Hamia kwenye habari

Biblia Inafundisha Nini Kuhusu Kusema kwa Lugha?

Biblia Inafundisha Nini Kuhusu Kusema kwa Lugha?

Jibu la Biblia

 ‘Kusema kwa lugha’ kunarejelea uwezo wa kimuujiza ambao Wakristo fulani wa mapema walikuwa nao uliowawezesha kuzungumza katika lugha ambazo hawakuwa wamejifunza awali. (Matendo 10:46, Union Version) Kila mtu aliyejua lugha hiyo alimwelewa yule anayezungumza. (Matendo 2:​4-8) Kusema kwa lugha ni moja kati ya zawadi za roho takatifu ambazo Mungu aliwapa baadhi ya Wakristo katika karne ya kwanza.​—Waebrania 2:4; 1 Wakorintho 12:​4, 30.

 Kusema kwa lugha kulianzia wapi na lini?

 Muujiza huu ulifanyika kwa mara ya kwanza Yerusalemu asubuhi ya Sherehe ya Kiyahudi ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Wanafunzi 120 hivi wa Yesu walikuwa wamekusanyika pamoja wakati ambapo “wote wakajazwa roho takatifu, wakaanza kusema katika lugha mbalimbali.” (Matendo 1:​15; 2:​1-4) Umati mkubwa wa watu “kutoka kila taifa lililo chini ya mbingu” ukakusanyika, na “kila mmoja wao aliwasikia wakiongea katika lugha yake mwenyewe.”​—Matendo 2:​5, 6.

 Kusudi la kusema kwa lugha lilikuwa nini?

  1.   Kuonyesha kwamba Mungu alikuwa akiwaunga mkono Wakristo. Zamani, Mungu alifanya ishara za kimuujiza ili kuthibitisha kwamba alikuwa akiwaunga mkono watu waaminifu kama vile Musa. (Kutoka 4:​1-9, 29-​31; Hesabu 17:10) Kusema kwa lugha kulitimiza kusudi kama hilo, kuonyesha kwamba Mungu alikuwa akilitegemeza kutaniko la Kikristo lililokuwa limetoka kuanzishwa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Lugha si ishara kwa ajili ya waamini bali kwa wasio waamini.”​—1 Wakorintho 14:22.

  2.   Ili kuwawezesha Wakristo kutoa ushahidi kamili. Wale waliowasikiliza wafuasi wa Yesu siku ya Pentekoste walisema hivi: “Tunawasikia wakisema katika lugha zetu kuhusu mambo makuu ya Mungu.” (Matendo 2:​11) Hivyo, kusudi lingine muhimu la muujiza huo lilikuwa kuwawezesha Wakristo “kutoa ushahidi kamili” na ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ kama Yesu alivyokuwa amewaamuru. (Matendo 10:42; Mathayo 28:19) Watu 3,000 hivi ambao waliona muujiza huo na kuwasikiliza wakitoa ushahidi wakawa wanafunzi siku hiyo.​—Matendo 2:​41.

 Je, kusema kwa lugha kulipaswa kuendelea?

 Hapana. Zawadi za roho takatifu, kutia ndani zawadi ya kusema kwa lugha, zilikuwa za muda tu. Biblia ilitabiri hivi: “Kama kuna zawadi za unabii, zitaondolewa; kama kuna lugha, zitakoma.”​—1 Wakorintho 13:8.

 Kusema kwa lugha kulikoma lini?

 Zawadi za roho takatifu zilipitishwa kwa Wakristo wengine mitume walipokuwepo, mara nyingi mitume waliweka mikono yao juu ya waamini wenzao ili wazipate. (Matendo 8:​18; 10:44-​46) Inaonekana kwamba wale waliopokea zawadi za roho kutoka kwa mitume hawakuwapitishia wengine. (Matendo 8:​5-7, 14-​17) Kwa mfano, ofisa wa serikali anaweza kumpa mtu leseni ya udereva, lakini mtu huyo hajapewa mamlaka ya kisheria ya kumpa mtu mwingine leseni. Kwa hiyo, inaonekana kwamba kusema kwa lugha kulikoma baada ya mitume na pia wale ambao walikuwa wamepata zawadi hiyo moja kwa moja kutoka kwa mitume walipokufa.

 Vipi kuhusu kusema kwa lugha leo?

 Ni wazi kwamba zawadi ya kimuujiza ya kusema kwa lugha ilikoma mwishoni mwa karne ya kwanza W.K. hivi. Hakuna mtu leo anayeweza kudai kwa usahihi kwamba nguvu za Mungu zimemwezesha kusema kwa lugha. a

 Wakristo wa kweli wanaweza kutambuliwaje?

 Yesu alisema kwamba upendo wa kujidhabihu ndio ungewatambulisha wanafunzi wake. (Yohana 13:34, 35) Vivyo hivyo, mtume Paulo alifundisha kwamba upendo ungekuwa utambulisho wa kudumu wa Wakristo wa kweli. (1 Wakorintho 13:​1, 8) Alionyesha kwamba roho ya Mungu ingetokeza sifa ndani ya Wakristo ambazo kwa ujumla zinaitwa “tunda la roho,” sifa ya kwanza ikiwa ni upendo.​—Wagalatia 5:​22, 23.