Hamia kwenye habari

Ninahisi Nina Hatia​—Je, Biblia Inaweza Kunisaidia Nijihisi Vizuri?

Ninahisi Nina Hatia​—Je, Biblia Inaweza Kunisaidia Nijihisi Vizuri?

Jibu la Biblia

 Ndiyo. Biblia inaweza kutusaidia kukabiliana kwa hekima na hisia za hatia. (Zaburi 32:1-5) Ikiwa tumekosea kwa njia fulani lakini tunajutia kikweli kosa letu, Mungu atatusamehe na kutusaidia kuhisi vizuri. (Zaburi 86:5) Biblia inaonyesha kwamba kuna faida kuwa na hisia za hatia—zinaweza kutuchochea kurekebisha mwenendo usiofaa na kujaribu sana kuepuka mwenendo huo wakati ujao. (Zaburi 51:17; Methali 14:9) Hata hivyo, Biblia inatuonya dhidi ya kujihisi tuna hatia kupita kiasi, labda tukijiona kuwa hatuna tumaini au hatufai machoni pa Mungu. Kujihukumu kwa ukatili kadiri hiyo kunaweza kutufanya ‘tulemewe na huzuni inayopita kiasi.’—2 Wakorintho 2:7.

 Ni nini huwafanya watu wawe na hisia za hatia?

 Kuna sababu kadhaa zinazoweza kutufanya tujihisi tuna hatia. Tunaweza kuhisi kwamba tumemkosea mtu tunayempenda au tumeshindwa kufikia kiwango ambacho tunapaswa kuishi kulingana nacho. Nyakati fulani, tunaweza kujihisi tuna hatia bila hata kuwa na hatia. Kwa mfano, tunapojiwekea viwango vya juu sana, kuna uwezekano kwamba tutajihisi tuna hatia kila mara tunaposhindwa kufikia viwango hivyo. Hiyo ndiyo sababu Biblia inatutia moyo tuwe na usawaziko kuhusu mambo tunayotarajia kutimiza.​—Mhubiri 7:16.

 Ninaweza kukabilianaje na hisia za hatia?

 Badala ya kukata tamaa kwa sababu ya kuhisi una hatia, fanya kile unachoweza ili kurekebisha mambo. Jinsi gani?

  •   Kubali makosa yako. Kupitia sala, mwombe Yehova a Mungu akusamehe. (Zaburi 38:18; Luka 11:4) Unaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atasikia maombi yako ikiwa unatubu na kujuta kikweli na ikiwa utajaribu kabisa kuepuka kurudia kosa lako. (2 Mambo ya Nyakati 33:13; Zaburi 34:18) Anaweza kumwona yule mtu wa ndani, ambaye hakuna mwanadamu anaweza kumwona. Mungu anapotuona tukijitahidi kuacha mwenendo mbaya, “yeye ni mwaminifu na mwadilifu naye atatusamehe dhambi zetu.”—1 Yohana 1:9; Methali 28:13.

     Bila shaka, ikiwa umemkosea mtu fulani, huenda ukahitaji kukubali jambo hilo na kumwomba mtu huyo msamaha kwa unyoofu. Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo! Utahitaji kuwa jasiri na mwenye unyenyekevu. Lakini kuomba msamaha kutoka moyoni hutimiza mambo mawili muhimu: Kutakusaidia kutua mzigo mzito sana na kudumisha amani.—Mathayo 3:8; 5:23, 24.

  •   Tafakari maandiko kuhusu rehema ya Mungu. Kwa mfano, fikiria 1 Yohana 3:19, 20. Biblia inaonyesha wazi kwamba “huenda mioyo yetu ikatuhukumu”—yaani, huenda tukajichambua kupita kiasi, labda tukijiambia kwamba hatustahili upendo wa Mungu. Hata hivyo, mstari huo pia unasema “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu.” Jinsi gani? Anajua kila kitu kutuhusu na anaelewa kikamili hisia na udhaifu wetu. Pia, anajua kwamba hatukuzaliwa tukiwa wakamilifu, hivyo tuna mwelekeo wa kufanya makosa. b (Zaburi 51:5) Kwa sababu hiyo, hawakatai wale ambao wanajutia kikweli makosa yao.—Zaburi 32:5.

  •   Usiendelee kufikiria kuhusu makosa yako ya zamani. Biblia ina masimulizi mengi ya wanaume na wanawake ambao walifanya makosa mengi lakini baadaye wakabadili maisha yao. Mfano mmoja ni Sauli wa Tarso, ambaye baadaye alijulikana kama mtume Paulo. Alipokuwa Farisayo, aliwatesa kikatili wafuasi wa Yesu. (Matendo 8:3; 9:1, 2, 11) Lakini alipojifunza kwamba alikuwa akimpinga Mungu na Masihi, au Kristo, alitubu, akabadili njia zake, na akawa Mkristo mzuri sana. Bila shaka, Paulo alihuzunishwa na mwenendo wake wa zamani, lakini hakuendelea kufikiria kuhusu makosa hayo. Kwa kuwa alitambua rehema ambayo Mungu alimwonyesha, Paulo akawa mhubiri mwenye bidii na hakuacha kukazia fikira tumaini la uzima wa milele.—Wafilipi 3:13, 14.

 Mistari ya Biblia kuhusu hatia na msamaha

 Zaburi 51:17: “Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaukataa.”

 Maana: Mungu hatakukataa kwa sababu ya makosa yako ikiwa unajuta kikweli kwamba ulimuumiza. Yeye huonyesha rehema.

 Methali 28:13: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeyote anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.”

 Maana: Tukikubali makosa yetu mbele za Mungu na kubadili njia zetu, atatusamehe.

 Yeremia 31:34: “Nitalisamehe kosa lao, nami sitaikumbuka tena dhambi yao.”

 Maana: Mara tu Mungu anapotusamehe, hatukumbushi kuhusu makosa yetu. Rehema yake ni ya kweli.

a Yehova ni jina la Mungu la kibinafsi.​—Kutoka 6:3.

b Mwelekeo wetu wa kufanya makosa unatokana na dhambi tuliyorithi kutoka kwa mwanamume wa kwanza, Adamu. Akiwa pamoja na Hawa, mke wake, Adamu alimwasi Mungu na kupoteza uhai mkamilifu wa kibinadamu aliokuwa nao na kwa ajili ya wazao wake.—Mwanzo 3:17-19; Waroma 5:12.