Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kileo? Je, Ni Dhambi Kunywa?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kileo? Je, Ni Dhambi Kunywa?

Jibu la Biblia

 Si dhambi kunywa kileo kwa kiasi. Biblia inasema kwamba divai ni zawadi kutoka kwa Mungu ambayo inaweza kufanya maisha yafurahishe. (Zaburi 104:14, 15; Mhubiri 3:​13; 9:7) Pia, Biblia inaeleza kwamba divai ina faida za kitiba.​—1 Timotheo 5:​23.

 Yesu alikunywa divai alipokuwa duniani. (Mathayo 26:29; Luka 7:​34) Katika mojawapo ya miujiza yake inayojulikana sana, Yesu aligeuza maji kuwa divai katika karamu ya arusi.​—Yohana 2:​1-​10.

Hatari za kunywa kupita kiasi

 Ingawa Biblia inataja mambo yanayofaa kuhusu divai, inashutumu kunywa kupita kiasi na ulevi. Hivyo, Mkristo anapoamua kunywa kileo anapaswa kufanya hivyo kwa kiasi. (1 Timotheo 3:8; Tito 2:​2, 3) Biblia inatupatia sababu kadhaa za kuepuka kunywa kupita kiasi.

  •   Kunaathiri uwezo wa kufikiri na kufanya maamuzi. (Methali 23:29-​35) Mtu aliyelewa hawezi kutimiza amri ya Biblia inayosema “mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.”​—Waroma 12:1.

  •   Kunywa kupita kiasi kunamfanya mtu ashindwe kujizuia na ‘kunaondoa kusudi jema.’​—Hosea 4:​11; Waefeso 5:​18.

  •   Kunaweza kumfanya mtu awe maskini na kupata matatizo makubwa ya afya.​—Methali 23:21, 31, 32.

  •   Kunywa sana na ulevi humchukiza Mungu.​—Methali 23:20; Wagalatia 5:​19-​21.

Ni kiasi gani kinachopita kiasi?

 Iwapo mtu anajihatarisha au kuwahatarisha wengine, basi inaweza kusemwa kuwa amekunywa kileo kupita kiasi. Kulingana na Biblia, ulevi haufafanuliwi kuwa kupoteza fahamu tu, bali mtu anaweza kusemwa kuwa amelewa anapoonyesha amechanganyikiwa, akianza kutembea akiyumbayumba, akianza kuwa mbishi, au akizungumza kwa njia isiyoeleweka. (Ayubu 12:25; Zaburi 107:27; Methali 23:29, 30, 33) Hata wale wanaoepuka kulewa wanaweza ‘kulemewa na kunywa sana’ na kupatwa na madhara makubwa.​—Luka 21:34, 35.

Kuepuka kabisa

 Biblia inaonyesha pindi ambazo Wakristo wanapaswa kuepuka kabisa kunywa kileo:

  •   Ikiwa wengine watakwazika.​—Waroma 14:21.

  •   Ikiwa kunywa kileo kunavunja sheria za nchi.​—Waroma 13:1.

  •   Ikiwa mtu hawezi kujidhibiti. Watu ambao ni waraibu wa kileo na wanaotumia kileo vibaya katika njia nyingine wanapaswa kuwa tayari kuchukua hatua thabiti ya kukomesha tatizo lao.​—Mathayo 5:29, 30.