Yoshua 8:1-35

8  Kisha Yehova akamwambia Yoshua: “Usiogope wala usiwe na hofu.+ Wachukue pamoja nawe watu wote wa vita kisha usimame, mwende Ai. Tazama, nimemtia mkononi mwako mfalme wa Ai na watu wake na jiji lake na nchi yake.+  Nawe unapaswa kulitendea Ai na mfalme wake kama vile ulivyolitendea Yeriko na mfalme wake.+ Lakini mnaweza kupora nyara zake na wanyama wake wa kufugwa kwa ajili yenu wenyewe.+ Weka kikundi cha kulivizia jiji upande wake wa nyuma.”+  Basi Yoshua na watu wote wa vita+ wakasimama waende Ai, kisha Yoshua akachagua wanaume wenye nguvu+ 30,000, akawatuma wakati wa usiku.  Naye akawaamuru, akisema: “Angalieni, mtajificha na kulivizia+ jiji, upande wa nyuma wa jiji. Msiende mbali sana na jiji, nanyi nyote kaeni tayari.  Lakini mimi na watu wote walio pamoja nami, tutaenda karibu na jiji. Na itatukia kwamba, wakitoka nje kukutana nasi kama walivyofanya pale mwanzoni,+ ndipo sisi tutakapokimbia mbele yao.  Nao watatoka nje watufuate mpaka tutakapokuwa tumewavuta mbali na jiji hilo, kwa maana watasema, ‘Wanakimbia mbele yetu kama walivyofanya pale mwanzoni.’+ Nasi tutakimbia mbele yao.  Kisha ninyi mtasimama kutoka hapo mlipovizia, nanyi mtalikamata jiji; na Yehova Mungu wenu hakika atalitia jiji hilo mikononi mwenu.+  Na itatukia kwamba mara tu mtakapokuwa mmelikamata jiji, mtaliteketeza jiji kwa moto.+ Mnapaswa kufanya kulingana na neno la Yehova. Angalieni, nimewaamuru ninyi.”+  Kisha Yoshua akawatuma, nao wakaenda mahali pa kuvizia, wakapiga kambi kati ya Betheli na Ai upande wa magharibi wa Ai, naye Yoshua akaendelea kukaa usiku huo katikati ya watu. 10  Ndipo Yoshua akaamka asubuhi na mapema,+ akawakagua watu, kisha akapanda kwenda Ai mbele ya watu, yeye pamoja na wanaume wazee wa Israeli. 11  Na watu wote wa vita+ waliokuwa pamoja naye wakaenda, wapate kukaribia na kuwa mbele ya jiji, nao wakaanza kupiga kambi upande wa kaskazini wa Ai, pakiwa na bonde kati yao na Ai. 12  Wakati huohuo akachukua wanaume elfu tano hivi, akawaweka kuvizia+ kati ya Betheli+ na Ai, upande wa magharibi wa jiji. 13  Basi watu wakaweka kambi kuu iliyokuwa upande wa kaskazini wa jiji+ na wale wa nyuma kabisa waliokuwa upande wa magharibi wa jiji,+ kisha Yoshua akaanza kwenda usiku huo katikati ya ile nchi tambarare ya chini. 14  Na ikawa kwamba, mara tu mfalme wa Ai alipoona hilo, wanaume wa jiji lile wakafanya haraka, wakaamka mapema, wakatoka nje wakutane kupigana na Israeli, yeye na watu wake wote, kwa wakati uliowekwa, mbele ya ile nchi tambarare ya jangwa. Lakini yeye hakujua kwamba palikuwa na waliomvizia upande wa nyuma wa jiji.+ 15  Wakati Yoshua na Israeli wote walipopigwa mbele yao,+ wakaanza kukimbia kupitia njia ya nyika.+ 16  Ndipo watu wote waliokuwa ndani ya jiji wakaitwa wawafuatilie, nao wakamfuatilia Yoshua na kuvutwa mbali na jiji.+ 17  Hakubaki mtu yeyote ndani ya Ai na Betheli ambaye hakufuatilia Israeli, hivyo wakaliacha jiji wazi kabisa, wakawafuatilia Israeli. 18  Sasa Yehova akamwambia Yoshua: “Nyoosha mkuki ulio mkononi mwako kuelekea Ai,+ kwa maana nitalitia mkononi mwako.”+ Basi Yoshua akaunyoosha mkuki uliokuwa mkononi mwake kuelekea jiji lile. 19  Na waliovizia wakasimama haraka kutoka mahali pao, nao wakaanza kukimbia mara tu aliponyoosha mkono wake, wakaingia ndani ya jiji na kulikamata.