Hamia kwenye habari

Ubatizo Ni Nini?

Ubatizo Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Kubatizwa ni kuzamishwa kabisa ndani ya maji. a Biblia inataja ubatizo wa watu mbalimbali. (Matendo 2:41) Mmoja kati yao ni Yesu ambaye alibatizwa kwa kuzamishwa ndani ya Mto Yordani. (Mathayo 3:13, 16) Miaka mingi baadaye, mwanamume Mwethiopia alibatizwa katika “mahali penye maji” kando ya barabara aliyokuwa akisafiria.​—Matendo 8:36-40.

 Yesu alifundisha kwamba ubatizo ni takwa kwa wafuasi wake. (Mathayo 28:19, 20) Mtume Petro pia alitaja jambo hilo waziwazi.​—1 Petro 3:21.

Katika makala hii

 Ubatizo unamaanisha nini?

 Ubatizo ni ishara ya nje, au wonyesho wa hadharani, kwamba mtu anayebatizwa ametubu dhambi zake na kwamba amemwahidi Mungu atafanya mapenzi yake bila masharti. Hilo linamaanisha kwamba atamtii Mungu na Yesu katika sehemu zote za maisha yake. Watu wanaobatizwa wanaanza kuishi katika njia ambayo Mungu anatazamia waishi, njia inayoongoza kwenye uzima wa milele.

 Kuzamishwa ndani ya maji ni ishara inayofaa kabisa kuonyesha badiliko ambalo mtu amefanya maishani mwake. Kwa nini? Biblia inalinganisha ubatizo na maziko. (Waroma 6:4; Wakolosai 2:12) Mtu anapozamishwa ndani ya maji, anaonyesha kwamba amekufa kuhusiana na maisha aliyokuwa akiishi hapo awali. Anapoinuliwa kutoka kwenye maji, anaonyesha kwamba anaanza kuishi mapya akiwa Mkristo aliyejiweka wakfu.

 Biblia inasema nini kuhusu kuwabatiza watoto wachanga?

 Biblia haitaji popote maneno “ubatizo wa watoto.” b Wala haifundishi kwamba watoto wachanga wanapaswa kubatizwa.

 Kuwabatiza watoto wachanga hakupatani na Maandiko. Biblia inafundisha kwamba mtu anayetaka kubatizwa lazima atimize matakwa fulani. Kwa mfano, anapaswa kuelewa angalau mafundisho ya msingi ya Neno la Mungu na anapaswa kuwa akiishi kupatana na mafundisho hayo. Anapaswa kuwa ametubu dhambi zake. Na anapaswa kuwa amejiweka wakfu kwa Mungu kupitia sala. (Matendo 2:38, 41; 8:12) Watoto wachanga hawawezi kufanya mambo hayo.

 Inamaanisha nini kubatizwa katika jina la Baba, la Mwana, na la roho takatifu?

 Yesu aliwaagiza wafuasi wake hivi: “Mkafanye wanafunzi . . . . mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.” (Mathayo 28:19, 20) Maneno “katika jina la” yanamaanisha kwamba yule anayebatizwa anaelewa na kukubali mamlaka na cheo cha Baba na cha Mwana, kutia ndani jukumu la roho takatifu ya Mungu. Kwa mfano: Mtume Petro alimwambia hivi mwanamume ambaye alikuwa mlemavu tangu alipozaliwa: “Katika jina la Yesu Kristo Mnazareti, tembea!” (Matendo 3:6) Maana iko wazi—Petro alitambua na kukubali mamlaka ya Kristo na akampa sifa kwa muujiza huo wa uponyaji.

  •   “Baba” anarejelea Yehova c Mungu. Akiwa Muumba, Mpaji-Uhai, na Mungu Mweza-Yote, Yehova ana mamlaka kamili.​—Mwanzo 17:1; Ufunuo 4:11.

  •   “Mwana” ni Yesu Kristo, ambaye alitoa uhai wake kwa ajili yetu. (Waroma 6:23) Hatuwezi kuokolewa isipokuwa tutambue na kuthamini jukumu muhimu la Yesu katika kusudi la Mungu kwa wanadamu.​—Yohana 14:6; 20:31; Matendo 4:8-12.

