Hamia kwenye habari

Dennis Christensen akiwa mahakamani mwaka wa 2017

MEI 10, 2018
URUSI

Mahakama ya Oryol Yasikiliza Ushahidi wa Kwanza wa Kesi ya Dennis Christensen

Mahakama ya Oryol Yasikiliza Ushahidi wa Kwanza wa Kesi ya Dennis Christensen

Aprili 23, 2018, kesi ya uhalifu ya Dennis Christensen iliendelea katika Mahakama ya Wilaya ya Zheleznodorozhniy iliyoko jijini Oryol. Bw. Christensen, raia wa Denmark na Shahidi wa Yehova, alikamatwa alipokuwa akihudhuria mkutano wa dini mnamo Mei 2017 na amekuwa mahabusu mpaka sasa.

Mwendesha-mashtaka, Bw. Fomin, alimshtaki Bw. Christensen kwa ‘kupanga utendaji wa shirika lenye msimamo mkali,’ yaani, Shirika la Kisheria la Mashahidi wa Yehova (LRO) jijini Oryol, ambalo lilifungwa Juni 2016 kwa mashtaka yasiyo ya haki ya msimamo mkali. Mawakili wa Bw. Christensen wamepinga madai hayo kwa sababu kutaniko la Mashahidi wa Yehova jijini Oryol si shirika la kisheria, bali ni kikundi cha waabudu wenye amani kinachokutana pamoja ili kujifunza Biblia. Mawakili wake wamesisitiza kwamba wenye mamlaka nchini Urusi, kwa maneno yao wenyewe, wamesema kwamba hawakupiga marufuku dini ya Mashahidi wa Yehova na kwamba katiba ya Urusi inahakikisha kuna haki ya kutangaza imani ya dini. a Hivyo, wakati Bw. Christensen aliposhiriki mkutano wa dini alikuwa akitekeleza masuala ya imani yake.

Ushahidi ulianza kutolewa Aprili 24, 2018. Kwanza, mwendesha-mashtaka alimwita ofisa wa Usalama wa Taifa atoe ushahidi. Ofisa huyo alithibitisha kwamba alikuwa ameweka kamera irekodi video kwenye eneo la Jumba la Ufalme la Oryol tangu mwaka wa 2017. Hata hivyo, hangeweza kueleza mambo yaliyokuwa yakifanywa ndani ya jumba, kwa kuwa rekodi hizo zilionyesha Bw. Christensen akisalimiana na wengine kwa uchangamfu walipokuwa wakiingia ndani ya jengo hilo. Kisha, mwendesha-mashtaka alimwita mwanamke ambaye alikuwa amehudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova jijini Oryol. Hata hivyo, mwanamke huyo hakutoa maelezo yoyote kuhusu utendaji wa Bw. Christensen kwa sababu alikuwa amehudhuria mikutano kabla shirika la kisheria jijini Oryol halijafungwa.

Irina Christensen

Siku iliyofuata, mwendesha-mashtaka alimwita mwanamke mwenye umri wa miaka 78, ambaye ni Shahidi wa Yehova, ili atoe ushahidi. Baada ya mwendesha-mashtaka kumuuliza maswali mwanamke huyo kwa saa mbili na nusu kwa kusudi la kupata “uthibitisho,” mwanamke huyo alieleza tu kwamba Mashahidi hawana wasimamizi au viongozi na kwamba wakati wa mikutano yao, hawatumii machapisho ya kidini yaliyopigwa marufuku nchini Urusi.

Kesi hiyo itaendelea kusikilizwa Mei 14, 2018, na imepangwa iendelee kusikilizwa kwa siku kadhaa katika mwezi huu. Akipatikana na hatia, Bw. Christensen anaweza kufungwa miaka sita hadi kumi gerezani. Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wana wasiwasi kwamba inawezekana akafungwa na wanahangaikia hali ya Bw. Christensen na mke wake, Irina.

a Ilipokuwa ikiunga mkono uamuzi wa kupiga marufuku Shirika la Kisheria la Mashahidi wa Yehova la Oryol, Mahakama Kuu ilisema hivi: “Haki ya washiriki wake ya kutangaza dini waliyochagua haitakiukwa, hivyo hawajakatazwa kufanya huduma za ibada kwa uhuru lakini hawapaswi kusambaza machapisho ya kidini yenye msimamo mkali.”