitalifanya jiji la Raba+ liwe malisho ya ngamia, na nchi ya Waamoni iwe mahali pa kupumzika kwa ajili ya mifugo; nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.”’”
6 “Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kwa sababu ulipiga makofi+ na kupiga miguu yako chini nawe ukashangilia kwa dharau kubwa dhidi ya nchi ya Israeli,+
7 kwa hiyo nitaunyoosha mkono wangu dhidi yako ili nikutie mikononi mwa mataifa uwe kitu cha kuporwa. Nitakukatilia mbali kutoka kati ya mataifa na kukuharibu kutoka katika nchi hizi.+ Nitakuangamiza, nawe utalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’
8 “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kwa sababu watu wa Moabu+ na Seiri+ wamesema, “Tazama! Nyumba ya Yuda ni kama mataifa mengine yote,”
9 ninauacha wazi mpaka* wa Moabu kwenye majiji yake ya mpakani, uzuri wa* nchi yake, Beth-yeshimothi, Baal-meoni, hadi Kiriathaimu.+
10 Nitaitoa pamoja na Waamoni kuwa mali ya watu wa Mashariki,+ ili Waamoni wasikumbukwe kati ya mataifa.+
11 Nami nitatekeleza hukumu katika Moabu,+ nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’
12 “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Nchi ya Edomu imelipiza kisasi dhidi ya nyumba ya Yuda nayo imepata hatia kubwa kwa kulipiza kisasi dhidi yake;+
13 kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Pia nitaunyoosha mkono wangu dhidi ya Edomu na kuwaangamiza wanadamu na wanyama waliomo, nami nitaifanya kuwa ukiwa.+ Kuanzia Temani mpaka Dedani, watauawa kwa upanga.+
14 ‘Nitalipiza kisasi dhidi ya Edomu kwa mkono wa watu wangu Waisraeli.+ Watawaletea watu wa Edomu hasira yangu na ghadhabu yangu, ili wapatwe na kisasi changu mwenyewe,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”’
15 “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kwa sababu ya chuki yao isiyo na mwisho, Wafilisti wamejaribu kwa nia ovu* kulipiza kisasi na kuleta maangamizi.+
16 Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ninaunyoosha mkono wangu dhidi ya Wafilisti,+ nami nitawakatilia mbali Wakerethi+ na kuwaangamiza wakaaji wanaobaki wa pwani ya bahari.+
17 Nitatekeleza matendo makubwa ya kisasi dhidi yao kwa adhabu kali, nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova nitakapoleta kisasi changu dhidi yao.”’”
Maelezo ya Chini
^ Au “kambi zao zenye ukuta.”
^ Au “mteremko.”
^ Au “pambo la.”
^ Au “kwa dharau iliyo katika nafsi yao.”