  •   “Roho takatifu” ni kani ya utendaji ya Mungu, au nguvu zake zinazotenda. d Mungu ametumia roho yake takatifu kuumba, kutokeza uhai, na kuwasilisha ujumbe kwa manabii wake na kwa wengine, na pia kuwapa nguvu za kufanya mapenzi yake. (Mwanzo 1:2; Ayubu 33:4; Waroma 15:18, 19) Pia, Mungu alitumia roho takatifu kuwaongoza waandikaji wa Biblia kuandika mawazo yake.​—2 Petro 1:21.

 Je, ni dhambi kubatizwa tena?

 Si ajabu kwa mtu kubadili dini yake. Lakini vipi ikiwa alikuwa amebatizwa katika dini aliyotoka? Je, ni dhambi kubatizwa tena? Watu fulani hujibu ndiyo, labda kwa kutegemea andiko la Waefeso 4:5, linalosema: “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.” Hata hivyo, mstari huo haumaanishi kwamba mtu hawezi kubatizwa tena. Kwa nini?

 Muktadha. Muktadha wa Waefeso 4:5 unaonyesha kwamba mtume Paulo alikuwa akikazia umuhimu wa Wakristo wa kweli kuwa na umoja katika imani. (Waefeso 4:5, 1-3, 16) Umoja huo unaweza kupatikana tu ikiwa wanamfuata Bwana yuleyule, Yesu Kristo; wana imani ileile, au uelewaji uleule kuhusu kile ambacho Biblia inafundisha; na wanafuata matakwa yaleyale ya Kimaandiko kuhusu ubatizo.

 Mtume Paulo aliwatia moyo baadhi ya watu ambao tayari walikuwa wamebatizwa wabatizwe upya. Sababu ya kufanya hivyo ni kwamba walikuwa wamebatizwa kabla ya kupata uelewaji kamili wa mafundisho ya Kikristo.​—Matendo 19:1-5.

 Msingi sahihi wa ubatizo. Ili ubatizo ukubaliwe na Mungu, unapaswa kutegemea ujuzi sahihi wa kweli ya Biblia. (1 Timotheo 2:3, 4) Mtu anapobatizwa kwa msingi wa mafundisho ya kidini ambayo yanapingana na Biblia, ubatizo huo hautambuliwi na Mungu. (Yohana 4:23, 24) Huenda ikawa mtu huyo alikuwa mnyoofu, lakini hakutenda “kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Ili kupata kibali cha Mungu, anahitaji kujifunza kweli ya Biblia, afuate mambo aliyojifunza, ajiweke wakfu kwa Mungu, na kubatizwa tena. Chini ya hali hizo, kubatizwa upya si dhambi. Badala yake, hilo ndilo jambo sahihi la kufanya.

 Ubatizo mwingine unaotajwa katika Biblia

 Biblia inataja ubatizo mwingine mbalimbali uliokuwa na maana tofauti na ule ubatizo wa kuzamishwa ndani ya maji uliofanywa na wafuasi wa Kristo. Fikiria mifano kadhaa.

 Ubatizo uliofanywa na Yohana Mbatizaji. e Wayahudi na wageuzwa-imani walibatizwa na Yohana kama ishara ya kwamba wametubu dhambi walizotenda dhidi ya Sheria ya Musa, yaani, Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli kupitia Musa. Ubatizo wa Yohana uliwatayarisha watu ili wamtambue na kumkubali Masihi, Yesu wa Nazareti.​—Luka 1:13-17; 3:2, 3; Matendo 19:4.

 Ubatizo wa Yesu mwenyewe. Ubatizo wa Yesu uliofanywa na Yohana Mbatizaji ulikuwa wa pekee. Yesu alikuwa mwanamume mkamilifu ambaye hakutenda dhambi. (1 Petro 2:21, 22) Kwa hiyo, ubatizo wake haukuhusisha toba au “ombi linalotolewa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema.” (1 Petro 3:21) Badala yake, ulionyesha kwamba alikuwa akijitoa kwa Mungu kufanya mapenzi Yake akiwa Masihi, au Kristo, aliyetabiriwa. Hilo lilitia ndani kufa kwa ajili yetu.​—Waebrania 10:7-10.

