Mambo ya Walawi 1:1-17
1 Yehova akamwita Musa, akasema naye kutoka katika hema la mkutano,+ akamwambia:
2 “Sema na wana wa Israeli,+ nawe utawaambia, ‘Ikiwa mtu fulani kati yenu atatoa toleo kwa Yehova kutoka katika wanyama wa kufugwa, mtatoa toleo lenu kutoka katika mifugo na kutoka katika kundi.
3 “‘Ikiwa toleo lake ni toleo la kuteketezwa+ kutoka katika mifugo, atamtoa dume, asiye na kasoro.+ Atamtoa kwenye mwingilio wa hema la mkutano kwa hiari yake mwenyewe mbele za Yehova.+
4 Naye ataweka mkono wake juu ya kichwa cha toleo hilo la kuteketezwa, nalo litakubaliwa+ kwa neema ili afanye upatanisho kwa ajili yake.+
5 “‘Kisha yule ng’ombe-dume mchanga atachinjwa mbele za Yehova; na wana wa Haruni, makuhani,+ wataitoa damu na kuinyunyiza damu hiyo kwenye madhabahu kuizunguka pande zote,+ madhabahu iliyo kwenye mwingilio wa hema la mkutano.
6 Nalo toleo la kuteketezwa litachunwa ngozi na kukatwa katika vipande vyake.+
7 Na wana wa Haruni, makuhani, watawasha moto kwenye madhabahu+ na kuweka kuni kwa utaratibu kwenye moto.+
8 Na wana wa Haruni, makuhani, watavipanga vile vipande+ kwa utaratibu, kichwa na mafuta juu ya kuni zilizo katika moto ulio kwenye madhabahu.
9 Na matumbo+ yake na miguu yake itaoshwa kwa maji; naye kuhani atafukiza vyote hivyo kwenye madhabahu viwe toleo la kuteketezwa, toleo linalotolewa kwa njia ya moto lililo na harufu ya kumtuliza Yehova.+
10 “‘Na ikiwa toleo lake linatoka katika kundi,+ kutoka kati ya wana-kondoo dume au mbuzi, wa kiume,+ asiye na kasoro, ndiye atakayemtoa kuwa toleo la kuteketezwa.+
11 Naye atachinjwa kando ya madhabahu kuelekea kaskazini mbele za Yehova, nao wana wa Haruni, makuhani, watainyunyiza damu yake kwenye madhabahu pande zote.+
12 Naye atamkata katika vipande vyake na kichwa chake na mafuta yake, naye kuhani ataviweka kwa utaratibu juu ya kuni zilizo katika moto ulio kwenye madhabahu.+
13 Naye atayaosha matumbo+ na miguu+ kwa maji; naye kuhani atatoa vyote hivyo na kuvifukiza+ kwenye madhabahu. Ni toleo la kuteketezwa, toleo linalotolewa kwa njia ya moto lililo na harufu ya kumtuliza Yehova.+
14 “‘Hata hivyo, ikiwa toleo lake la kuteketezwa kwa Yehova ni toleo linalotoka kati ya ndege, basi atatoa toleo lake kutoka kati ya njiwa-tetere+ au hua wachanga.+
15 Naye kuhani atamtoa kwenye madhabahu na kukikongonyoa+ kichwa chake na kumfukiza kwenye madhabahu, lakini damu yake itamwagwa kando ya madhabahu.
16 Naye ataondoa gole lake na manyoya yake na kuyatupa kando ya madhabahu, upande wa mashariki, mahali pa majivu yenye mafuta.+
17 Naye atampasua kwenye mabawa yake. Hatamgawanya.+ Kisha kuhani atamfukiza kwenye madhabahu juu ya kuni zilizo katika moto. Ni toleo la kuteketezwa,+ toleo linalotolewa kwa njia ya moto lililo na harufu ya kumtuliza Yehova.+