Je, Mungu Yuko Kila Mahali?
Jibu la Biblia
Mungu ana uwezo wa kuona kila kitu na kutenda popote anapotaka. (Methali 15:3; Waebrania 4:13) Hata hivyo, Biblia haifundishi kwamba Mungu yuko kila mahali na ndani ya kila kitu. Badala yake, inafundisha kwamba yeye ni mtu na ana makao.
Umbo la Mungu: Mungu ni Roho. (Yohana 4:24) Hawezi kuonekana na wanadamu. (Yohana 1:18) Maono yote yaliyorekodiwa katika Biblia kumhusu Mungu yanamwonyesha akiwa na makao hususa. Haonyeshwi kamwe akiwa kila mahali.—Isaya 6:1, 2; Ufunuo 4:2, 3, 8.
Makao ya Mungu: Mungu anakaa katika makao ya kiroho, ambayo ni tofauti kabisa na uumbaji halisi. Makao yake yako mbinguni. (1 Wafalme 8:30) Biblia inataja pindi ambapo viumbe wa roho “waliingia na kusimama mbele za Yehova,” a kuonyesha kwa njia fulani kwamba Mungu anakaa mahali fulani hususa.—Ayubu 1:6.
Ikiwa Mungu hayuko kila mahali, je, anaweza kunijali?
Ndiyo. Mungu anawajali sana wanadamu mmojammoja. Ingawa anaishi katika makao ya kiroho, Mungu anawaona watu duniani wanaotaka kikweli kumpendeza, naye anatenda kwa niaba yao. (1 Wafalme 8:39; 2 Mambo ya Nyakati 16:9) Fikiria jinsi ambavyo Yehova huonyesha kwamba anawajali watu wanaomwabudu kikweli:
Unaposali: Yehova anaweza kusikia sala yako mara tu unaposali.—2 Mambo ya Nyakati 18:31.
Unaposhuka moyo: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zaburi 34:18.
Unapohitaji mwongozo: Yehova atakufanya “uwe na ufahamu na kukufundisha” kupitia Neno lake, Biblia.—Zaburi 32:8.
Maoni yasiyo sahihi kuhusu kuwepo kwa Mungu
Maoni yasiyo sahihi: Mungu yuko kila mahali katika uumbaji.
Ukweli: Mungu hakai duniani wala mahali pengine popote katika ulimwengu halisi. (1 Wafalme 8:27) Ni kweli kwamba nyota na kazi nyingine za uumbaji “zinatangaza utukufu wa Mungu.” (Zaburi 19:1) Hata hivyo, Mungu hakai ndani ya uumbaji wake, kama tu ambavyo msanii hawezi kukaa ndani ya picha aliyochora mwenyewe. Hata hivyo, picha hiyo inaweza kutueleza jambo fulani kumhusu msanii aliyeichora. Vivyo hivyo, ulimwengu unaoonekana unatueleza mengi kuhusu ‘sifa za Muumba ambazo hazionekani,’ kama vile nguvu, hekima, na upendo wake.—Waroma 1:20.
Maoni yasiyo sahihi: Lazima Mungu awe kila mahali ili aweze kujua kila kitu na kuwa Mweza-Yote.
Ukweli: Roho takatifu ya Mungu, au kani ya utendaji, ni nguvu za Mungu zinazotenda. Kupitia roho hiyo takatifu, Mungu anaweza kutambua na kufanya chochote, popote, na wakati wowote, bila yeye mwenyewe kuwa hapo.—Zaburi 139:7.
Maoni yasiyo sahihi: Zaburi 139:8 inafundisha kwamba Mungu yuko kila mahali inaposema: “Kama ningepanda mbinguni, ungekuwa huko; na kama ningetandika kitanda changu katika Kaburi, tazama! ungekuwa huko.”
Ukweli: Andiko hilo halizungumzi kuhusu mahali Mungu alipo. Linafundisha kwa njia ya kishairi kwamba hakuna mahali ambapo ni mbali sana hivi kwamba Mungu hawezi kutusaidia.
a Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.