+ Kisha wakafanya haraka na kuliwasha moto jiji hilo.+ 20  Ndipo watu wa Ai wakaanza kugeuka nyuma wakaona, na tazama, moshi wa jiji hilo ulikuwa unapaa juu mbinguni, na ndani yao haukubaki uwezo wowote wa kukimbia huku au huku. Kisha wale watu waliokuwa wakikimbilia nyikani wakawageukia wale waliokuwa wakiwafuatilia. 21  Na Yoshua na Israeli wote wakaona kwamba waliovizia+ walikuwa wamelikamata jiji hilo, na kwamba moshi wa jiji ulikuwa unapaa juu, kwa hiyo wakageuka, wakaanza kuwapiga na kuwaua watu wa Ai. 22  Na hao wengine wakatoka katika jiji kuja kukutana nao, hata wale wakawa katikati ya Israeli, hawa upande huu na hawa upande ule, nao wakawaua hata asibaki yeyote kati yao, mwenye kuokoka wala mwenye kupona.+ 23  Naye mfalme+ wa Ai wakamkamata akiwa hai, wakamleta karibu na Yoshua. 24  Na ikawa kwamba Israeli walipokuwa wakimaliza kuwaua wakaaji wote wa Ai uwanjani, katika nyika ambamo walikuwa wamewafuatilia, wote waliendelea kuanguka, kwa makali ya upanga mpaka walipokwisha. Kisha Israeli wote wakarudi Ai na kulipiga kwa makali ya upanga. 25  Na wote walioanguka siku hiyo, kuanzia mwanamume mpaka mwanamke, jumla yao ilikuwa kumi na mbili elfu, watu wote wa Ai. 26  Yoshua naye hakuurudisha nyuma mkono wake ambao alitumia kunyoosha ule mkuki+ mpaka alipokuwa amewaangamiza+ wakaaji wote wa Ai. 27  Ni wanyama wa kufugwa peke yao na nyara za jiji ndizo ambazo Israeli waliteka kwa ajili yao wenyewe, kulingana na neno la Yehova ambalo alikuwa amemwamuru Yoshua.+ 28  Kisha Yoshua akateketeza Ai na kulifanya kuwa kilima kinachodumu mpaka wakati usio na kipimo,+ na kuwa ukiwa mpaka leo hii. 29  Naye akamtundika mfalme wa Ai+ juu ya mti mpaka jioni;+ na jua lilipokaribia kutua, Yoshua akatoa amri nao wakachukua maiti yake+ kutoka mtini na kuitupa kwenye mwingilio wa lango la jiji nao wakaweka rundo kubwa la mawe juu yake, mpaka leo hii. 30  Ndipo Yoshua akaanza kujenga madhabahu+ kwa Yehova Mungu wa Israeli, katika Mlima Ebali,+ 31  kama vile Musa mtumishi wa Yehova alivyokuwa amewaamuru wana wa Israeli, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha sheria+ ya Musa: “Madhabahu ya mawe mazima, ambayo chombo cha chuma hakikutumiwa juu yake”;+ nao wakatoa juu yake matoleo ya kuteketezwa kwa Yehova na kutoa dhabihu za ushirika.+ 32  Kisha akaandika hapo juu ya mawe nakala+ ya maandishi ya sheria ya Musa ambayo alikuwa ameandika mbele ya wana wa Israeli.+ 33  Na Israeli wote na wanaume wao wazee+ na maofisa na waamuzi wao walikuwa wamesimama upande huu wa Sanduku na upande ule mwingine mbele ya makuhani+ Walawi, waliochukua sanduku la agano la Yehova,+ mkaaji mgeni na mwenyeji+ vilevile, nusu yao walisimama mbele ya Mlima Gerizimu+ na nusu ile nyingine mbele ya Mlima Ebali,+ (kama vile Musa mtumishi wa Yehova alivyokuwa ameamuru,)+ ili kuwabariki+ watu wa Israeli kwanza. 34  Kisha akasoma kwa sauti maneno yote ya sheria,+ baraka+ na laana,+ kulingana na yote ambayo yameandikwa katika kitabu cha sheria. 35  Hakuna neno lolote kati ya yote ambayo Musa alikuwa ameamuru ambalo Yoshua hakusoma kwa sauti mbele ya kutaniko lote la Israeli,+ pamoja na wanawake+ na watoto wadogo+ na wakaaji wageni+ waliokuwa katikati yao.

Maelezo ya Chini