Hamia kwenye habari

Kuja kwa Kristo Kunamaanisha Nini?

Kuja kwa Kristo Kunamaanisha Nini?

Jibu la Biblia

 Maandiko yanataja mara nyingi sana kuhusu wakati ambapo Kristo atakuja kuwahukumu watu duniani. a Kwa mfano, Mathayo 25:31-​33 inasema hivi:

 “Wakati Mwana wa binadamu [Yesu Kristo] atakapofika katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu, mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi. Naye atawaweka kondoo kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto.”

 Kipindi hicho cha hukumu kitakuwa sehemu ya “dhiki kuu” ambayo haijawahi kutokea tena katika historia. Dhiki hiyo itafikia mwisho wakati wa vita vya Har-Magedoni. (Mathayo 24:21; Ufunuo 16:16) Maadui wa Kristo, wanaofafanuliwa katika mfano wake kuwa mbuzi, “watahukumiwa adhabu ya uharibifu wa milele.” (2 Wathesalonike 1:9; Ufunuo 19:11, 15) Hata hivyo, watumishi wake waaminifu, wanaofananishwa na kondoo, watakuwa na tumaini la kupata “uzima wa milele.”​—Mathayo 25:46.

Kristo atakuja lini?

 Yesu alisema hivi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua.” (Mathayo 24:36, 42; 25:13) Hata hivyo, alizungumzia “ishara” inayoonekana, yenye mambo mengi, ambayo ingetambulisha kipindi kinachoongoza kwenye kuja kwake.​—Mathayo 24:​3, 7-​14; Luka 21:10, 11.

Je, Kristo anakuja akiwa na mwili wa roho au wa nyama?

 Yesu alifufuliwa akiwa na mwili wa roho, kwa hiyo anakuja akiwa kiumbe wa roho, si akiwa na mwili wa nyama. (1 Wakorintho 15:45; 1 Petro 3:​18) Hiyo ndiyo sababu Yesu aliwaambia hivi mitume wake siku iliyotangulia kifo chake: “Bado muda kidogo zaidi na ulimwengu hautaniona tena.”​—Yohana 14:19.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu kuja kwa Kristo

 Uwongo: Biblia inaposema kwamba watu watamwona Yesu “akija juu ya mawingu,” inamaanisha kwamba Yesu ataonekana anapokuja.​—Mathayo 24:30.

 Ukweli: Mara nyingi Biblia inahusianisha mawingu na kitu kilichofichika. (Mambo ya Walawi 16:2; Hesabu 11:25; Kumbukumbu la Torati 33:26) Kwa mfano, Mungu alimwambia Musa hivi: “Nitakujia katika wingu lenye giza.” (Kutoka 19:9) Musa hakumwona Mungu kihalisi. Vivyo hivyo, Kristo ‘anakuja juu ya mawingu’ katika maana ya kwamba watu watatambua kuwa amekuja ingawa hawatamwona kwa macho halisi.

 Uwongo: Maneno “kila jicho litamwona” yanayotumiwa katika Ufunuo 1:7 kuzungumzia kuja kwa Kristo, yanapaswa kueleweka kihalisi.

 Ukweli: Maneno ya Kigiriki “jicho” na “kuona” yanayotajwa katika Biblia, nyakati nyingine hutumiwa kumaanisha utambuzi au uelewaji badala ya kurejelea uwezo wa kuona. b (Mathayo 13:15; Luka 19:42; Waroma 15:21; Waefeso 1:​18) Biblia inasema kwamba Yesu aliyefufuliwa ndiye “anayekaa katika nuru isiyoweza kufikiwa, ambaye hakuna hata mmoja kati ya wanadamu . . . anaweza kumwona.” (1 Timotheo 6:​16) Hivyo, “kila jicho litamwona” katika maana ya kwamba watatambua Yesu ndiye anayetekeleza hukumu ya Mungu.​—Mathayo 24:30.

 Uwongo: Maneno ya 2 Yohana 7 yanaonyesha kwamba Yesu atarudi katika mwili.

 Ukweli: Mstari huo wa Biblia unasema: “Wadanganyifu wengi wametokea katika ulimwengu, watu ambao hawamkiri Yesu Kristo kuwa alikuja katika mwili.”

 Katika siku za mtume Yohana, watu fulani walipinga kwamba Yesu alikuja duniani akiwa na mwili wa nyama. Watu hao waliitwa Waagnosti. Mstari wa 7 wa barua ya pili ya Yohana uliandikwa ili kupinga dai hilo la uwongo.

a Ingawa watu wengi hutumia msemo “kuja mara ya pili” au “kuja kwa pili” ili kurejelea kuja kwa Kristo, maneno hayo hayapatikani katika Biblia.

b Ona kitabu The New Thayer’s Greek-English Lexicon of the New Testament (1981), ukurasa wa 451 na 470.