Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kufanya Nini ili Niache Kuhuzunika?

Ninaweza Kufanya Nini ili Niache Kuhuzunika?

“Kila wakati rafiki zangu wanapokuwa na matatizo, mimi huwasaidia kuyatatua na kuwafariji. Hata hivyo, jambo ambalo wengi hawajui ni kwamba, ninaporudi nyumbani, mimi huingia chumbani mwangu na kulia.”​—⁠Kellie.

“Ninapokuwa na huzuni, mimi hujitenga na wengine. Nikialikwa mahali, ninatoa kisababu cha kutoenda. Mara nyingi watu wa familia yetu hawajui kwamba nina huzuni. Wao hufikiri niko sawa.”​—⁠Rick.

Umewahi kuwa na maoni kama ya Kellie au Rick? Ikiwa ndiyo, usikate kauli kwamba una kasoro fulani. Ukweli ni kwamba kila mtu huwa na huzuni mara kwa mara. Hata wanaume na wanawake waaminifu katika Biblia walihuzunika nyakati nyingine.​—⁠1 Samweli 1:​6-8; Zaburi 35:14.

Nyakati nyingine, huenda ukajua sababu inayokufanya uhuzunike lakini huenda nyakati nyingine usijue. “Si lazima uwe katika hali mbaya ili uwe na huzuni,” asema Anna, mwenye umri wa miaka 19. “Huzuni inaweza kutokea wakati wowote, hata wakati ambapo huna matatizo. Ni jambo lisiloeleweka, lakini ndivyo ilivyo!”

Haidhuru sababu ni nini, au hata kama hakuna sababu, unaweza kufanya nini unapolemewa na huzuni? Jaribu mambo yafuatayo:

  1. Zungumza kuhusu hali yako. Alipokuwa katika taabu, Ayubu alisema hivi: “Nitasema kwa uchungu wa nafsi yangu!”​—⁠Ayubu 10:1.

    Kellie: Baada ya kuongea na mtu kuhusu tatizo langu, mimi huhisi nimetulia sana. Hatimaye, kuna mtu anayeelewa kile ninachopitia. Ninajua kwamba anaweza kuniokoa—atanisaidia nikabiliane na huzuni yangu!

  2. Andika kuhusu hisia zako. Unapokuwa na huzuni nyingi, huenda ikawa vizuri kuandika mawazo yako. Nyakati nyingine Daudi alieleza huzuni yake kubwa katika zaburi alizoandika kwa kuongozwa na roho ya Mungu. (Zaburi 6:6) Kuandika kuhusu hisia zako kutakusaidia ‘ulinde hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.’​—⁠Methali 3:​21.

    Heather: Kuandika hunisaidia kupanga mawazo yangu mengi yanayosababishwa na huzuni. Unapofaulu kueleza hisia zako na kupanga mawazo yako, huzuni haitakulemea.

  3. Sali kuhusu tatizo lako. Biblia inasema kwamba unaposali kuhusu mahangaiko yako, ‘amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote italinda moyo wako na nguvu zako za akili.’​—⁠Wafilipi 4:​6, 7.

    Esther : Nilijaribu sana kuelewa sababu iliyonifanya nihuzunike, lakini sikufua dafu. Nilimwomba Yehova anisaidie niwe mwenye furaha. Kuhuzunika bila sababu yoyote kulinichosha sana. Hatimaye nilifaulu kukabiliana na tatizo hilo. Usifikiri kamwe kwamba sala haina nguvu!

    Ukijitahidi na kutafuta msaada, unaweza kutoka katika lindi la huzuni

    Pendekezo: Tumia Zaburi 139:23, 24 kama kielelezo cha sala yako mwenyewe kwa Yehova. Mweleze Yehova hisia zako zote za ndani kabisa, na umwombe akusaidie kutambua chanzo cha huzuni yako.

Pamoja na madokezo yaliyo juu, Neno la Mungu, Biblia, ni msaada mkubwa. Kujaza akili yako mambo yenye kujenga yanayopatikana katika masimulizi ya Biblia kunaweza kufanya uhisi vizuri.​—⁠Zaburi 1:​1-3.

Unapoendelea Kuwa na Huzuni

Ryan anasema: “Nyakati nyingine ninapoamka asubuhi, mimi huhisi ni afadhali nibaki kitandani tu badala ya kuamka na kushinda siku nzima nikiwa na huzuni.” Ryan anaugua ugonjwa wa kushuka moyo sana na kuna watu wengi kama yeye. Uchunguzi unaonyesha kwamba kijana 1 kati ya vijana 4 huugua aina fulani ya ugonjwa wa kushuka moyo sana kabla ya kuwa mtu mzima.

Unaweza kujua jinsi gani ikiwa unaugua ugonjwa wa kushuka moyo? Dalili fulani zinatia ndani badiliko kubwa la hisia na mwenendo, kujitenga na watu, kutopendezwa na karibu kila kitu, badiliko kubwa katika mazoea ya kula na kulala, na hisia kali za kujidharau au kuhisi hatia bila msingi wowote.

Ni kweli kwamba mara kwa mara karibu kila mtu huwa na dalili moja au zaidi kati ya hizo. Hata hivyo, dalili hizo zikiendelea kwa zaidi ya majuma kadhaa, zungumza na wazazi wako ili wafanye mpango umwone daktari. Daktari anaweza kujua iwapo huzuni yako inatokana na ugonjwa fulani.

Ikiwa una ugonjwa wa kushuka moyo sana, usiaibike. Baada ya kupata matibabu, wengi wanaougua wamepata nafuu—na huenda hata sasa wanahisi vizuri kuliko wakati mwingine wowote! Iwe huzuni yako inasababishwa na kushuka moyo au la, kumbuka maneno yenye kufariji ya Zaburi 34:18: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”