 Kubatizwa kwa roho takatifu. Yohana Mbatizaji na Yesu Kristo walizungumza kuhusu kubatizwa kwa roho takatifu. (Mathayo 3:11; Luka 3:16; Matendo 1:1-5) Ubatizo huo si sawa na ubatizo katika jina la roho takatifu. (Mathayo 28:19) Kwa nini?

 Ni wafuasi wachache tu wa Yesu wanaobatizwa kwa roho takatifu. Wafuasi hao wanatiwa mafuta kwa roho takatifu kwa sababu wanaitwa wakatumikie pamoja na Kristo mbinguni wakiwa wafalme na makuhani juu ya dunia. f (1 Petro 1:3, 4; Ufunuo 5:9, 10) Raia wao watakuwa mamilioni ya wafuasi wa Yesu ambao wana tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani.​—Mathayo 5:5; Luka 23:43.

 Ubatizo katika Kristo Yesu na katika kifo chake. Watu wanaobatizwa kwa roho takatifu pia ‘wanabatizwa katika Kristo Yesu.’ (Waroma 6:3) Hivyo, ubatizo huo unawahusu wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta, ambao watatawala pamoja naye mbinguni. Kwa kubatizwa katika Yesu, wanakuwa washiriki wa kutaniko lake lililotiwa mafuta. Yeye ndiye Kichwa, nao ndio mwili.​—1 Wakorintho 12:12, 13, 27; Wakolosai 1:18.

 Wakristo watiwa-mafuta pia ‘wanabatizwa katika kifo chake Yesu.’ (Waroma 6:3, 4) Kwa kumwiga Yesu, wanaishi maisha ya kujidhabihu kwa kumtii Mungu na wanajua kwamba hawana tumaini la kuishi milele duniani. Wanakamilisha ubatizo huo wa mfano wanapokufa na kupokea ufufuo wa kuishi mbinguni wakiwa viumbe wa roho.​—Waroma 6:5; 1 Wakorintho 15:42-44.

 Kubatizwa kwa moto. Yohana Mbatizaji aliwaambia wasikilizaji wake hivi: “Yeye [Yesu] atawabatiza ninyi kwa roho takatifu na kwa moto. Sepetu yake ya kupepetea imo mkononi mwake, naye atausafisha kabisa uwanja wake wa kupuria, na kukusanya ngano yake katika ghala, lakini atayateketeza makapi kwa moto usioweza kuzimwa.” (Mathayo 3:11, 12) Ona kwamba kuna tofauti kati ya kubatizwa kwa moto na kubatizwa kwa roho takatifu. Yohana alimaanisha nini alipotoa mfano huu?

 Ngano inawakilisha wale watakaomsikiliza na kumtii Yesu. Wana tumaini la kubatizwa kwa roho takatifu. Makapi yanawakilisha wale ambao hawatamsikiliza Yesu. Mwisho wao ni ubatizo kwa moto, unaowakilisha uharibifu wa milele.​—Mathayo 3:7-12; Luka 3:16, 17.

a Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ubatizo” linarejelea “kuingia ndani ya maji, kuzamishwa, na kuinuliwa,” kulingana na Vine’s Complete Expository Dictionary of Old and New Testament Words.

b Makanisa fulani hufanya sherehe ambapo watoto wachanga wanapewa jina kisha “wanabatizwa” kwa kunyunyiziwa maji kichwani.

c Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?

d Ona makala “Roho Takatifu Ni Nini?

g Biblia pia hutumia neno “ubatizo” kufafanua aina fulani ya usafi wa kisherehe, kama vile kumwagilia vyombo maji. (Marko 7:4; Waebrania 9:10) Bila shaka, aina hiyo ya ubatizo ni tofauti na kuzamishwa kabisa ndani ya maji kama Yesu na wafuasi wake walivyofanya.