Yeremia 22:1-30
22 Yehova amesema hivi: “Shuka nyumbani kwa mfalme wa Yuda, nawe useme hapo neno hili.
2 Nawe useme, ‘Lisikie neno la Yehova, Ee mfalme wa Yuda unayeketi juu ya kiti cha ufalme cha Daudi,+ wewe pamoja na watumishi wako na watu wako, wale wanaoingia kupitia malango haya.+
3 Yehova amesema hivi: “Toeni haki na uadilifu, nanyi mumkomboe yeye anayenyang’anywa kutoka mkononi mwa mpunjaji; wala msimtendee vibaya mkaaji mgeni yeyote, mvulana asiye na baba au mjane.+ Msiwatendee jeuri yoyote.+ Wala msimwage damu yoyote isiyo na hatia mahali hapa.+
4 Kwa maana mkilifanya neno hili kwelikweli, hakika pia wataingia kupitia malango ya nyumba hii wafalme wanaoketi kwa ajili ya Daudi juu ya kiti chake cha ufalme,+ wakipanda magari na farasi, yeye pamoja na watumishi wake na watu wake.”’+
5 “‘Lakini ikiwa hamtayatii maneno haya, mimi ninaapa kwa nafsi yangu mwenyewe,’+ asema Yehova, ‘kwamba nyumba hii itakuwa ukiwa kabisa.’+
6 “Kwa maana Yehova amesema hivi kuhusu nyumba ya mfalme wa Yuda, ‘Wewe ni kama Gileadi kwangu, kichwa cha Lebanoni.+ Hakika nitakufanya uwe nyika;+ nayo majiji, hakuna hata moja litakalokaliwa.+
7 Nami nitatakasa juu yako wale wanaoleta uharibifu,+ kila mmoja na silaha zake;+ nao wataikata mierezi+ yako iliyo bora zaidi na kuiangusha ndani ya moto.+
8 Na kwa kweli mataifa mengi watapita kando ya jiji hili na kila mmoja atamwambia mwenzake: “Kwa nini Yehova alilitendea hivi jiji hili kuu?”+
9 Nao watasema: “Kwa sababu wameliacha agano la Yehova Mungu+ wao na kuinamia miungu mingine na kuitumikia.”’+
10 “Msimlilie aliyekufa,+ wala msimsikitikie. Mlilieni sana yule anayeenda zake, kwa maana hatarudi tena wala kwa kweli hataiona nchi ya jamaa zake.
11 Kwa maana Yehova amesema hivi kumhusu Shalumu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda anayetawala badala ya Yosia baba yake,+ ambaye ameondoka mahali hapa, ‘Hatarudi hapo tena.
12 Kwa maana katika mahali ambapo wamempeleka uhamishoni ndipo atakapokufa, naye hataiona tena nchi hii.’+
13 “Ole wake anayejenga nyumba yake,+ lakini si kwa uadilifu, na vyumba vyake vya juu, lakini si kwa haki, kwa kutumia mwanadamu mwenzake anayetumikia bure, na ambaye hampi malipo yake;+
14 yeye anayesema, ‘Nitajijengea nyumba yenye nafasi tele na vyumba vya juu vyenye nafasi kubwa;+ na madirisha yangu yatapanuliwa kwa ajili yake, nayo itafunikwa kwa mierezi+ na kupakwa rangi nyekundu.’+
15 Je, utaendelea kutawala kwa sababu unashindana kwa kutumia mierezi? Naye baba yako, je, hakula na kunywa na kutekeleza haki na uadilifu?+ Kwa hiyo alifanikiwa.+
16 Alitetea dai halali la mwenye kuteseka na maskini.+ Kwa hiyo akafanikiwa. ‘Je, hiyo haikuwa hivyo kwa sababu ya kunijua mimi?’ asema Yehova.
17 ‘Hakika macho yako na moyo wako haviko juu ya chochote ila pato lisilo la haki,+ na juu ya damu ya asiye na hatia ili kuimwaga,+ na juu ya kupunja na juu ya unyang’anyi ili kuyaendeleza mambo hayo.’
18 “Kwa hiyo Yehova amesema hivi kumhusu Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, ‘Hawataomboleza kwa ajili yake: “Aa! ndugu yangu! Na Aa! dada yangu!” Hawataomboleza kwa ajili yake: “Aa! Ee bwana! Na Aa! heshima yake!”+
19 Atazikwa kwa maziko ya punda-dume,+ kwa kukokotwa na kutupwa, nje ya malango ya Yerusalemu.’+
20 “Panda mpaka Lebanoni+ na upaaze kilio, na juu ya Bashani+ upaaze sauti yako. Na ulie kutoka Abarimu,+ kwa sababu wale wote wanaokupenda sana wamevunjwa-vunjwa.+
21 Nilisema nawe wakati ulipokuwa huna wasiwasi.+ Ulisema, ‘Sitatii.’+ Hii imekuwa njia yako tangu ujana wako, kwa maana hukuitii sauti yangu.+
22 Upepo utawachunga wachungaji wako wote;+ na wale wanaokupenda sana wataingia utekwani.+ Kwa maana wakati huo utaona aibu na hakika ufedheheke kwa sababu ya msiba wako wote.+
23 Ewe unayekaa katika Lebanoni,+ unayekaa katika kiota juu ya mierezi,+ lo! jinsi utakavyougua uchungu wa kuzaa utakapokujia,+ uchungu kama wa mwanamke anayezaa!”+
24 “‘Kama ninavyoishi,’ asema Yehova, ‘hata kama Konia+ mwana wa Yehoyakimu,+ mfalme wa Yuda, angekuwa pete ya muhuri+ kwenye mkono wangu wa kuume, ningekung’oa wewe kutoka hapo!+
25 Nami nitakutia wewe katika mkono wa wale wanaoitafuta nafsi yako+ na katika mkono wa wale unaoogopa na katika mkono wa Nebukadreza mfalme wa Babiloni na katika mkono wa Wakaldayo.+
26 Nami nitakutupa wewe pamoja na mama yako+ aliyekuzaa mwende katika nchi nyingine ambayo hamkuzaliwa huko, nanyi mtakufa huko.+
27 Na katika nchi ambayo watakuwa wakiiinua nafsi yao ili warudi, hawatarudi huko.+
28 Je, mtu huyu Konia+ ni umbo tu lililodharauliwa, lililovunjwa vipande-vipande,+ au ni chombo ambacho hakipendezi?+ Kwa nini yeye na uzao wake ni lazima waangushwe chini na kutupwa katika nchi ambayo hawakuijua?’+
29 “Ee dunia, dunia, dunia, lisikie neno la Yehova.+
30 Yehova amesema hivi, ‘Andikeni kwamba mtu huyu hana mtoto,+ kama mwanamume ambaye hatafanikiwa kwa vyovyote katika siku zake; kwa maana hakuna hata mmoja atakayefanikiwa kwa vyovyote kutoka kwa uzao wake,+ mwenye kuketi juu ya kiti cha ufalme cha Daudi+ na kutawala tena katika Yuda.’”