Yeremia 34:1-22

34  Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova, wakati Nebukadreza mfalme wa Babiloni+ na jeshi lake lote+ na falme zote za dunia, mamlaka iliyo chini ya mkono wake,+ na vikundi vyote vya watu vilipokuwa vikipiga vita juu ya Yerusalemu na juu ya majiji yake yote,+ kusema:  “Yehova Mungu wa Israeli amesema hivi, ‘Nenda, umwambie Sedekia mfalme wa Yuda,+ ndiyo, umwambie hivi: “Yehova amesema hivi, ‘Tazama, ninalitia jiji hili mkononi mwa mfalme wa Babiloni,+ naye ataliteketeza kwa moto.+  Nawe mwenyewe hutaponyoka kutoka mkononi mwake, kwa sababu bila shaka utakamatwa na kutiwa mkononi mwake.+ Na macho yako yatayaona macho ya mfalme wa Babiloni,+ na kinywa chake kitasema na kinywa chako, nawe utaenda Babiloni.’  Hata hivyo, lisikie neno la Yehova, Ee Sedekia mfalme wa Yuda,+ ‘Yehova amesema hivi kukuhusu wewe: “Hutakufa kwa upanga.  Utakufa kwa amani;+ nao watakufanyia mfukizo,+ kama ule mfukizo ambao waliwafanyia baba zako, wale wafalme wa zamani waliokutangulia,+ na ‘Aa, Ee bwana!’+ ndivyo watakavyosema wakikuombolezea,+ kwa maana ‘mimi mwenyewe nimesema neno hili,’ asema Yehova.”’”’”  Na Yeremia nabii akamwambia Sedekia mfalme wa Yuda maneno hayo yote+ katika Yerusalemu,  wakati majeshi ya mfalme wa Babiloni yalipokuwa yakipiga vita juu ya Yerusalemu na juu ya majiji yote ya Yuda ambayo yalikuwa yamebaki,+ juu ya Lakishi+ na juu ya Azeka;+ kwa maana hayo, majiji yenye ngome,+ ndiyo yaliyobaki kati ya majiji ya Yuda.+  Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova baada ya Mfalme Sedekia kufanya agano pamoja na watu wote waliokuwa Yerusalemu ili kuwatangazia uhuru,+  kila mtu kumwachilia huru mtumishi wake wa kiume na kila mtu mjakazi wake, mwanamume Mwebrania+ na mwanamke Mwebrania, ili wasiwatumie kama watumishi, yaani, Myahudi, ambaye ni ndugu yake.+ 10  Basi wakuu+ wote wakatii, na watu wote waliokuwa wameingia katika agano la kwamba kila mtu amwachilie huru mtumishi wake wa kiume na kila mtu mjakazi wake, ili wasiwatumie tena kama watumishi, nao wakatii na kuwaachilia waende zao.+ 11  Lakini wakageuka+ baada ya hayo na kuanza kuwarudisha wale watumishi wa kiume na wajakazi ambao walikuwa wamewaachilia huru, nao wakawatiisha kama watumishi wa kiume na kama wajakazi.+ 12  Kwa hiyo neno la Yehova likamjia Yeremia kutoka kwa Yehova, na kusema: 13  “Yehova Mungu wa Israeli amesema hivi, ‘Mimi mwenyewe nilifanya agano pamoja na mababu+ zenu katika siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri,+ kutoka katika nyumba ya watumishi,+ nikisema: 14  “Mwishoni mwa miaka saba mnapaswa kumwachilia kila mtu ndugu yake,+ Mwebrania,+ ambaye uliuziwa+ na ambaye amekutumikia miaka sita; nawe lazima umwachilie aende huru asiwe pamoja nawe.” Lakini mababu zenu hawakunisikiliza, wala hawakutega sikio lao.+ 15  Nanyi leo mnageuka na kufanya yaliyo sawa machoni pangu kwa kumtangazia uhuru kila mtu mwenzake, nanyi mnafanya agano mbele zangu+ ndani ya nyumba ambayo jina langu limeitwa juu yake.+ 16  Kisha mnageuka+ nyuma na kulitia unajisi jina langu+ na kumrudisha kila mtu mtumishi wake wa kiume na kila mtu mjakazi wake, ambaye mlimwachilia huru kwa kukubaliana na nafsi yao, nanyi mnawatiisha wawe watumishi wenu wa kiume na wajakazi wenu.’+ 17  “Kwa hiyo Yehova amesema hivi, ‘Ninyi hamkunitii mimi kwa kuendelea kumtangazia uhuru+ kila mtu ndugu yake na kila mtu mwenzake. Tazama, mimi ninawatangazia ninyi uhuru,’+ asema Yehova, ‘upanga,+ tauni+ na njaa,+ na hakika mimi nitawatoa ninyi kwa ajili ya kutetemesha falme zote za dunia.+ 18  Nami nitawatoa wale watu wanaolivunja agano langu,+ kwa sababu hawakutenda yale maneno ya agano ambalo walifanya mbele zangu kwa yule ndama ambaye walimkata vipande viwili+ ili wapite katikati ya vipande vyake;+ 19  yaani, wakuu wa Yuda na wakuu wa Yerusalemu,+ maofisa wa makao ya mfalme na makuhani na watu wote wa nchi waliopita katikati ya vile vipande vya ndama​—​ 20  ndiyo, nitawatia mkononi mwa adui zao na mkononi mwa wale wanaoitafuta nafsi yao;+ na maiti zao zitakuwa chakula kwa viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kwa wanyama wa dunia.+ 21  Na Sedekia mfalme wa Yuda+ na wakuu wake nitawatia mkononi mwa adui zao na mkononi mwa wale wanaoitafuta nafsi yao na mkononi mwa majeshi ya mfalme wa Babiloni+ ambayo yanaondoka kuwaacha ninyi.’+ 22  “‘Tazama, mimi ninaamuru,’ asema Yehova, ‘na hakika mimi nitawarudisha katika jiji hili,+ nao watapiga vita juu yake na kuliteka na kuliteketeza kwa moto;+ na majiji ya Yuda nitayafanya kuwa mahame yenye ukiwa bila mkaaji.’”+

Maelezo ya Chini