Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Niko Tayari Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?

Je, Niko Tayari Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?

 Urafiki wa kimapenzi ni nini?

  •   Ni kawaida kwako kwenda matembezi pamoja na mtu wa jinsia tofauti. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?

  •   Unavutiwa na mtu wa jinsia tofauti naye anavutiwa nawe pia. Mara kadhaa kwa siku unamtumia ujumbe mfupi kwenye simu au unampigia simu. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?

  •   Kila mara mnapokuwa katika tafrija pamoja na marafiki, unatumia muda mwingi pamoja na mtu yuleyule wa jinsia tofauti. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?

 Huenda haikuwa vigumu kwako kujibu swali la kwanza. Lakini huenda ulisita kidogo kabla ya kujibu la pili na la tatu. Urafiki wa kimapenzi ni nini hasa?

 Urafiki wa kimapenzi ni urafiki kati ya watu wawili wanaovutiana kimahaba na unatia ndani shughuli yoyote ya kirafiki ambayo wanafanya pamoja.

 Kwa hiyo, jibu la maswali yote matatu ni ndiyo. Iwe kwa simu, uso kwa uso, mbele ya watu, au mahali pasipo na watu, ikiwa wewe na rafiki yako wa jinsia tofauti mnaonyeshana mahaba na mnawasiliana kwa ukawaida, basi huo ni urafiki wa kimapenzi.

 Ni nini kusudi la kuanzisha urafiki wa kimapenzi?

 Urafiki wa kimapenzi unapaswa kuwa na kusudi lenye kuheshimika, yaani, kumsaidia mwanamume na mwanamke kujua ikiwa wanaweza kufungua ndoa.

 Labda vijana wenzako hawauoni urafiki huo kuwa jambo zito. Pengine wanafurahia tu kuwa na rafiki wa pekee wa jinsia tofauti bila kusudi lolote la kufunga ndoa. Huenda hata wengine wao wanawaona rafiki hao kuwa tuzo au pambo ambalo linawafanya waheshimiwe.

 Hata hivyo, mara nyingi urafiki huo usio na msingi mzuri haudumu. Msichana mmoja anayeitwa Heather alisema hivi: “Vijana wengi ambao wanaanzisha urafiki wa kimapenzi, wanauvunja baada ya juma moja au mawili. Wanaanza kuwa na maoni ya kwamba urafiki huo ni wa muda tu, na maoni hayo yanawatayarisha kwa talaka badala ya ndoa.”

 Ni wazi kwamba unapoanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu fulani, hisia zake zinahusika. Kwa hiyo hakikisha kwamba una nia nzuri.—Luka 6:31.

Ukianzisha urafiki wa kimapenzi bila kusudi la kufunga ndoa, utakuwa kama mtoto anayechezacheza na kitu cha kuchezea kisha anakiacha

 Jiulize: Je, ungependa mtu fulani achezee hisia zako kama vile mtoto anavyochezacheza na kitu cha kuchezea kisha anakiacha? Basi usimchezee mtu mwingine! Biblia inasema kwamba upendo “haujiendeshi bila adabu.”—1 Wakorintho 13:4, 5.

 Msichana anayeitwa Chelsea anasema hivi: “Wakati mwingine ninaona kwamba urafiki wa kimapenzi unapaswa kuwa jambo la kujifurahisha tu, lakini haliwezi kuwa jambo la kujifurahisha tu ikiwa mtu mmoja anauchukulia urafiki huo kwa uzito naye yule mwingine anauona kuwa mchezo tu.”

  Dokezo: Ili ujitayarishe kwa ajili ya kuanzisha urafiki wa kimapenzi na ndoa, soma 2 Petro 1:5-7 na uchague sifa moja ambayo unapaswa kufanyia kazi. Baada ya mwezi mmoja, chunguza uone umejifunza kuihusu kwa kadiri gani na umeifanyia kazi kwa kadiri gani.

 Je, nina umri wa kutosha kuanzisha urafiki wa kimapenzi?

  •    Unafikiri ni umri gani unaofaa kijana kuanzisha urafiki wa kimapenzi?

  •    Sasa mwulize mmoja wa wazazi wako swali hilohilo.

 Kuna uwezekano mkubwa kwamba jibu lako limetofautiana na la mzazi wako. Au labda majibu yanafanana! Huenda ukawa kati ya vijana wengi ambao kwa hekima wanasubiri kuanzisha urafiki wa kimapenzi hadi watakapokuwa na umri wa kutosha kujielewa vizuri zaidi.

