NOVEMBA 22, 2024
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE
Matokeo Mazuri ya Kampeni ya Ulimwenguni Pote ya Kuanzisha Mafunzo ya Biblia Septemba 2024
Septemba 2024, Mashahidi wa Yehova katika nchi 240 walishiriki kwenye kampeni ya pekee ya kuanzisha mafunzo ya Biblia. Ndugu na dada ulimwenguni pote walitumia kila fursa waliyopata kuwaonyesha watu jinsi ya kujifunza Biblia kwa kutumia chapisho Furahia Maisha Milele! Yafuatayo ni masimulizi yenye kusisimua ambayo wahubiri walipata katika mwezi huo wa utendaji wa pekee.
Chile
Nchini Chile, mwanamke mwenye umri wa miaka 30 aliona vigari vya machapisho yetu akiwa kwenye basi. Akiwa kwenye dirisha la basi, alitumia simu yake kusoma alama ya QR kwenye ubao uliokuwa na mwaliko wa kujifunza Biblia bila malipo. Alama hiyo ya QR ilimwongoza kwenye jw.org. Baada ya kusoma makala yenye kichwa “Unaweza Kumtumaini Nani?—Biblia Inasema Nini?” kwenye tovuti yetu, aliomba kutembelewa na Mashahidi. Muda mfupi baadaye, ndugu mmoja na mke wake walimtembelea nyumbani kwake baada ya kupata ombi lake. Aliwaambia wenzi hao wa ndoa kwamba alikuwa akisali kwa Mungu amsaidie ajue jinsi ya kumwabudu kwa njia inayofaa. Walipomwalika ajifunze Biblia alifurahi sana na wakaanza kujifunza papo hapo. Walipokuwa wakijifunza, mwanamke huyo alieleza jinsi anavyofurahia video wanazotazama kwenye funzo. Tayari amemaliza somo la tatu la Furahia Maisha Milele! na anaendelea kujifunza Biblia.
Senegal
Nchini Senegal, mwanamke mmoja aliwasikia dada wawili wakizungumza na mwanamume fulani kuhusu Biblia nje ya nyumba yake. Mwanamke huyo alipendezwa na mambo aliyoyasikia na akawafuata nje ili kuzungumza nao kabla hawajaondoka. Dada hao walizungumzia kuhusu ukosefu wa haki na wakamsomea mwanamke huyo andiko la Isaya 32:16, 17 na pia wakamwonyesha ahadi za Biblia za wakati ujao katika somo la 02 la Furahia Maisha Milele! Mwanamke huyo alianza kulia alipokuwa akiwaeleza kuhusu hali ngumu alizokuwa amekabili maishani. Baada ya kumfariji na kumsomea andiko la 1 Petro 5:7, dada hao walimwalika ajifunze Biblia, naye akakubali mara moja.
Taiwan
Ndugu mmoja alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba nchini Taiwan, alizungumza na mwanamume kijana ambaye alisema alikuwa na wasiwasi kuhusu maisha yake ya baadaye. Ndugu huyo alimsomea andiko la Isaya 65:21, 22 na akamuuliza kijana huyo ikiwa angependa kuishi kwenye dunia ambayo kila mtu anafurahia kazi yake. Ndugu huyo alitumia jambo kuu la 4 katika somo la 02 la broshua Furahia Maisha Milele! kumwelezea kuhusu tumaini la wakati ujao ambalo Biblia inatupatia na akamwonyesha jinsi tunavyojifunza Biblia. Kijana huyo alisema kwamba amefurahia mazungumzo hayo na akakubali kujifunza Biblia. Majuma machache baadaye, baba ya kijana huyo alianza kupendezwa na mambo ambayo mwanaye alikuwa akijifunza naye pia akaanza kujifunza. Wote wawili wanajifunza Biblia kwa ukawaida.
Ukrainia
Ndugu zetu walipokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba katika kijiji fulani nchini Ukrainia, walimsomea mwanamume mmoja andiko la Danieli 2:44 na wakamweleza kwamba Ufalme wa Mungu ndiyo serikali pekee ambayo inaweza kusuluhisha matatizo ya wanadamu. Akiwa na furaha, mwanamume huyo aliwaeleza ndugu hao kwamba yeye husoma Biblia na ana maswali mengi. Alisema kwamba alikuwa akisubiri Mashahidi wamtembelee na hata alikuwa amejaribu kutafuta Jumba la Ufalme karibu na nyumbani kwake. Akina ndugu walimweleza kwamba kujifunza Biblia kutamsaidia kupata majibu ya maswali yake, na wakamwonyesha jinsi tunavyojifunza Biblia. Mwanamume huyo alikubali funzo na sasa anafurahia kujifunza Biblia kwa ukawaida.
Tunafurahia kusikia mambo haya yenye kusisimua ambayo wahubiri walipata katika kampeni ya ulimwenguni pote. Tunamshukuru Yehova kwa kubariki jitihada za ndugu na dada zetu za kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu wajifunze kumhusu yeye na Neno lake.—1 Wathesalonike 2:13.
Picha zifuatazo zinaonyesha ndugu na dada zetu kutoka nchi mbalimbali wakishiriki kwa furaha katika kampeni ya pekee ya kuhubiri ya Septemba 2024.
Bulgaria
Chile
Ugiriki
Iceland
Filipino
Rwanda
Marekani
Zimbabwe

