Hamia kwenye habari

Inakuwaje Tunapokufa?

Inakuwaje Tunapokufa?

Jibu la Biblia

 Biblia inasema: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5; Zaburi 146:4) Kwa hiyo, tunapokufa, hatupo. Wafu hawafikiri, hawatendi, wala kuhisi chochote.

“Utarudi mavumbini”

 Mungu alieleza kile kinachotokea tunapokufa aliposema na mwanadamu wa kwanza, Adamu. Kwa sababu Adamu alikosa kutii, Mungu alimwambia hivi: “Wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Mwanzo 3:19) Kabla ya Mungu kumuumba Adamu “kutoka katika mavumbi ya nchi,” hakuwepo. (Mwanzo 2:7) Vivyo hivyo, Adamu alipokufa, alirudi mavumbini na kuacha kuwapo.

 Jambo hilohilo hutukia kwa wale wanaokufa wakati huu. Inapozungumzia kuhusu wanadamu na wanyama, Biblia husema: “Wote wametoka katika mavumbi, nao wote wanarudi mavumbini.”​—Mhubiri 3:19, 20.

Kifo si mwisho wa mambo yote

 Biblia inalinganisha kifo na usingizi. (Zaburi 13:3; Yohana 11:11-14; Matendo 7:60) Mtu aliyelala usingizi mzito hajui jambo lolote linaloendelea. Ndivyo ilivyo kwa wafu pia, hawajui lolote. Hata hivyo, Biblia inafundisha kwamba Mungu anaweza kuwaamsha wafu kana kwamba walikuwa wamelala na kuwapa uhai tena. (Ayubu 14:13-15) Kwa wale ambao Mungu huwafufua, kifo si mwisho wa mambo yote.