2 Mambo ya Nyakati 1:1-17
1 Naye Sulemani mwana wa Daudi akaendelea kupata nguvu katika ufalme wake,+ na Yehova Mungu wake alikuwa pamoja naye,+ akaendelea kumfanya kuwa mkuu zaidi.+
2 Na Sulemani akasema na Israeli wote, kwa wakuu wa maelfu+ na wa mamia+ na kwa waamuzi+ na wakuu wote wa Israeli,+ vichwa vya nyumba za ukoo wa upande wa baba.+
3 Kisha Sulemani na kutaniko lote pamoja naye wakaenda mahali pa juu palipokuwa katika Gibeoni;+ kwa maana hapo ndipo lilipokuwa lile hema la mkutano+ la Mungu wa kweli, ambalo Musa mtumishi+ wa Yehova alitengeneza nyikani.
4 Hata hivyo, Daudi alikuwa amelileta sanduku+ la Mungu wa kweli kutoka Kiriath-yearimu+ mpaka mahali ambapo Daudi alikuwa amelitayarishia,+ kwa maana alikuwa amelisimamishia hema katika Yerusalemu.+
5 Na ile madhabahu ya shaba+ ambayo Bezaleli+ mwana wa Uri mwana wa Huru+ alikuwa ametengeneza ilikuwa imewekwa mbele ya maskani ya Yehova; na Sulemani na kutaniko wakatoa maombi yao mbele yake kama kawaida.
6 Kisha Sulemani akafanya matoleo hapo mbele za Yehova juu ya ile madhabahu ya shaba ya hema la mkutano, naye akatoa juu yake matoleo elfu moja ya kuteketezwa.+
7 Usiku huo Mungu akamtokea Sulemani na kumwambia: “Omba! Nikupe nini?”+
8 Ndipo Sulemani akamwambia Mungu: “Wewe Ndiye uliyemwonyesha Daudi baba yangu+ fadhili kubwa zenye upendo na kunifanya niwe mfalme mahali pake.+
9 Sasa, Ee Yehova Mungu, acha ahadi yako kwa Daudi baba yangu itimie,+ kwa maana wewe mwenyewe umenifanya kuwa mfalme+ juu ya watu wengi sana kama chembe za mavumbi ya dunia.+
10 Sasa unipe hekima na ujuzi+ ili nitoke mbele ya watu hawa na ili niingie ndani,+ kwa maana ni nani anayeweza kuwahukumu hawa watu wako walio wengi?”+
11 Ndipo Mungu akamwambia Sulemani: “Kwa sababu jambo hili liko moyoni+ mwako nawe hukuomba mali, utajiri wala heshima wala nafsi ya wale wanaokuchukia, wala hata hukuomba wingi wa siku,+ bali unaomba hekima na ujuzi kwa ajili yako ili uwahukumu watu wangu ambao nimekufanya kuwa mfalme juu yao,+
12 unapewa hekima na ujuzi;+ pia nitakupa mali na utajiri na heshima ambavyo hakuna mfalme yeyote aliyekutangulia amepata kuwa navyo,+ wala baada yako hakuna yeyote atakayekuwa navyo.”+
13 Basi Sulemani akatoka pale mahali pa juu palipokuwa katika Gibeoni,+ kutoka mbele ya hema la mkutano,+ akaja Yerusalemu, akaendelea kutawala juu ya Israeli.+
14 Na Sulemani akaendelea kukusanya magari na farasi wa vita hivi kwamba akawa na magari elfu moja na mia nne na farasi wa vita kumi na mbili elfu,+ akawaweka katika majiji ya magari+ na karibu na mfalme katika Yerusalemu.
15 Na mfalme akafanya fedha na dhahabu iliyomo Yerusalemu kuwa kama mawe;+ naye akafanya mierezi iwe kama mikuyu+ iliyoko Shefela+ kwa wingi.
16 Na farasi wa Sulemani walisafirishwa kutoka Misri,+ na wanabiashara wa mfalme wakawa wakichukua kundi la farasi kwa bei fulani.+
17 Nao wakawa wakipandisha na kusafirisha kwa ukawaida gari kutoka Misri kwa vipande 600 vya fedha na farasi kwa vipande 150; na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa wafalme wote wa Wahiti na wafalme wa Siria.+ Walikuwa wakisafirisha vitu kupitia hao.