Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Waroma 15:13​—“Basi Mungu wa Tumaini na Awajaze Ninyi Furaha Yote na Amani”

Waroma 15:13​—“Basi Mungu wa Tumaini na Awajaze Ninyi Furaha Yote na Amani”

 “Mungu anayetoa tumaini na awajaze ninyi shangwe yote na amani kwa kumtegemea, ili tumaini lenu liongezeke kwa nguvu za roho takatifu.”​—Waroma 15:13, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Basi Mungu wa tumaini na awajaze ninyi furaha yote na amani katika kuamini, mpate kuzidi sana kuwa na tumaini, katika nguvu za Roho Mtakatifu.”​—Waroma 15:13, Union Version.

Maana ya Waroma 15:13

 Mtume Paulo alisema maneno hayo kueleza tamaa yake kwamba Mungu awajaze waamini wenzake ‘shangwe na amani.’ Sifa hizo nzuri zinapatana na tumaini ambalo Mungu anatoa na nguvu za roho takatifu.

 Tunajifunza kuhusu tumaini ambalo Mungu anatoa katika Neno lake, Biblia. Kulingana na Waroma 15:4, “mambo yote yaliyoandikwa zamani [katika Biblia] yaliandikwa ili kutufundisha, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutoka kwa Maandiko tuwe na tumaini.” Biblia inafunua ahadi ya Mungu ya kusuluhisha matatizo yanayofanya watu wakose tumaini leo, kama vile umaskini, ukosefu wa haki, ugonjwa na kifo. (Ufunuo 21:4) Mungu atamtumia Yesu Kristo, kutimiza ahadi hizo, na kwa sababu hiyo tuna tumaini la wakati ujao ulio bora zaidi.​—Waroma 15:12.

 Tumaini hilo linalotoka kwa Mungu linaweza ‘kuongezeka’ au “kuzidi sana” ikiwa tu tutamtegemea Mungu. Kadiri tunavyoendelea kujifunza kumhusu Mungu, ndivyo tunavyopata uhakika zaidi kwamba anategemeka kabisa. (Isaya 46:10; Tito 1:2) Kwa sababu ya tumaini lenye kutegemeka ambalo Mungu anatupatia, mtu anaweza kujaa shangwe na amani, hata anapokabili magumu.​—Waroma 12:12.

 Amani, shangwe, na tumaini pia zinahusiana na “roho takatifu,” yaani, nguvu za utendaji za Mungu. a Mungu hutumia roho yake takatifu kutimiza ahadi zake, na hilo linatupatia tumaini. Roho hiyo inaweza kuwasaidia watu, wasitawishe sifa nzuri kama vile shangwe na amani.​—Wagalatia 5:22.

Muktadha wa Waroma 15:13

 Kitabu cha Waroma ni barua iliyoandikwa kwa Wakristo walioishi jijini Roma. Baadhi ya Wakristo hao walikuwa Wayahudi. Paulo aliwatia moyo wote wajitahidi kufikiri na kutenda kwa umoja licha ya tofauti katika malezi na tamaduni zao.​—Waroma 15:6.

 Paulo aliwakumbusha Wakristo huko Roma kwamba, Mungu alikuwa ametabiri zamani kuhusu wakati ambapo watu wa mataifa yote wangemwabudu kwa umoja. Ili kuhakikisha jambo hilo, Paulo alinukuu mara nne kutoka kwa Maandiko ya Kiebrania. b (Waroma 15:9-12) Alimaanisha hivi: Wayahudi na watu wasio Wayahudi pia, wanaweza kunufaika kutokana na huduma ya Kristo. Vikundi vyote viwili vina tumaini lilelile kutoka kwa Mungu. Kwa hiyo wote katika kutaniko la Roma, licha ya asili yao, walitarajiwa ‘kukaribishana,’ yaani kuonyeshana fadhili na ukarimu.​—Waroma 15:7.

a Kwa habari zaidi, soma makala yenye kichwa, “Roho Takatifu Ni Nini?

b Wakati mwingine Maandiko ya Kiebrania yanaitwa Agano la Kale.