 Hivyo ndivyo Danielle, mwenye umri wa miaka 17 alivyoamua kufanya. Anasema hivi: “Nikifikiria jinsi nilivyohisi miaka miwili iliyopita, sifa ambazo ningependa mtu ninayetaka kufunga ndoa naye awe nazo ni tofauti sana ninapolinganisha na zile ninazoangalia sasa. Kwa kweli, hata sasa sioni kama ninaweza kufanya uamuzi mzuri kuhusu hilo. Ninapohisi kwamba nimetulia kwa miaka kadhaa bila kubadili-badili utu wangu, basi nitafikiria kuanzisha urafiki wa kimapenzi.”

 Kuna sababu nyingine kwa nini kuna hekima kusubiri. Biblia inatumia maneno “upeo wa ujana” kufafanua kipindi katika maisha ya mtu ambapo hisia za ngono na za kimahaba huanza kuwa na nguvu sana. (1 Wakorintho 7:36) Kuwa na uhusiano wa karibu na mtu mmoja tu wa jinsia tofauti unapokuwa na umri huo kunaweza kuchochea tamaa hizo na kuongoza katika mwenendo usiofaa.

 Ni kweli huenda hilo lisiwe jambo zito kwa vijana wenzako. Huenda wengi wao wakawa na tamaa ya kufanya ngono. Lakini si lazima​—wala hupaswi—​kufikiri kama wao! (Waroma 12:2) Isitoshe, Biblia inatusihi ‘tuukimbie uasherati.’ (1 Wakorintho 6:18) Unaposubiri hadi upite upeo wa ujana, tunaweza ‘kuondolea mbali msiba.’—Mhubiri 11:10.

 Kwa nini nisubiri kabla ya kuanzisha urafiki wa kimapenzi?

 Kuwa chini ya mkazo wa kuanzisha urafiki wa kimapenzi kabla ya kuwa tayari ni kama kulazimishwa kufanya mtihani wa somo ambalo umeanza tu kujifunza. Bila shaka, utahisi kwamba umeonewa! Unahitaji wakati wa kujifunza somo hilo ili uwe na habari zitakazokuwezesha kupita mtihani huo.

 Ndivyo ilivyo pia kuhusiana na urafiki wa kimapenzi.

 Urafiki wa kimapenzi si mchezo. Kwa hiyo, kabla ya kuwa tayari kumkazia fikira mtu mmoja hususa, unahitaji kujifunza “somo” muhimu—jinsi ya kujenga urafiki.

 Baadaye, utakapompata mtu anayekufaa, utakuwa tayari kujenga urafiki wenye kudumu. Kusema kweli, ndoa nzuri ni muungano wa marafiki wawili wakubwa.

 Kungoja muda upite kabla ya kuanzisha urafiki wa kimapenzi hakukunyimi uhuru. Badala yake, kunakupa uhuru zaidi wa ‘kushangilia katika ujana wako.’ (Mhubiri 11:9) Nawe utakuwa na wakati wa kujitayarisha kwa kuboresha utu wako, na zaidi ya yote, hali yako ya kiroho.—Maombolezo 3:27.

 Kwa sasa, unaweza kufurahia kushirikiana na watu wa jinsia tofauti. Jinsi gani? Njia bora ni kushirikiana nao mkiwa katika vikundi vyenye mchanganyiko wa wavulana na wasichana ambavyo vinasimamiwa vizuri. Msichana anayeitwa Tammy anasema: “Nafikiri inafurahisha zaidi mambo yanapofanywa kwa njia hiyo. Ni afadhali kuwa na marafiki wengi.” Monica anakubaliana naye. Anasema: “Kushirikiana katika vikundi ni wazo zuri, kwa sababu unapata kuchangamana na watu wenye nyutu tofauti-tofauti.”

 Kwa upande mwingine, ukimkazia fikira mtu mmoja tu mapema sana maishani, huenda ukavunjwa moyo. Kwa hiyo, usiwe na haraka. Tumia wakati huu wa maisha yako kujifunza jinsi ya kusitawisha na kudumisha urafiki. Baadaye, ukichagua kuanzisha urafiki wa kimapenzi, utakuwa umejifahamu vizuri zaidi na kufahamu sifa ambazo ungependa mwenzi wa ndoa awe nazo.